MZAZI MKANYE MWANAO TUMEJIPANGA ASEMA WAZIRI KATAMBI
Waziri wa Mambo ya Ndani, Patrobas Katambi, ametoa onyo kali na la mwisho kwa watu wanaopanga kufanya maandamano yasiyo rasmi na kuwataka wazazi nchini kuwakanya watoto wao mapema ili wasiingie kwenye mkumbo wa ushawishi utakaowaponza.
Akizungumza wakati alipotembelea Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Katambi alisisitiza kuwa vyombo vyuote vya ulinzi na usalama vimejipanga kikamilifu kila maeneo kuwakabili wale wote watakaojaribu kuvunja amani ya nchi.
Aliongeza kuwa jinai hailipi na wala haiozi, hivyo hata mtu akifanya uhalifu leo na kukimbilia nje ya nchi, mkono wa sheria utamfikia na kumkamata wakati wowote.
Kiongozi huyo amewahakikishia Watanzania kuwa hakuna tishio lolote la usalama litakaloruhusiwa kuvuruga utulivu wa nchi, akibainisha kuwa serikali haiwezi kupangiwa tarehe na hakuna mtu yeyote aliye juu ya sheria.
Alifafanua kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi ya mhalifu yeyote atakayetishia usalama, kwani mkakati uliopo ni kuimarisha ulinzi ili kuhakikisha raia wanaenda kwenye shughuli zao za kiuchumi na wanafunzi wanaenda shule bila hofu.
Katambi ameweka wazi kuwa kwa sasa Tanzania si salama tena kwa wahalifu wa aina yoyote na kwamba nchi itaendelea kulindwa kwa nguvu zote.
Kuhusu utaratibu wa kisheria, Katambi alikumbusha kuwa miongozo ya maandamano na mikusanyiko yote imeainishwa wazi kwenye sheria za nchi, hivyo hakuna anayepaswa kutumia vibaya ustahimilivu wa serikali kufanya vurugu.
Pia, alitoa onyo maalum kwa watu wanaotumia mitandao ya kijamii kurusha na kusambaza maudhui yenye viashiria vya kuvunja amani, akitaka vitendo hivyo vikome mara moja. Amesitiza kuwa serikali itasimama kidete kulinda amani iliyoachwa na waasisi wa taifa na haitasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayebainika kukiuka maelekezo hayo.

Post a Comment