JWTZ:OLE WAO WATAKAOJARIBU KUVURUGA AMANI
JESHI la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limetoa
msimamo mkali kuhusu hali ya amani nchini na kuwataka wananchi kupuuza wito
wowote unaohamasisha vurugu na uvunjifu wa amani, likisisitiza kuwa litaendelea
kutekeleza wajibu wake wa kulinda nchi, katiba na mamlaka ya dola kwa mujibu wa
sheria.
Taarifa hiyo ilitolewa jana na Mkuu wa Uhusiano wa
JWTZ, Luteni Kanali Sylvester Mangure kutoka makao makuu ya jeshi aliyesema hali
ya usalama nchini na katika mipaka ya Tanzania inaendelea kuwa shwari, jambo
lililowezesha wananchi kuendelea na shughuli zao za kila siku za kujenga uchumi
na maendeleo ya taifa.
Mangure aliwapongeza wananchi kwa kuendelea
kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama katika kudumisha amani na utulivu,
huku akibainisha kuwa ushirikiano huo umechangia kuendelea kuwepo kwa mazingira
salama nchini.
Hata hivyo, alisema kuna watu wasioitakia mema nchi
wanaoendelea kuhamasisha na kupotosha wananchi kushiriki katika vitendo vya
vurugu na uvunjifu wa amani, huku wakilihusisha JWTZ kwa madai yasiyo ya kweli
kwamba litawalinda watakaoshiriki katika vitendo hivyo.
Alisema vurugu na ghasia zinazohamasishwa zinaweza
kusababisha madhara makubwa kwa washiriki na wananchi wengine wasiokuwa na
hatia, ikiwemo kupoteza maisha, kujeruhiwa, kuharibika kwa mali, kuvurugika kwa
shughuli za uzalishaji na kuathiri uchumi wa Taifa.
Kutokana na hali hiyo, JWTZ limewataka wananchi
kuendelea na shughuli zao za kila siku bila hofu na kupuuza wito wowote
unaochochea vurugu, likisisitiza kuwa halitasita kuchukua hatua za kisheria
dhidi ya mtu yeyote atakayeshiriki katika vitendo vya uvunjifu wa amani.
Mangure alifafanua kuwa kwa mujibu wa Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, JWTZ ina wajibu wa kulinda usalama wa nchi na
wananchi na pia lina mamlaka ya kusaidia mamlaka za kiraia wakati wa vurugu,
ghasia au matukio mengine ya uvunjifu wa amani pale litakapohitajika kufanya
hivyo kwa mujibu wa sheria.
Aliwahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo
vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa kwa viongozi wa vijiji, mitaa na
mamlaka husika endapo watabaini viashiria vya uchochezi au vitendo vinavyoweza
kuhatarisha amani na utulivu wa nchi.
Mangure aliwahakikishia wananchi kuwa JWTZ itaendelea
kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii, uaminifu na uhodari, kwa kuzingatia
viapo walivyoapa, huku likiendelea kushirikiana na wananchi pamoja na vyombo
vingine vya ulinzi na usalama kulinda amani, utulivu, umoja na maendeleo ya taifa.

Post a Comment