Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Friday, July 26, 2024

Kokteli ya Jack Daniel’s na Coca-Cola katika kopo yazinduliwa Dar





Brown-Forman Corporation  na  Kampuni ya Coca-Cola wameingiza mtaani kitu kipya  ambacho ni kileo kilicho tayari kwa kunywekwa (ARTD) .

Kinywaji hicho ambacho ni mchanganyiko wa Jack Daniel’s na Coca-Cola, ni kionjo kikamilifu cha kufurahia wakati mzuri na marafiki. 

"Tunafurahi kuleta Jack Daniel’s na Coca-Cola kwenye soko la Afrika na kuwapa watumiaji njia mpya na ya kusisimua ya kufurahia mchanganyiko wa chapa zetu mbili za kipekee," alisema Peter Orfanidis, Meneja wa Kanda wa Brown-Forman.

"Tunapoendelea kusikiliza wateja kupitia bidhaa zetu mpya na kupanua upatikanaji wa Jack Daniel’s na Coca-Cola duniani kote, tunafurahi kuanzisha kinywaji hiki kilichohamasishwa na moja ya kokteili maarufu zaidi duniani. 

"Bidhaa hii mpya inaonyesha kujitolea kwetu kuleta uzoefu bora wa ladha kwa watumiaji katika muundo rahisi wa kuwa tayari kunyweka," aliongeza Natasha Chetty, Mkurugenzi Mtendaji wa Bidhaa mpya katika kampouni ya Coca-Cola Afrika.

Kuingizwa mtaani kwa kinywaji hiki kunaonyesha dhamira ya dhati ya kampuni ya Coca-Cola ya kuwafanya wateja wake kuwa na furaha muda wote kwa kuwa na bunifu mbalimbali za kuwaburudisha.

Imeelekezwa kuwa baada ya kuzinduliwa kwa mafanikio katika masoko zaidi ya 25 duniani kote yakiwemo ya Marekani, Mexico, na Japan kinywaji cha Jack Daniel’s na Coca-Cola ARTD sasa kimefika Dar es salaam katika bara la Afrika.

Wataalamu wa vileo wamekiri kuwa ubunifu huu mpya utawapa watumiaji watu wazima wa Afrika fursa ya kufurahia ladha ya kipekee ya kokteili hii maarufu ya baa katika muundo rahisi wa kuwa tayari kunywekwa. 

Uzinduzi ulijumuisha aina mbili za vinywaji yaani, Jack Daniel’s na Coca-Cola ya asili, na toleo la Coca-Cola Zero Sugar, ili kukidhi mapendeleo tofauti ya watumiaji.

Msemaji wa Coca-Cola Company akizungumza katika uzinduzi alisema kampuni yake inaelewa jukumu lake muhimu katika kukuza kunywa kwa uwajibikaji miongoni mwa wale waliofikisha umri wa kisheria wa kunywa, na itafuata Sera yake ya Uuzaji wa Pombe kwa Uwajibikaji inayoongoza katika sekta hiyo. 

"Watumiaji wanaweza kutarajia kuona alama wazi za uwajibikaji kwenye kopo na ufungaji, ukisisitiza ujumbe kwamba kinywaji kinapaswa kufurahishwa kwa uwajibikaji na watu wazima tu waliofikisha umri wa kisheria wa kunywa," alisema.

Katika awamu ya kwanza baada ya uzinduzi kinywaji hicho kitapatikana katika maduka ya pombe na maeneo yaliyochaguliwa  na itakuwa inapatikana katika makopo ya milimita 300 yenye kiwango cha pombe cha asilimia 5.


Wednesday, July 24, 2024

TIMU YA TAIFA YA MICHEZO YA OLIMPIKI UFARANSA 2024 YAWASILI PARIS


Kundi la kwanza la wachezaji wa Tanzania watakaoiwakilisha nchi katika  Michezo ya Olimpiki limewasili salama asubuhi ya leo Julai 24, 2024 jijini Paris nchini Ufaransa.

Kundi hilo la kwanza lina waogeleaji wawili, Sofia Anisa Latiff na Collins Phillip  Saiboko na mwalimu wao Alexander Harrison Mwaipasi pamoja na Daktari wa timu, Dkt Eliasa Abdallah Mkongo. 

Waogeleaji wataanza kuchuana Agosti 30 mwaka huu, ambapo Collins Phillip Saiboko atashindana katika michuano ya mita 100 Freestyle kwa wanaume huku, Sofia Anisa Latiff atashindana Agosti 3,  katika mita 50 freestyle kwa wanawake.

Mwingine aliyewasili leo Paris ni mwalimu wa mchezo wa Judo, Innocent John Mallya, ambaye mchezaji wake, Andrew Thomas Mlugu (Kg 73), tayari yupo Paris kwa mwaka mmoja katika kambi maalumu ya mazoezi ya CRJ Centre iliyoandaliwa na Kamati ya Olimpiki ya Kimataifa (IOC) na ataanza kuingia dimbani Agosti 2 mwaka huu.

Wanamichezo wanne, ambao wote ni wakimbiaji wa Marathon, bado wako kambini Jijini  Arusha wakiendelea kujifua na wanatarajiwa kuwasili Paris Augosti 7 na Marathon itakuwa Agosti 11, 2024.

Wanariadha hao wa marathon ni wanaume Alphonce Felix Simbu na Gabriel Geay, na wanawake ni  Jackline Juma Sakilu na Magdalena Crispin Shauri.

KCB EAST AFRICA GOLF TOUR KUFANYIKA LUGALO

 



SHINDANO la wazi la mchezo wa gofu (KCB EAST Africa Golf tour) linatarajiwa kufanyika Agosti 3 mwaka huu katika Viwanja vya Lugalo Dar es Salaam.

Akizungumza Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wa klabu ya Lugalo, Brigedia Jenerali mstaafu, Michael Luwongo alisema shindano hilo litashirikisha wachezaji 150 kutoka nchi mbalimbali na klabu za hapa nchini.

Luwongo alisema lengo ni kupata timu ya wachezaji wanne watakaokwenda kushiriki mashindano Nairobi, Kenya Desemba 6 mwaka huu.

"Maandalizi ya shindano hili yanaendelea vizuri, mpaka sasa tunaendelea kuboresha miundombinu ya viwanja vyetu ili shindano lifanyike kwa weledi” alisema Luwongo.

Pia aliipongeza Benki ya KCB kwa udhamini wao na kuwataka wale ambao hawajathibitisha ushiriki wao wafanye haraka muda umeisha.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa KCB, Cosmas Kimario alisema benki hiyo inatoa huduma kwa jamii pamoja na michezo mbalimbali ikiwemo riadha, mpira wa miguu na ngumi.

"Tuna uhakika hii timu itakayokwenda Kenya itafanya vizuri na kurudi na ushindi nyumbani, ili fainali ijayo ifanyika hapa nchini, alisema Kimario.

Alisema wameamua kuwekeza katika michezo kwa lengo la kukuza vipaji vya vijana wadogo wanaochipukia.

Naye nahodha wa klabu ya Lugalo, Meja Japhet Masai alisema shindano hilo litachezwa kwa mfumo wa kuhesabu mashimo kwa pointi na atakayepata pointi nyingi atapata nafasi ya kwenda Kenya.

SIMBA YAMCHUKULIA KIBU MTORO KAZINI

 

UONGOZI wa Simba umesema kitendo cha mshambuliaji Denis Kibu kutokuwepo kambini hakiathiri mipango yao ila watamchukulia hatua za kinidhamu kwa kosa hilo.

Kauli hiyo imetolewa na Meneja wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally Morogoro leo walipokwenda kuzindua jezi mpya za msimu ujao.

Kibu aliongezewa mkataba wa miaka miwili utakaomalizika Juni 2026 na kulipwa stahiki zake za kimkataba jambo ambalo hata meneja wake Carlos Mastermind amekiri mchezaji huyo haidai Simba.

Ahmed alisema kutokuwepo kwa Kibu hakuathiri programu za Kocha Mkuu Fadlu Davis kwa sababu wamefanya usajili kulingana na mahitaji ya timu.

“Kibu hadi sasa hajaungana na timu nchini Misri. Tulimuongeza mkataba wa miaka miwili na amesaini kuitumikia Simba, tumemlipa fedha zote na mahitaji yote aliyohitaji. Amelipwa kama kondakta, fedha alikabidhiwa mkononi na kuondoka, hatuna deni na mchezaji bali Simba inamdai utumishi wake,” alisema Ahmed.

Pia alisema baada ya kumaliza ligi alienda Marekani lakini walimpa taarifa ya kambi, kupima afya na safari ya Misri, baadaye alisema hati ya kusafiria imejaa.

“Kweli alirudi na kufuatilia hati yake lakini hakutokea ofisini kwa ajili ya safari, alipotafutwa apeleke hati yake akasema ameenda Kigoma, baada ya hapo zikaanza danadana za hapa na pale, tutaendelea kumtafuta lakini jana tulisikia ameenda nje ya nchi,” alisema Ahmed.

Tetesi zinasema Kibu amevutiwa na Yanga na anaweza kutambulishwa Siku ya Wananchi itakayofanyika Agosti 4 Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Endapo atasajiliwa Yanga haitakuwa ajabu kwani meneja wake Carlos pamoja na kukiri Simba kumlipa stahili zote alidai Yanga ndio waliotoa dau kubwa.

Hata hivyo Carlos anasema mchezaji huyo amepata mwaliko wa moja ya klabu nchini Norway.

“Ni kweli Kibu hajajiunga na timu Misri kwa sasa yupo Ulaya, ninachojua hawadai Simba wamemalizana na suala la kwanini hajajiunga na wenzake nchini Misri, Simba wana uwezo wa kujibu hilo,” alisema Carlos.

AZIZI KI, FEI TOTO WAKABANA KOO TUZO ZA TFF

 

Fei Toto

Aziz Ki

TUZO ya mchezaji bora wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2023/2024 imeonekana kuwa na ushindani baada ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kutoa orodha ya wachezaji wanaowania tuzo mbalimbali.

Katika tuzo hizo zitakazotolewa Agosti 1, mwaka huu Masaki, Dar es Salaam kipengele cha mchezaji bora kinawaniwa na wachezaji wanane ambao ni Stephane Aziz Ki, Feisal Salum ‘Fei Toto’, Kipre Jr. Djigui Diarra, Ley Matampi, Yao Kouassi, Ibrahim Bacca na Mohamed Hussein ‘Tshabalala’.

Katika kipengele cha kipa bora wa Ligi Kuu Tanzania Ayoub Lakred, Djigui Diarra na Ley Matampi kwa upande wa mabeki ni Yao, Bacca na Tshabalala, tuzo ya kiungo bora Aziz Ki, Fei Toto na Kipre Jr, kocha bora ni David Ouma, Bruno Ferry na Miguel Gamondi.

Aziz Ki huenda akatwaa tuzo zaidi ya moja kwa sababu tayari tuzo ya mfungaji bora wa Ligi Kuu ni yake kwa kuwa anaongoza kwa kufunga mabao 21.

Pia Fei Toto ana nafasi nzuri ya kuondoka tuzo, kwani alikuwa na msimu bora na alimaliza ligi akishika nafasi ya pili katika ufungaji wa mabao akiweka kambani mabao 19.

Aidha tuzo zilijumuisha mashindano yote yaliyochini ya TFF kuanzia Ligi Kuu zote kwa maana ya wanawake na wanaume, Championship, First League, soka la ufukweni, Kombe la Shirikisho na Ligi ya Vijana ya U20.

Kadhalika kutakuwepo na tuzo ya mchezaji bora anayecheza nje ya nchi wa kiume na wanaowania ni Mbwana Samatta, Himid Mao na Novatus Dismas na kwa wanawake wapo Opa Clement, Clara Luvanga na Aisha Masaka.

SIMBA YAZINDUA JEZI ZA MSIMU 2024/2025

 




UZINDUZI wa wiki ya Simba na jezi zinazotumika kwa msimu ujao umefanya mji wa Morogoro uliopambwa na milima kuwa rangi nyekundu na nyeupe baada ya mashabiki wat imu hiyo kuwasili.

Safari ilianzia Dar es Salaam saa 12:00 alfajiri kwa kutumia Reli ya Kisasa ya kimataifa (SGR), na kuwasili stesheni ya Morogoro saa 1:30 ikiwa na mashabiki na wananchama wa Simba wakiongozwa na Ofisa Mtendaji wa klabu hiyo Imani Kajula na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Ahmed Ally.

Jezi zitakazotumika msimu huu zilizinduliwa kwenye hifadhi ya Mikumi ambazo ni bluu, nyekundu na nyeupe baada ya msimu uliopita kuzinduliwa kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro.

Msafara huo ulifika Mikumi saa 8:30 ambapo pia kulikuwa na mchezo wa kirafiki kati ya wafanyakazi wa hifadhi hiyo na viongozi wa Simba.

Ahmed alimtambulisha mwanamuziki wa kizazi kipya, Ali Kiba kuwa ndiye atatumbuiza kwenye Simba Day itakayofanyika Agosti 3, mwaka Uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam ikiwa ni msimu wake wa pili kutumbuiza.

Simba ambayo iko kambini Misri siku hiyo itacheza mchezo wa kirafiki na APR ya Rwanda, kabla ya kucheza nusu fainali ya Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga, Agosti 8, mwaka huu.

Imani Kajula, alisema wamefanya uzinduzi wa Wiki ya Simba katika mbuga ya Mikumi kwa ajili ya kutangaza utalii.

Viingilio vya kilele cha Simba Day, mzunguko ni Sh 5000, rangi ya chungwa Sh 10,000, VIP C, Sh 20,000, B Sh 30,000, A Sh 40,000 na Platinum Sh 200,000.

DUBE AIBEBA YANGA

 



YANGA imepata ushindi wa kwanza wa michuano ya Kombe la Mpumalanga baada ya kuafunga wenyeji wao Tx Galaxy kwa bao 1-0 katika Uwanja wa Mbombela, Afrika Kusini leo

Bao pekee katika mchezo huo lilifungwa na Prince Dube dakika ya 55 lakini pia Galaxy walipata penalti dakika ya 73, wakakosa.

Kwa matokeo hayo Yanga ina pointi tatu sawa na Augsburg ya Ujerumani ambao walishinda 2-1 dhidi ya Yanga.

Usajili mpya wa Yanga unaonekana kuwa na tija kwani mabao katika michezo yaote yamefungwa na Jean Baleke ambaye amesajiliwa kwa mkopo kutoka TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Dube kutoka Azam FC.

Yanga wanatumia michuano hiyo kama sehemu ya matayarisho ya msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara na mashindano ya kimataifa.

Yanga watakamilisha ziara yao nchini humo kwa kuikabili Kaizer Chiefs kwenye michuano ya Kombe la Toyota Julai 28 mwaka huu na wanatarajia kurejea nchini Julai 30 kwa maandalizi ya Kilele cha Wiki ya Mwanachi, Agosti 3, mwaka huu.

Mwisho