WAZEE TAIFA WAIBARIKI RIPOTI YA TUME YA CHANDE, WAUNGA MKONO UCHUNGUZI WA JINAI
BARAZA la Ushauri la Wazee Taifa limepongeza ripoti ya Tume
ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, wakisema
imeweka wazi ukweli na kutoa mwelekeo wa kudumisha amani nchini.
Akizungumza mjini Bariadi, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mzee
David Sendo alisema tume hiyo imefanya kazi ya kina, yenye kuzingatia haki bila
upendeleo, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wa kuunda
chombo hicho.
Alisema ripoti imegusa maeneo muhimu, ikiwemo kubaini kuwa
baadhi ya kaulimbiu za kisiasa zilichangia kuchochea vurugu wakati wa uchaguzi
wa Oktoba 29, 2025.
Sendo alisisitiza umuhimu wa vyama vya siasa kujitathmini
upya kuhusu lugha na kaulimbiu wanazotumia, akionya kuwa maneno yasiyo na
tahadhari yanaweza kuleta taharuki badala ya kujenga mshikamano wa kitaifa.
Alivitaka vyama kuelekeza nguvu katika hoja zenye manufaa
kwa wananchi na zinazolinda amani, hasa kwa kuzingatia mazingira ya sasa ya
teknolojia. Kuhusu pendekezo la kuundwa kwa tume ya kijinai kuchunguza wahusika
wa vurugu hizo, alisema wazee wanaunga mkono hatua hiyo kwa asilimia 100 ili
kuhakikisha waliohusika wanabainika na kuchukuliwa hatua stahiki.
Aidha, alipongeza juhudi za serikali kuwahudumia waathirika
wa vurugu hizo, akisisitiza umuhimu wa kuwajumuisha pia wafanyabiashara wadogo
waliopoteza mitaji yao ili waweze kurejea kwenye shughuli zao.
Wakati huo huo, wakazi wa Mwanza waliizungumzia ripoti hiyo
na kuipongeza kwa kubaini ukweli, tofauti na taarifa zilizokuwa zikisambazwa
awali na kusababisha taharuki katika jamii.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Machifu Tanzania, Mtemi Nyamironda
III Aaron Mikomangwa alisema ripoti hiyo imeleta majibu sahihi kuhusu matukio
ya vurugu, akiwataka wanasiasa kuepuka kauli zinazochochea hofu na badala yake
kuheshimu matokeo ya tume.
Kwa upande wake, mkazi wa Mwanza, Mary Libaba alisema
kuwekwa wazi kwa ukweli kumesaidia kutoa uelewa sahihi kwa wananchi, akionya
kuwa wanaopinga ripoti hiyo wanaweza kuwa na nia isiyo njema.

Post a Comment