KOMBE LA DUNIA: Pumziko Fupi Kabla ya Historia Kuandikwa



Baada ya michezo 96 na siku 26 mfululizo za soka la Kombe la Dunia, sasa tunapata mapumziko ya siku moja huku kukiwa na timu nane pekee zilizosalia ambazo zimegawanyika sawa pacha. 

Upande mmoja kuna mataifa ambayo yameshawahi kuonja ladha ya ubingwa huko nyuma, na upande mwingine ni timu ambazo hazijawahi hata kufika fainali, huku mbili kati yao zikiwa hazijawahi hata kugusa hatua ya nusu fainali. 

Kila mchezo wa robo fainali unakutanisha timu kutoka pande hizi mbili, huku timu nane hizi zote zikiwa na uwezo wa kuandika historia kubwa, lakini swali la msingi si nani atashinda au nani anastahili, bali ni bingwa yupi ambaye ushindi wake utaendelea kuzungumzwa kwa miongo mingi ijayo badala ya kusahaulika kwenye kurasa za historia.

Kila timu ina sababu zake nzito za kuifanya iache alama isiyofutika ambapo kwa kuanza na Argentina, wakitwaa ubingwa watakuwa taifa la tatu pekee kutetea taji hilo, na kwa kuwa walifika fainali pia mwaka 2014, kizazi hiki kitaonekana kama cha utawala wa kipekee wa soka. 

Lionel Messi atakuwa bingwa mara mbili miaka michache tu baada ya kuonekana kama angemaliza soka lake bila kikombe hiki kikubwa, jambo ambalo bila shaka litamaliza mjadala wa nani mchezaji bora wa muda wote duniani. 

Kwa upande wa Ufaransa au Uhispania, ushindi kwa yeyote kati yao utaimarisha hadhi yao kama timu inayotawala soka la Ulaya kwa kizazi kizima, ambapo Ufaransa itafikisha taji la tatu la Kombe la Dunia na kucheza fainali tatu mfululizo huku Uhispania ikitwaa taji lake la pili la dunia ndani ya miaka ya hivi karibuni sambamba na mataji matatu ya Ulaya. Kwa Uingereza, bingwa mwingine wa zamani aliyesalia, kutwaa taji hili la pili itakuwa hatua kubwa ya kisaikolojia kwani tangu mwaka 1966 wamekuwa wakihangaika kushinda kitu chochote, na miaka 30 ya maumivu yaliyolambwa wimbo mwaka 1996 sasa imetimia miaka 60, hivyo ushindi utawabadilisha kutoka timu inayojivunia mafanikio ya kale hadi kuwa timu ya mafanikio ya sasa.

Tukiachana na mabingwa hao wa zamani, mataifa ya Ulaya yaliyosalia ambayo ni Ubelgiji, Norway, na Uswisi yatakuwa mfano bora wa mipango mizuri na uwekezaji kwenye miundombinu ya soka. Mataifa haya yanashika nafasi za nyuma sana duniani kwa idadi ya watu, na hata ukiyajumlisha yote hayataingia kwenye mataifa 50 yenye watu wengi zaidi, hivyo kubeba kombe hili kutathibitisha kuwa mafanikio makubwa yanaweza kupatikana kwa mipango madhubuti, roho ya timu, na uchawi kidogo kutoka kwa miungu ya soka. 

Mwisho kabisa lakini kwa umuhimu mkubwa kuna Morocco ambao mnamo mwaka 2022 waliandika historia kwa kuwa taifa la kwanza la Afrika kufika nusu fainali, na kutwaa ubingwa safari hii kunaweza kuwa kama kuvunja mwiko wa jambo lililodhaniwa kuwa haliwezekani na kulifanya liwezekane kwa wengi. 

Ushindi wa Morocco utayapa mataifa ya Afrika lengo halisi la kufikia badala ya kuamini kuwa kufanya vizuri ni muujiza, na michezo hii minane ijayo itatengeneza mustakabali mzima wa soka la baadaye.

No comments