WATANZANIA WATAKIWA KUTOKUBALI KURUDISHWA NYUMA KUSAKA AMANI NA UTULIVU

 



Siku moja baada ya kutolewa kwa ripoti ya Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2025, hali ya usalama nchini imeendelea kuwa shwari huku wananchi wakitekeleza majukumu yao ya kila siku kama kawaida.

Mamilioni ya Watanzania waliofuatilia uwasilishwaji wa ripoti hiyo na mapendekezo yake wameonesha kuwa na matumaini makubwa ya kusonga mbele, wakigubikwa na hisia za kuumizwa na ghasia zilizojitokeza kipindi hicho lakini wakiwa na dhamira ya kutorejea huko tena.

Hata hivyo, vyama vikuu vya upinzani nchini, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na ACT Wazalendo, vimejitokeza hadharani kuipinga kazi iliyofanywa na Tume hiyo kupitia matamko yao kwa umma.

Pamoja na malalamiko hayo, uchambuzi wa kina unaonesha kuwa hoja zinazotolewa na vyama hivyo ni dhaifu ikilinganishwa na mustakabali wa Taifa na ukweli wa madhara yaliyopatikana, hasa ikizingatiwa kuwa hali ya nchi ilikuwa shwari kabla ya kupandikizwa kwa mbegu za chuki na chokochoko za ghasia zilizoratibiwa takribani miezi sita kabla ya uchaguzi.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya uchunguzi, ghasia hizo zilipangwa na kufadhiliwa na watu waliopata mafunzo maalumu, jambo ambalo limewafanya Watanzania walio wengi kutamani kurejea kwenye amani yao ya asili na kukataa kutumika kama nyenzo ya wanasiasa kwa maslahi binafsi.

CHADEMA inadai kuwa Tume hiyo si chombo huru kwa madai kuwa imeundwa chini ya Sheria ya Uchunguzi ya mwaka 2002 inayompa Rais mamlaka ya kuiongoza, lakini ufafanuzi wa kisheria unaonesha kuwa Tume ina kinga na uhuru wa kufanya kazi bila kuingiliwa, ikiwa na mamlaka sawa na Mahakama Kuu katika kukusanya ushahidi.

Upande wa ACT Wazalendo nao umetoa hoja zinazofanana na hizo ukidai Tume iliundwa kulinda wahusika, hoja ambayo inakosa mashiko kwani ripoti imegusia masuala ya uwajibikaji kwa uwazi.

Vyama hivi vinaonekana kuyumba baada ya mikakati yao kutofua dafu, huku uamuzi wao wa kususia mchakato wa Tume ukiwanyima fursa ya kusikilizwa .Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mohamed Chande Othman, alieleza kuwa zaidi ya watu 63,000 walifika kutoa ushahidi ilikuwa ni fursa kwa kila mwananchi kushiriki.

Kwa sasa, huku wawakilishi wa taasisi za kimataifa kama Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya Madola wakiahidi kushirikiana na Tanzania katika hatua hii, ni dhahiri kuwa hoja za kupuuza mchakato wa ndani hazina msingi imara.

Ni muhimu kwa Watanzania kuendelea kuwa macho na kuwakataa wanasiasa wanaojaribu kuwatumia kwa maslahi yao, ili kuhakikisha kuwa changamoto na machungu yaliyopita hayajirudii tena katika historia ya nchi yetu.

 

No comments