RAIS DKT. SAMIA ASISITIZA ULINZI WA MIUNDOMBINU YA MAWASILIANO AKIZINDUA MINARA 758 DODOMA
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia
Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu wa kulinda miundombinu ya mawasiliano nchini
akiitaja kama rasilimali ya kimkakati kwa ajili ya uchumi na usalama wa taifa.
Katika hotuba yake, Rais amewataka wananchi na
mamlaka husika kuhakikisha miundombinu hiyo inatunzwa, huku akiagiza usimamizi
wa huduma za mawasiliano uzingatie maadili, mila, na utamaduni wa Mtanzania.
Agizo hilo limetolewa leo wakati wa hafla ya uzinduzi
wa minara 758 ya mawasiliano na maunganisho ya Mkongo wa Taifa katika wilaya 85
nchini, iliyofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani
Dodoma.
Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Samia
ameshuhudia makabidhiano ya miundombinu hiyo kwa Serikali na kubainisha kuwa
uwekezaji huo ni nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa kidigitali, hususan
maeneo ya vijijini na mipakani.
Rais
Dkt. Samia ameeleza kuwa dunia inabadilika kwa kasi na
mawasiliano si huduma ya anasa tena, bali ni msingi wa uchumi wa kisasa
utakaofungua fursa za ajira na ubunifu kwa vijana.
Aidha, Mheshimiwa Rais amezitaka halmashauri zote
nchini kuondoa urasimu katika utoaji wa vibali vya miradi ya mawasiliano ili
kuepuka kuongeza gharama za uwekezaji na kuchelewesha huduma kwa wananchi.
Kwa
upande wake, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah
Kairuki, amebainisha kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano kati ya
Serikali na sekta binafsi.
Post a Comment