MJUMBE MAALUMU WA AU, KIKWETE AREJESHA MATUMAINI SUDAN KUSINI
Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na
Bahari ya Sham, Rais mstaafu wa Tanzania, Dkt. Jakaya Kikwete amekutana na Rais
Salva Kiir kujadili utekelezaji wa Mkataba wa Amani wa mwaka 2018 (R-ARCSS).
Katika mazungumzo hayo, Rais Kiir alisisitiza kuwa mchakato wa amani
unaendelea, huku serikali ikiendeleza juhudi za majadiliano jumuishi
yanayohusisha pande zote, ikiwemo pande ambazo hazijasaini makubaliano hayo.
Lengo kuu, amesema Rais Kiir, ni kufikia mwafaka wa kitaifa kabla ya
uchaguzi uliopangwa kufanyika Desemba 2026, ambao utakuwa wa kwanza tangu nchi
hiyo ipate uhuru mwaka 2011.
Lakini
ziara ya Kikwete haikuishia tu ndani ya kuta za serikali. Akiwa na dhamira ya
kuhakikisha sauti ya kila mmoja inasikika, alikutana na viongozi wa vyama vya
upinzani, asasi za kiraia, viongozi wa kidini na wasomi. Dk Kikwete alifanya mashauriano na vyama vya
siasa kama SPLM-IG, SPLM-IO na SSOA, pamoja na asasi za kiraia, viongozi wa
dini na wanazuoni.
Mkakati huo jumuishi umepongezwa na
wadau wengi wa amani, akiwemo mwanaharakati mashuhuri Edmund Yakani, aliyesema
kuwa uzoefu wa Kikwete katika upatanishi ni nyenzo muhimu itakayosaidia
kuwaleta watu wote kwenye meza ya mazungumzo, hata wale wenye mitazamo tofauti.
Uzito wa ziara hii unachochewa na
historia ya Kikwete nchini humo. Mwaka 2015, yeye ndiye aliyekuwa kiungo muhimu
katika kufanikisha Makubaliano ya Arusha yaliyowatunanisha wanachama wa SPLM.
Kabla ya kutua Juba, Kikwete
alishafanya mazungumzo na marais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini na Yoweri
Museveni wa Uganda, ambao ni wadhamini wakuu wa amani ya Sudan Kusini. Hatua
hizi zinaashiria kuwa Umoja wa Afrika sasa umejipanga dhabiti kuivusha nchi
hiyo kutoka kwenye misukosuko na kuingia katika kipindi kipya cha neema na
utulivu.

Post a Comment