MSIGWA: TUNAJALI NA TUMEJIPANGA USALAMA MAJINI
Katika kuhakikisha
kuwa ukuaji wa uchumi wa majini unaenda sambamba na usalama wa maisha ya
wananchi, Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika mifumo ya uokoaji na
mawasiliano katika Maziwa Makuu.
Msemaji wa Serikali,
Gerson Msigwa, amebainisha kuwa ujenzi wa Kituo Kikuu cha Uratibu wa Masuala ya
Utafutaji na Uokozi (MRCC) katika Ziwa Victoria umefikia asilimia 98, huku
vituo vidogo vitatu vya uokoaji (SAR) vikijengwa Kanyara (91%), Ukerewe (85%),
na Musoma (91%).
Hatua nyingine ni
ununuzi wa boti maalum ya wagonjwa (Ambulance Boat) kwa ajili ya Ziwa Victoria,
ambayo tayari imewasili na iko tayari kutoa huduma kama hospitali inayotembea
majini.
Gharama za usalama
pia zimehusisha ununuzi wa boti nyingine nne za uokoaji zilizosambazwa katika
Ziwa Tanganyika, Victoria, na Ukanda wa Bahari ya Hindi (Tanga) ili kuimarisha
uwezo wa kukabiliana na majanga.
Pamoja na miundombinu
hiyo, serikali inaendelea na ujenzi wa minara mitatu ya mawasiliano katika
visiwa vya Soswa (50%), Kunene (50%), na Kweru (70%) ndani ya Ziwa Victoria ili
kuimarisha tahadhari za hali ya hewa na uratibu wa dharura.
Kwa ujumla, msemaji
huyo wa serikali amesema uwekezaji huo wa zaidi ya shilingi trilioni moja
katika sekta nzima unalenga kuhakikisha usafiri wa majini unakuwa salama na wa
kisasa.
Hii inatoa uhakika
kwa wasafiri na wafanyabiashara, jambo linalochochea watu wengi zaidi kutumia
usafiri wa majini bila hofu ya usalama wa maisha yao.
Post a Comment