Milioni 432 kujenga kituo cha taaluma cha Edward Mpogolo Dar
HALMASHAURI ya Jiji la Dar es Salaam, imetenga kiasi cha Sh.milioni 432 kujenga kituo cha umahili taaluma kitakacho fahamika kama Edward Jonas Mpogolo Center for Excellence Capacity Building.
Hayo yameelezwa katika hafla ya utangazaji matokeo ya mitihani ya ndani na utoaji wa tuzo kwa wanafunzi na shule za sekondari zilizofanya vizuri katika mitihani hiyo kwa kidato cha kwanza cha pili cha tatu na cha sita, jiji Dar es Salaam.Aidha shule za sekondari zilizofanya vibaya zilikabidhiwa vinyago maalumu vya mpingo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam,Elihuruma Mabelya, alisema tayari Halmashauri imetenga Sh milioni 219 za ujenzi wa kituo hicho ambacho kimepewa jina la mkuu huyo wa wilaya kwa kutambua mchango wake katika maendeleo hususan elimu.
" Kituo hiki kitakapo kamilika kitasaidia kuboresha usimamizi wa mitihani,umahili wa walimu na tutatengeneza mfumo kama wa wenzetu wa Baraza la Mitihani la Taifa (NACTE) kwa ajili ya mitihani yetu ya ndani," alisema Mabelya.
Alieleza halimashauri hiyo inahitaji kufanya jitihada kubwa kuongeza ufaulu na kujiandaa kupokea wanafunzi 89,782 wa double cohort mwaka 2028.
" Hivyo basi tunaamini kituo hiki kikakamilika kitatusaidia Ilala hata kuingia katika tatu bora ya matokeo ya mitihani kitaifa.Tunataka kufikia ubora wa asilimi 50 kwa sasa tuko asilimi 35 Kwa ubora wa kawaida,"alieleza Mabelya.
Akikabidhi tuzo hizo, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, alisema, mkakati uliopo katika kuboresha sekta ya elimu ni kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
"Pia kutekeleza maono ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuboresha miumdombinu ya elimu na ubora wa elimu itakayo mwezesha mhitimu kupata taaluma yenye tija," alisema Mpogolo.
Alisisitiza, Jiji la Dar es Salaam, linaendelea na ujenzi wa sekondari za ghorofa zenye vifaa vya kisasa,vitabu, kuimarisha nidhamu na uwajibikaji, matumizi ya teknolojia na kutekeleza mkakati wa kufuta ufaulu wa daraja sifuri na la nne.
Alipongeza halimashauri ya jiji hil kuamua kuwa na kituo cha taaluma alichosema kitakuwa ni chachu ya kuongeza ufaulu, kuwaongezea ujuzi walimu na kufanya tathimini ya elimu.
Ofisa Elimu Sekondari wa Jiji la Dar es Salaam,Mussa Ally, alisema hafla hiyo ya utoaji tuzo ni baada ya matokeo ya mitihani ya ndani ya halimashauri iliyoratibiwa na kamati maalumu iliyoundwa nia ikiwa ni kupandidha ufaulu wa ndani Kwa lengo la kufanya vizuri katika mitihani ya kitaifa.










Post a Comment