VYOMBO VYA HABARI VYA MTANDAONI KINARA UWASILISHAJI KAZI SAMIA KALAMU 2026 AWARDS
Hadi kufikia Jumatatu, tarehe 15 Juni 2026, jumla ya kazi za kushindanishwa 624 zimekwishawasilishwa kutoka sehemu mbalimbali nchini kupitia mfumo wa kidijitali wa samiaawards.tz kwa ajili ya kuwania Tuzo za Uandishi wa Habari na Makala za Maendeleo, maarufu kama Samia Kalamu Awards kwa mwaka 2026.
Takwimu hizo zimetolewa
Juni 17,2026 katika taarifa iliyosainiwa kwa pamoja kati ya mwenyekiti wa tuzo
hizo Peter P. Mwasalyanda na Dkt. Rose Reuben ambaye ni mwenyekiti mwenza.
Katika taarifa
hiyo imeandikwa pia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Bodi ya Ithibati ya
Waandishi wa Habari (JAB), wanaendelea kupokea kazi hizo huku takwimu zikionyesha
kuwa kazi 569 (asilimia 91.2) ziko kwenye makundi ya tuzo za kisekta, kazi 25
(asilimia 4.0) kwenye tuzo maalumu za kitaifa, na kazi 20 (asilimia 4.8) zikiwa
katika kundi la tuzo za vyombo vya habari.
Katika
uwasilishaji huo, vyombo vya habari vya mtandaoni vimeibuka kidedea kwa kuwa
vinara baada ya kuwasilisha kazi 276, ambayo ni sawa na asilimia 44 ya kazi
zote zilizopokelewa hadi sasa.
Upande wa
majukwaa mengine ya habari unaonyesha kuwa magazeti yamefuatia kwa kuwasilisha
kazi 178 (asilimia 29), yakifuatiwa na televisheni zenye kazi 102 (asilimia
16), redio zikiwa na kazi 60 (asilimia 10), wakati majarida yakifunga orodha
hiyo kwa kuchangia kazi 8 pekee ambayo ni sawa na asilimia 1 ya maombi yote.
Mwitikio
huu mkubwa unaonyesha wazi jinsi matumizi ya majukwaa ya kidijitali yanavyozidi
kushika kasi katika uzalishaji na usambazaji wa habari za maendeleo, huku
ukionyesha dhamira thabiti ya wanahabari nchini katika kuelimisha na
kuhamasisha jamii.
Kamati ya
maandalizi imewapongeza wote waliowasilisha kazi zao na kuwasihi wale ambao
hawajamaliza mchakato huo kutumia vyema muda uliosalia kabla ya dirisha
kufungwa rasmi tarehe 30 Juni 2026 saa 5:59 usiku, ambapo kazi zinazokubaliwa
ni zile tu zilizochapishwa au kurushwa kuanzia tarehe 1 Julai 2025 hadi tarehe
30 Juni 2026.
Tuzo
za Samia Kalamu zilianzishwa kwa mara ya kwanza mwaka 2025 kufuatia ahadi na
maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan,
aliyetaka ziwe mchakato endelevu wa kila mwaka, jambo ambalo alilisisitiza tena
wakati wa ufunguzi wa Bunge la 13 tarehe 14 Novemba 2025.
Chini ya kaulimbiu "Kalamu kwa
Maendeleo", jukwaa hili la kitaifa linalenga kutambua na kuhamasisha
weledi, maadili, utafiti na ubunifu katika uandishi wa habari zinazochochea
maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku waandaaji wakiwakaribisha wadau
mbalimbali kushirikiana nao kwa hali na mali kufanikisha hafla ya utoaji tuzo
inayotarajiwa kufanyika kati ya mwezi Oktoba na Desemba 2026.

Post a Comment