SERIKALI YAPOKEA GAWIO LA TRILIONI 1.3 KUTOKA KWA TAASISI ZA UMMA NA KAMPUNI

 







SERIKALI imepokea Sh trilioni 1.327 za gawio na michango mingine kutoka taasisi za umma na kampuni ambazo ina umiliki wa hisa chache.

Kiasi hicho ni sawa na ongezeko la asilimia 30 ikilinganishwa na Sh trilioni 1.028 za gawio la mwaka jana.

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu alisema hayo katika hafla ya Gawio 2026 Ikulu ya Dar es Salaam leo.
Alisema kiasi hicho kilichokusanywa hadi Juni 29, mwaka huu ni ongezeko la Sh bilioni 299 kutoka makusanyo ya mwaka uliopita.

Mchechu alisema kati ya fedha hizo, Sh bilioni 800.5, sawa na asilimia 60 ya makusanyo yote zimetokana na gawio kutoka mashirika na kampuni za biashara, Sh bilioni 406 (asilimia 30) ni michango ya asilimia 15 ya mapato ghafi kutoka taasisi zisizo za kibiashara, huku Sh bilioni 121.5 (asilimia 10) zikitokana na mapato mengine yanayohusiana na uwekezaji wa serikali.

Alisema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, makusanyo ya gawio na michango yameongezeka kutoka Sh bilioni 637 mwaka 2020/2021 hadi Sh trilioni 1.327 mwaka 2025/2026, sawa na ukuaji wa asilimia 108.

Aidha, Mchechu alisema thamani ya uwekezaji wa serikali unaosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina imeongezeka kutoka Sh trilioni 67.01 mwaka 2020/2021 hadi Sh trilioni 92.2 mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 37.

Alisema mafanikio hayo yamechangiwa na kuimarika kwa utawala bora, uwajibikaji, matumizi ya teknolojia, uwekezaji wa kimkakati na usimamizi madhubuti wa mali za umma.

“Taasisi hizi zimekumbatia mageuzi ya kiuongozi na kibiashara na zimeendelea kujijenga upya ili ziweze kutoa matokeo makubwa zaidi kwa taifa,” alisema Mchechu.

Alitoa mfano kuwa baadhi ya mashirika yaliyokuwa yakikabiliwa na changamoto za kifedha sasa yameanza kurejea katika faida.

Alitaja Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) lililopata faida ya Sh bilioni 22.9 mwaka 2024/2025 baada ya kupata hasara ya Sh bilioni 18 mwaka uliotangulia na hivyo kutoa gawio la Sh bilioni 1.6 kwa serikali.

Pia, alisema Shirika la Posta Tanzania limepata faida ya Sh bilioni 2.8 baada ya kutoka kwenye hasara ya Sh bilioni 27.9, huku Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) likiendelea kupata faida ya Sh bilioni 20.5 na kuendelea kutoa gawio kila mwaka.

Kwa upande wa huduma za umma, alisema Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imefanikiwa kuwafanyia upasuaji mkubwa wa moyo zaidi ya wagonjwa 760 kwa kutumia uwekezaji na ruzuku ya serikali ya Sh bilioni 6.7, hatua iliyopunguza rufaa za matibabu nje ya nchi na kuokoa fedha za kigeni.

Aidha, alisema Hospitali ya Benjamin Mkapa imeendelea kufanya upandikizaji wa figo na uloto kwa wagonjwa wa selimundu, wakati Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imeendelea kuwa mhimili wa uchumi wa kidijiti na mwaka huu imewasilisha gawio la Sh bilioni 61 kwa serikali.

Mchechu alisema serikali pia imeendelea kupanua umiliki wake katika sekta ya madini ambapo idadi ya miradi ambayo serikali ina hisa kupitia Msajili wa Hazina imeongezeka kutoka 10 hadi 15 kufikia Juni 2026 na mingine 10 ipo hatua za mwisho za majadiliano.

Alisema kampuni ambazo serikali ina hisa, zikiwemo NMB Bank, NBC Bank, TAZAMA Pipelines Limited, Puma Energy Tanzania, TPC Limited, Mbeya Cement Company Limited na Airtel Tanzania, zimeendelea kuongeza faida, thamani ya uwekezaji na gawio kwa serikali.

No comments