RAIS SAMIA APONGEZA GAWIO ATAKA BIDII ZAIDI

 

 



RAIS Samia Suluhu Hassan amepongeza taasisi na kampuni za umma zilizotoa gawio la Sh trilioni 1.327 na kuagiza zisibweteke.

Akizungumza kwenye hafla ya Siku ya Gawio Ikulu Dar es Salaam leo, Rais Samia alisema gawio hilo limetokana na uzalishaji na kuimarika kwa tija na ufanisi wa taasisi hizo. 

Siku ya Gawio ni jukwaa la kuwapa wananchi fursa ya kuona matokeo ya uwekezaji unaofanywa kwa niaba yao. Kwa mujibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina, takribani taasisi na kampuni za umma 308 zinatakiwa kutoa gawio kwa serikali ambayo mpaka Juni 2025, imewekeza zaidi ya Sh trilioni 92 katika taasisi na kampuni za umma.

Rais Samia alisema anatarajia gawio kubwa zaidi mwakani na atafurahi ikiwa hivyo. Ameonya watumishi wazembe na wenye matumizi mabaya ya rasilimali za nchi kwamba hawatasita kuwachukulia hatua.

“Mwaka huu tumepata Shilingi trilioni 1. 327 kulinganisha na Shilingi trilioni 1.028 za mwaka jana, tumeongeza karibu Shilingi bilioni 300 si haba, mambo sio mabaya. Nawapongeza wote mliochangia mafanikio haya lakini msibweteke… Najivunia ninyi,” alisema rais.

Aliongeza: “Tathmini hii niliagiza mwaka jana ifanyike na Msajili wa Hazina (Nehemiah Mchechu) na timu yake waliifanya vizuri na matokeo yake tumeyaona… Wote wametuonesha kuwa taasisi za umma zinaweza kufanya vizuri kwa kutoa huduma na kujiendesha kwa ufanisi kushindana katika mapato ya serikali, haya ndio maono na mwelekeko tunaotaka kwa hiyo kwenye mafanikio hatuatacha kuwatambua,” alisema.

Alisema huo ndio mwelekeo inaoutaka serikali na pongezi zake ziwe chanzo cha kuongeza juhudi na maarifa, kwani gawio ni sehemu ya lengo la serikali la kuongeza mapato ya ndani.

“Tulipotoka ni mbali, tunakwenda polepole. Bajeti ya mwaka huu, kipande cha kujitegemea kimebaki kidogo, tukikaza mwendo baada ya miaka miwili tutakwenda vizuri,” alisema.

Kuhusu kufanyika kwa mageuzi katika taasisi, alisema alielekeza kwenye hafla za mwaka jana kwamba taasisi hizo haziwezi kutegemea serikali kwa kila changamoto wakati zina uwezo.

Alisema sasa zimeanza kuonekana, huku akitolea mfano wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kwamba ina uwezo wa kukopa fedha ikatanua bandari, wakawa na uwezo wa kulipa mkopo wenyewe.

Rais Samia alitoa maelekezo kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina kuendelea na kazi ya kutathmini taasisi hizo na ipewe uzito unaostahili, lengo likiwa ni kutoka kwenye dhamira na kufikia malengo waliyojiwekea.

Akizungumzia kaulimbiu ya Siku ya Gawio: “Uwekezaji wa Umma wenye Matokeo: Nguzo ya Uchumi Shindani na Maendeleo Endelevu Kuelekea Dira 2050,” rais alisema inakumbusha uwekezaji wenye matokeo ni unaovutia mitaji, kupunguza gharama za kufanya biashara, kukuza huduma, kuongeza mapato ya serikali na kulinda maslahi ya wananchi.

“Ili kaulimbiu hiyo ipate maana na uhalisia lazima itafsiriwe katika misingi ya kazi na huduma kwa wananchi ili tufikishe huduma na kukuza uchumi wetu. Nasisitiza sababu utekelezaji wa dira unahitaji taasisi zenye uwezo wa kuingia kwenye ushindani wa soko,” alisema.

Aliongeza: “Tunapoianza kesho (leo) kutumia dira, tunatakiwa kuwa makini, taasisi zetu ziwe imara kwelikweli, wenye taasisi zenye kichefuchefu (zisizofanya vizuri) zitafutiwe dawa zitulie ili twende nazo pamoja.”

Rais Samia alizitaka taasisi hizo kufungua milango kwa sekta binafsi, akisisitiza kwamba hataki taasisi zinazofanya kazi kwa mazoea. Alisema ili nchi ijenge uchumi shindani, inahitaji taasisi zinazoleta matokeo ili kutoka kwenye takwimu na kwenda kwenye ukweli.

“Tunasema mipango sio matumizi. Maofisini mwetu tuna mipango mingi, sera, mikakati, kauli kabambe lakini zipo tu, hayo si matumizi. Dira yetu nzuri sana, ndani yake tuna mipango ya maendeleo ya muda mfupi na mrefu na tumemaliza nyenzo zinazoongoza utekelezaji wake lakini yote hayo hayataleta maendeleo ya nchi kama hakuna kutafsiri, kutathmini na kusimamia utekelezaji wake. Kwa hiyo tujipange kwenye utekelezaji wa dira yetu,” alisema.

“Msajili wa hazina, kampuni, taasisi za serikali na Watanzania wote, twende tukaitafsiri na kutekeleza dira yetu kila mmoja katika maeneo tofauti tofauti,” alisema rais.

Alizitaka wizara kusimamia taasisi zake na kutafsiri dira kwenye mpangokazi wao, akisema hilo si jukumu la msajili pekee.

Wakati huo huo, Rais Samia pia alikabidhiwa tuzo kwa kutambua mchango wake kwenye mafanikio hayo. Alisema ameipokea kwa unyenyekevu, akitambua ni ya kazi ya pamoja na si peke yake.

No comments