SERIKALI YAONDOA USHURU MPYA WA BODABODA
SERIKALI imekubali
ushauri wa wabunge wa kufuta pendekezo la kuzitoza pikipiki ushuru wa bidhaa wa
asilimia tano.
Sambamba na hilo,
imefuta mpango wa kuongeza ada ya usajili wa pikipiki kutoka Sh 95,000 hadi Sh
150,000.
Waziri wa Fedha,
Balozi Khamis Mussa Omar alitangaza uamuzi huo wakati akiwasilisha maelezo ya
Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2026 bungeni Dodoma jana.
Balozi Omar alisema
serikali imekubaliana na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuondoa pendekezo
la kutoza ushuru wa bidhaa wa asilimia tano kwenye pikipiki kama ilivyokuwa
imependekezwa kwenye Ibara ya 11(g) ya muswada huo.
Juni 11, mwaka huu,
wakati akiwasilisha mapendekezo ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha
2026/2027, waziri alipendekeza kutoza ushuru wa bidhaa kwa kiwango cha asilimia
tano kwenye pikipiki isipokuwa pikipiki za wagonjwa wa dharura, pikipiki
zinazotumia gesi asilia na pikipiki za umeme.
Awali, Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Bajeti ilipinga pendekezo la serikali na kuitaka itafakari
upya kwa kusema kwamba pikipiki zimetoa fursa ya ajira kwa vijana wengi.
“Kiwango
kinachopendekezwa cha ushuru ni kikubwa kinachoweza kuathiri si tu bei ya
pikipiki hizo bali kitaathiri
pia ajira za vijana wanaojiajiri kupitia biashara ya kusafirisha abiria,”
alisema Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mashimba Ndaki.
Mbunge wa Kigoma
Mjini, Clayton Chipando (CCM) alisema, “Hizi tozo zipelekwe sehemu zingine, si
mtuletee sisi watu wa tungi (walevi)?... watoleeni bodaboda mtuletee sisi watu
wa tungi tutalipa hiyo hela wala haina shida yoyote,” alisema Chipando maarufu kwa
jina la Baba Levo.
Mbali na hilo,
Balozi Omar alisema Sehemu ya 24 ya Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2026
inapendekeza marekebisho katika Kifungu cha 25 cha Sheria ya Bima ya Afya kwa
Wote, Sura ya 161 ili kuongeza Sh 20 zinazotozwa katika kila sigara 1,000.
Pia, Sh 20 itatozwa
katika kila kilo moja ya sukari inayoagizwa kutoka nje ya nchi kuwa chanzo cha
mapato ya Mfuko wa Bima ya Afya kwa Wote.
“Lengo la
marekebisho haya ni kugharimia huduma ya bima ya afya kwa watu wanaostahili
kugharamiwa na mfuko huo,” alisema.
Balozi Omar alisema
sehemu ya saba ya muswada huo inapendekeza kufanya marekebisho katika Kifungu
cha 34 cha Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, Sura ya 41 ili kuongeza kodi
kwenye zawadi ya ushindi katika michezo ya kubahatisha hadi kufikia asilimia
15.
Aliwaeleza wabunge
pia kuwa uboreshaji unafanyika kwenye mgawanyo ili kubainisha mgawanyo wa
mapato yanayotozwa kwenye zawadi ya ushindi katika michezo ya kubashiri
matokeo.
Alisema asilimia
saba ya mapato ya kasino za ardhini yanagawanywa kwa asilimia 70 kwenda Mfuko
wa Udhamini wa Kudhibiti Ukimwi na asilimia 30 itaelekezwa kwenye Mfuko wa Bima
ya Afya kwa Wote.
“Aidha, asilimia 13
ya mapato ya michezo ya kubashiri yanagawanywa kwa asilimia 70 kwenda Mfuko wa
Udhamini wa Kudhibiti Ukimwi na asilimia 30 itaelekezwa kwenye Mfuko wa Bima ya
Afya kwa Wote,” alisema.
Alisema asilimia 70
ya tozo itawasilishwa moja kwa moja katika Mfuko wa Barabara, asilimia 25
itawasilishwa katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali na asilimia tano
itawasilishwa katika akaunti maalumu iliyopo BoT kwa ajili ya ujenzi wa
miundombinu saidizi katika maeneo maalumu ya kiuchumi au maeneo ya uzalishaji
kwa mauzo ya nje ya nchi

Post a Comment