Rais wa Namibia Kurudi Magomeni Alikoishi Miaka ya 1980!
Mtaa wa Magomeni Mwembechai jijini Dar es Salaam
unatarajiwa kufurika shangwe na nderemo wakati utakapomkaribisha aliyekuwa
"jirani" yao wa miaka ya 1980, ambaye sasa anarudi akiwa Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe.
Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah.
Dkt. Nandi-Ndaitwah anawasili nchini kesho, Juni 19,
2026, kwa ziara ya kitaifa ambapo mbali na kukutana na mwenyeji wake Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan
Ikulu siku ya Jumamosi, atatenga muda maalum wa kwenda kupaona alipokuwa
anaishi Magomeni alipokuwa akipigania uhuru wa nchi yake kupitia chama cha
SWAPO.
Huu ni ugeni mzito unaoamsha kumbukumbu za jinsi Dar es
Salaam ilivyolea viongozi wakubwa barani Afrika wakati wa harakati za ukombozi.
Baada ya Magomeni, Rais huyo pia ataelekea Kongwa, Dodoma kutembelea kambi ya
zamani ya wapigania uhuru.
Ratiba
ya Ziara ya Kitaifa
- Juni 19, 2026:
Kuwasili nchini kwa Rais Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah.
- Juni 20, 2026:
Mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan
Ikulu jijini Dar es Salaam, yakifuatiwa na mkutano na waandishi wa habari.
- Ziara ya Kumbukumbu:
Kutembelea Magomeni Mwembechai (Dar es Salaam) na Kambi ya Wapigania Uhuru
iliyopo Kongwa, mkoani Dodoma.
- Juni 22, 2026:
Hitimisho la ziara.
"Ziara hii ni dhihirisho la
uhusiano wa kindugu na wa kihistoria kati ya Tanzania na Namibia, uliojengwa
katika misingi ya harakati za ukombozi wa Afrika, mshikamano na ushirikiano wa
maendeleo," ilieleza taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya
Rais (Ikulu), Bakari S. Machumu.
Magomeni kaeni mkao wa kula, 'mtoto
wa nyumbani' anarudi akiwa Rais!

Post a Comment