Ukuaji wa Idadi ya Wanyamapori Nchini: Fursa ya Dhahabu ya Ajira Kwenye Mnyororo wa Thamani wa Utalii Tanzania



Na Mwandishi Wetu

Kuongezeka kwa idadi ya wanyamapori nchini kumeendelea kufungua milango mikubwa ya ajira na fursa za kiuchumi kwa Watanzania, huku nchi ikithibitisha nafasi yake kama moja ya mataifa yenye utajiri mkubwa zaidi wa wanyamapori barani Afrika.

Matokeo ya Sensa ya Kitaifa ya Wanyamapori ya Mwaka 2024/2025 yaliyozinduliwa hivi karibuni jijini Arusha yanaonesha uwepo wa spishi 28 za wanyamapori wakubwa katika mifumo mbalimbali ya ikolojia.

Ongezeko hili la wanyama linamaanisha kukua kwa uhakika kwa soko la ajira katika mnyororo mzima wa sekta ya utalii, kuanzia waongoza watalii, madereva, wafanyakazi wa hoteli na kambi za kitalii, hadi kwa watoa huduma za usafiri na chakula.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa matokeo hayo kwa niaba ya Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Ashatu Kijaji alieleza kuwa Tanzania sasa inashika nafasi ya tatu Afrika kwa idadi ya tembo ikiwa nao 66,737, na nafasi ya nne kwa faru weusi na weupe wanaofikia 322.

Utajiri huu wa kipekee wa bayoanuwai, unaojumuisha pia uongozi wa Tanzania barani Afrika kwa kuwa na nyati zaidi ya 321,437 na simba zaidi ya 17,200, unazidi kuimarisha nafasi ya nchi kama kitovu kikuu cha utalii duniani.

Ujio mkubwa wa watalii unaochochewa na takwimu hizi una matokeo ya moja kwa moja katika kuongeza nafasi za kazi na vipato kwa jamii zinazozunguka hifadhi na Watanzania kwa ujumla.

Hata hivyo, ili kulinda mnyororo huu unaozalisha maelfu ya ajira, serikali imeonya kuwa shinikizo la shughuli za kibinadamu katika maeneo ya ikolojia linaweza kuhatarisha mustakabali wa sekta hiyo.

Dk. Kijaji alibainisha kuwepo kwa migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, akitolea mfano Pori la Akiba la Longido ambako wanyama kama swala na twiga wameanza kupotea.

Kutokana na hali hiyo, aliziagiza taasisi za utafiti kama Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) kufanya tafiti za kina kuhusu matumizi ya ardhi na athari za kibinadamu katika korido za wanyama ili kulinda rasilimali hizi zinazolisha uchumi wa nchi.

Mkurugenzi Mkuu wa TAWIRI, Dk. Eblate Mjingo aliongeza kuwa juhudi za kupambana na ujangili zimesaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza idadi ya wanyama, hususan tembo ambao wameongezeka kutoka viwango vya chini vya miaka ya nyuma. Licha ya mafanikio hayo, Dk. Mjingo alitahadharisha kuwa mwingiliano wa makazi ya watu, kilimo, na ufugaji karibu na maeneo ya hifadhi kama vile Maswa na Selous-Nyerere unavuruga njia za asili za uhamaji wa wanyama.

Changamoto hii inatishia uendelevu wa utalii, jambo linalofanya takwimu hizi kuwa mwongozo muhimu wa jinsi ya kubalansi uhifadhi na maendeleo ya kijamii.

Kwa upande wao, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk. Hassan Abbasi, na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Timotheo Mzava, walisisitiza kuwa sensa hii ni zana ya kimkakati itakayosaidia kuunda sera bora za matumizi endelevu ya ardhi na kutatua migogoro iliyopo.

Sensa hiyo ya Mwaka 2024/2025, ambayo imefadhiliwa kwa asilimia 100 na serikali ya Tanzania, inaweka msingi imara wa jinsi nchi inavyoweza kulinda ikolojia yake huku ikihakikisha kuwa sekta ya utalii inaendelea kuwa mhimili mkuu wa uzalishaji wa ajira na kukuza uchumi wa taifa.

No comments