MAMILIONI YA WHICKERS YATUA TANZANIA KUKAMILISHA FILAMU YA CHIDREN OF HONEY
Na Rahel Pallangyo
Filamu ya Kitanzania
ya Children of Honey imejipatia ruzuku nono ya pauni 120,000 za
Uingereza, ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 400 za Kitanzania, baada ya
kushinda tunzo ya 2026 ya Whickers Film & TV Funding Award ya Uingereza.
Mradi huo ni miongoni
mwa miradi 600 duniani kote iliyoomba kufadhiliwa ukamilishaji wake.
Waongozaji wenza,
Jigar Ganatra na Emanuel Musa Marco,walipigania vilivyo mradi wao wakati
walipoingia katika hatua za tano bora kati ya maingizo 600.
Kazi ya kupigania
mradi huo waliifanya kwenye jukwaa kubwa la tamasha la Sheffield DocFest—ambalo
ni moja ya masoko yenye ushawishi mkubwa zaidi wa filamu za dokumentari duniani.
Baada ya mchujano huo
wa awali ulioweka kando mamia ya washiriki, ni miradi mitano tu ya kipekee
iliyoalikwa nchini Uingereza ukiwamo wa Children of Honey na kuchuana katika
jukwaa hilo mbele ya jopo la majaji waliobobea, akiwemo mwandaaji wa filamu
kutoka Kenya Sam Soko na mkurugenzi wa ubunifu wa Sheffield DocFest,
Raul Niño Zambrano.
Katika fainali hiyo
ya kukata na shoka, Tanzania ilichuana bega kwa bega na filamu kutoka mataifa
makubwa zikiwemo Welcome to Our Bathhouse kutoka Japan, Ashes
kutoka Syria, Mexico is Ours kutoka Scotland, na All Fixed Up
kutoka China, ambapo kila mshiriki alipewa dakika saba tu za kusimama jukwaani
kuwasilisha wazo lake na vionjo vya video, kisha kukabiliwa na maswali magumu
ya papo kwa papo kutoka kwa majaji ili kutetea sanaa yake.
Filamu ya Children
of Honey, iliyoundwa kwa ushirikiano wa karibu na jamii ya wawindaji na
waokotaji matunda ya Wahadzabe wa kaskazini mwa Tanzania, imeweka rekodi ya
kuwa filamu ya kwanza ya ukweli ya urefu wa kati kuongozwa kwa ushirikiano na
mwandaaji anayetokea ndani ya jamii hiyo yenyewe.
Hadithi hii
inafuatilia kwa ukaribu maisha ya vijana watatu wa Kihadza wanapopita katika
kipindi cha mpito kuelekea utu uzima, huku wakikabiliwa na mabadiliko makubwa
ya kijamii na kiutamaduni yanayotishia mazingira yao ya asili.
Kupitia mfumo huu
bunifu wa ushirikishwaji, Wahadzabe wenyewe si tu wahusika wa filamu bali ni
wasimulizi wakuu wa hadithi yao, wakitumia vifaa vya kurekodi na picha
walizopiga wenyewe ili kuonesha taswira halisi ya maisha, mila, na mustakabali
wao kwa ulimwengu.
Kupatikana kwa ruzuku
hii sasa kunafungua milango ya kuendeleza uzalishaji wa Children of Honey,
huku ukiongeza nguvu katika kampeni ya uhifadhi wa lugha na utamaduni wao,
wakati filamu ya Kijapani ya Welcome to Our Bathhouse ikishika nafasi ya
pili na kuondoka na pauni elfu ishirini na tano.

Post a Comment