Rais Samia amwomba Drogba kuwa Balozi wa Tanzania AFCON 2027

RAIS Samia Suluhu Hassan amemuomba mshambuliaji wa zamani wa timu ya taifa ya mpira wa miguu ya Ivory Coast na Chelsea ya England, Didier Drogba kuwa Balozi wa Tanzania kuelekea fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027). 

Kwa mujibu wa Ikulu, ombi hilo limetolewa leo wakati nyota huyo alipowasili Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma kuonana na Rais Samia.

Aidha, Rais Samia ameitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kushirikiana na Drogba kubadilishana uzoefu wa kuendesha vituo vya michezo nchini.

Drogba aliyekuwa nchini kwa mwaliko wa waziri mwenye dhamana ya habari na michezo, Paul Makonda amemshukuru Rais Samia na kuonesha utayari wa kushirikiana na serikali.

Tanzania inaandaa Afcon 2027 kwa pamoja na Kenya na Uganda na droo ya kufuzu itafanyika Mei 19, mwaka huu. Fainali hizo zitaanza Juni 19 hadi Julai 17, 2027.

Huo ni mwanzo wa mchakato utakaohusisha mataifa 48 yatakayopangwa katika makundi 12, ambapo washindi wawili wa kwanza kila kundi watakata tiketi ya kucheza fainali hizo.

Pamoja na mafanikio kadhaa aliyoyapata katika mpira wa miguu, mwaka 2005 Drogba alifanya ushawishi uliosaidia kusitishwa kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini kwao vilivyodumu kwa miaka kadhaa.

Drogba baada ya kuiongoza Ivory Coast kufuzu kwa Kombe la Dunia mwaka 2006 kwa mara ya kwanza Oktoba 8, 2005 alichukua kipaza sauti kwenye chumba cha kubadili nguo akizungukwa na wachezaji wenzake kutoka Kaskazini na Kusini mwa nchi, akapiga magoti mbele ya kamera ya televisheni ya taifa na kuwaomba wapiganaji waweke silaha chini.

Ndani ya wiki moja baada ya ombi lake, pande zote mbili zilizoingia kwenye mgogoro zilikubali kusitisha mapigano, tukio ambalo lilionesha nguvu ya michezo katika kuunganisha taifa.

Ili kuimarisha zaidi amani hiyo, Drogba alishauri mechi ya kufuzu dhidi ya Madagascar ya mwaka 2007 ichezwe katika Mji wa Bouaké, uliokuwa ngome ya waasi na hiyo ilikuwa ishara kubwa ya maridhiano ambapo viongozi wa serikali na waasi walikaa pamoja kushuhudia ushindi wa timu ya taifa.







 

No comments