England Premier League: Umri wa Miaka 23 Ndio Dhahabu

Morgan Rogers alikuwa na umri wa miaka 23 alipohama kutoka Aston Villa kwenda Chelsea.

Dirisha la usajili la majira ya joto katika Ligi Kuu ya England (Premier League) linaendelea kushuhudia mabadiliko makubwa ya kimkakati huku klabu zikiweka wazi mfumo wao wa kusaka vipaji kupitia takwimu za wachezaji zaidi ya 800 waliouzwa na kununuliwa katika misimu mitatu iliyopita. 

Uchambuzi wa kina unaonesha kuwa soko la usajili limekuwa na utulivu wa kustaajabisha katika eneo la umri, ambapo wastani wa umri wa mchezaji anayesajiliwa umekuwa ukisomeka miaka 24, wakati wale wanaopigwa bei wakiondoka klabuni wakiwa na wastani wa miaka 27, jambo linalodhihirisha jinsi timu zinavyowekeza kwa vijana na kuachana na wakongwe kwa wakati sahihi.

Katika nafasi ya mawinga, mifumo ya usajili imekuwa thabiti kiasi cha kushangaza bila kubadilika msimu hadi msimu, ambapo mawinga wa kushoto wamekuwa wakisajiliwa wakiwa na wastani wa umri wa miaka 22 na miezi mitatu, wakati wa kulia wakiwa na miaka 22 na miezi minne. 

Klabu zinaonekana kusaka nguvu mpya, kasi, na hata chembe fulani ya fujo za kiufundi uwanjani kutoka kwa vijana hawa, huku suala la thamani ya mauzo ya baadaye (resale value) likiwa na uzito mkubwa kwani winga wa miaka 22 anaweza kuuzwa kwa faida kubwa baada ya misimu miwili au mitatu. 

Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kuwa mawinga hawa ndio huuzwa wakiwa na umri mdogo zaidi wa miaka 25 hadi 26, mara nyingi wakihamia kwenye klabu kubwa zaidi baada ya kung'ara kwenye timu za wastani.

Baada ya msimu mgumu, Tottenham imewaleta baadhi ya wachezaji wenye uzoefu mkubwa, akiwemo Andrew Robertson.


Msimu huu wa joto umezua gumzo kubwa baada ya klabu za Chelsea na Spurs kwenda kinyume na upepo wa kawaida kwa kusajili wachezaji wenye wastani wa umri mkubwa zaidi kuliko wale waliowapiga bei, ikiwa ni ishara ya kuhitaji mafanikio ya haraka uwanjani badala ya kusubiri mradi wa miaka mingi. 

Wakati Chelsea ikileta wachezaji wenye wastani wa miaka 24.5 dhidi ya 24 waliotoka, Spurs wamefanya uamuzi mkubwa zaidi kwa kusajili wenye wastani wa karibu miaka 27 huku wanaoondoka wana miaka 24, jambo ambalo ni tofauti kabisa na misimu iliyopita ambapo timu hizo zilikuwa mstari wa mbele kuwinda vipaji vya miaka 21 pekee. 

Kwa upande mwingine, timu kama Newcastle na Everton zimeendelea kung'ang'ana na sera ya kupunguza wastani wa umri kwa kuleta vijana wadogo sana wenye umri mdogo kwa miaka saba hadi nane ikilinganishwa na wachezaji waliowapisha.

Mabadiliko haya ya kimkakati pia yamegusa eneo la uzoefu, ambapo huku kukiwa na wimbi la wachezaji wa miaka 40 na staa Lionel Messi mwenye miaka 39 kucheza Kombe la Dunia, klabu za Premier League nazo zimeonekana kuanza kugeukia uzoefu badala ya ujana mtupu. 

Idadi ya wachezaji waliotimia au kuvuka miaka 28 waliosajiliwa msimu huu imeongezeka hadi kufikia asilimia 24 kutoka asilimia 16 ya msimu uliopita, huku vijana wa chini ya miaka 19 wakishuka hadi kufikia asilimia tisa pekee, jambo linaloonyesha kuwa uzoefu unaanza kuthaminiwa zaidi katika mbio za ubingwa na kuwania nafasi za juu.

Katika upande wa idadi ya usajili, timu nyingi zimeonekana kuwa na msimamo unaofanana kwa kusajili wachezaji kati ya watatu na sita pekee kama ilivyokuwa kwa klabu 15 kati ya 17 zilizobaki kwenye ligi msimu uliopita, huku wakwepaji wa kanuni hiyo wakionyesha matokeo tofauti uwanjani. 


Sunderland ilifanya mabadiliko makubwa kwenye kikosi chake msimu uliopita na yaliseta matokeo ya kustaajabisha – lakini mabadiliko huambatana na hatari.


Wakati Sunderland iliwahi kufanya maajabu ya kusajili wachezaji 13 na kumaliza nafasi ya saba, wengine kama Nottingham Forest walijikuta kwenye vita ya kushuka daraja baada ya kufanya usajili mkubwa wa mabaka, jambo linalothibitisha kuwa katika soka la kisasa la England, kuwa na mpango thabiti na kusajili kwa malengo mahususi kunalipa zaidi kuliko kufumua kikosi kizima.

No comments