SAMIA KUFUNGUA RASMI BWAWA LA JULIUS NYERERE
Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuzindua rasmi
Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP), chenye uwezo wa kuzalisha
Megawati 2,115, Agosti 22, 2026, katika eneo la mradi Rufiji, Mkoa wa Pwani.
Waziri wa
Nishati, Deogratius Ndejembi, amesema hayo
Agosti 15, 2026 jijini Dar es Salaam.
Amesema JNHPP ni
mradi mkubwa zaidi wa kuzalisha umeme nchini uliotekelezwa kwa fedha za ndani,
ukiwa na uwekezaji wa takribani shilingi trilioni 7.452, sawa na Dola za
Marekani bilioni 3.35. Mradi huo ulianza kujengwa Juni 2019 na kukamilika Machi
2025.
Kwa mujibu wa
Ndejembi, hadi Mei 31, 2026, JNHPP ilikuwa imezalisha takribani asilimia 44.9
ya umeme wote uliozalishwa na kuingizwa katika Gridi ya Taifa kwa kipindi cha
mwaka mmoja, hivyo kuchangia karibu nusu ya umeme unaotumika nchini na kusaidia
kupunguza changamoto ya upungufu wa umeme.
Ameongeza kuwa
mbali na uzalishaji wa umeme, mradi huo wenye bwawa lenye uwezo wa kuhifadhi
mita za ujazo bilioni 33 za maji, unatarajiwa kusaidia kudhibiti mafuriko
katika Mto Rufiji, kilimo cha umwagiliaji, utalii na matumizi ya binadamu.
Ndejembi amesema
mradi wa JNHPP pia unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na amewaalika
Watanzania kufuatilia na kushiriki katika uzinduzi huo, akieleza kuwa ni tukio
la kihistoria katika maendeleo ya sekta ya nishati nchini.

Post a Comment