WANASAYANSI WAZUNGUMZIA MPIRA WA TRIONDA KWA WAPENDA MASHUTI YA MBALI



Na Mwandishi Maalumu

Wakati homa ya Kombe la Dunia ikizidi kupanda, mjadala mzito umehamia kwenye maabara za sayansi ya michezo, huku wanasayansi wakitupa onyo mapema kwa wapiga mashuti ya mbali kujiandaa na mabadiliko makubwa ya mpira rasmi wa mashindano hayo unaojulikana kama Trionda.

Mpira huo uliotengenezwa na kampuni ya Adidas, umeingia kwenye historia ya Kombe la Dunia kuwa mpira wa kwanza kuwahi kutengenezwa kwa kutumia vipande vinne tu (4 panels).

Idadi hiyo ndogo ya vipande ilizua hofu ya mapema kuwa mpira huo ungekuwa mnyororo sana (smooth profile) na kuanza "kuyumba na kupaa" hewani kama ule mpira wa hovyo wa Jabulani uliosababisha vilio kwa makipa kwenye Kombe la Dunia la mwaka 2010 nchini Afrika Kusini.

Hata hivyo, wataalamu wa masuala ya usugu wa hewa (aerodynamics) wamebaini kuwa 'Trionda' una tatizo la tofauti kabisa: Mashuti ya mbali yatakuwa yanapungua kasi na kuishia njiani!

Wanasayansi hao hawatilii shaka ubora wa mpira mpya wa Kombe la Dunia, Trionda, bali wanahoji uwezo wake wa kusafiri umbali mrefu unapovurumushwa kwa nguvu kubwa. Mashaka yao makuu yamegawanyika katika maeneo matatu:

·         Kupunguza Kasi na Kuishia Njiani: Ngozi ya kwaruza na mifereji mirefu ya mpira huo husababisha upinzani mkubwa wa upepo (drag). Shuti kali la mbali litapoteza nguvu haraka na kuanguka hadi mita 10 mapema kuliko mipira ya miaka ya nyuma.

·         Mtihani kwa Wapigaji Mashuti ya Nguvu: Wachezaji wanaotegemea mashuti makali ya mbali na pasi ndefu watajikuta wakifeli kupata kasi na umbali waliozoea, jambo litakalowalazimu kubadili mbinu zao za upigaji uwanjani ili kufidia mita hizo 10 zinazopotea.

·         Kupinda Zaidi Hewani (Extreme Spin): Muundo wa kwaruza unawaongezea faida wapiga free-kick mafundi kwani mpira utapinda kwa kiwango kikubwa kuliko kawaida, hatua itakayowapa wakati mgumu magolikipa kuotea mwelekeo wake wa mwisho.

Siri ya Mistari na Ngozi ya Trionda

Ili kufidia uhaba wa mishono (seams) ambao ungeufanya mpira kuwa mnyororo mno, Adidas waliongeza mifereji mirefu (deep grooves) kwenye kila kipande, pamoja na kuuweka mtindo wa ngozi ya kwaruza (rough outer texture).

Mwanasayansi wa fizikia kutoka Chuo Kikuu cha Puget Sound, Dk. John Eric Goff, ameeleza kuwa uamuzi huo wa Adidas umebadilisha tabia ya msuguano wa hewa (drag crisis), jambo ambalo litawaumiza vichwa washambuliaji wanaopenda kupiga mashuti ya mbali au mabeki wanaopiga pasi ndefu.

“Kwa lugha rahisi, maana yake ni kwamba shuti kali la mbali litakuwa linapoteza nguvu na umbali hewani. Kwenye majaribio yetu ya kompyuta, tofauti hiyo si kubwa sana, lakini inatosha kabisa kwa wachezaji kugundua kuwa mashuti yao yanaangukia mita chache kabla ya pale walipokusudia,” alieleza Dk. Goff.

Mizania ya Kitaalamu: Trionda vs Mipira ya Zamani

Wanasayansi walifanya majaribio hayo kwa kuingiza mpira huo kwenye mtambo maalum wa upepo (wind tunnel) ili kupima kasi ambapo mpira huanza kupoteza mwelekeo (drag crisis point). Habari njema ni kwamba Trionda utakuwa mpira imara na unaotabirika kuliko Jabulani.

Hapa kuna ulinganifu wa kasi ambayo mpira huanza kupoteza utulivu (Drag Crisis Speed):

Jina la Mpira

Mwaka wa Kombe la Dunia

Kasi ya Kupoteza Utulivu (Km/h)

Hali yake Uwanjani

Jabulani

2010 (Afrika Kusini)

Km/h 79 – 97

Haubadiriki, ulikuwa unacheza na kuyumba hewani ghafla.

Brazuka

2014 (Brazil)

Km/h 50 – 65

Imara na wa kawaida.

Telstar 18

2018 (Urusi)

Km/h 50 – 65

Imara na wa kawaida.

Al Rihla

2022 (Qatar)

Km/h 50 – 65

Imara na wa kawaida.

Trionda

Mwaka Huu

Km/h 43 pekee

Hauyumbi kabisa, lakini unapunguza umbali ukiwa hewani.


Kwanini Jabulani Ikishindikana na Trionda ni Salama?

Tangu mwaka 1970, Adidas wamekuwa wakileta mipira mipya kwenye kila fainali za Kombe la Dunia, lakini mabadiliko madogo tu ya muundo hugusa moja kwa moja burudani ya uwanjani.

Dk. Goff na timu yake waliiweka Trionda kwenye mtambo wa upepo (wind tunnel) kupima uwezo wake wa kuhimili hewa na kuingiza data hizo kwenye kompyuta.

Siri kubwa ya mpira uliotulia uwanjani ipo kwenye hatua inayoitwa kitaalamu kama 'drag crisis'. Mpira ukiwa hewani, safu nyembamba ya hewa hunaswa pembezoni mwa ngozi yake na kuusaidia kusafiri mbali. Mpira ukiwa mnyororo kupitiliza kama Jabulani, hufikia hatua hii ukiwa tayari kwenye kasi ya mchezo, na kusababisha mabadiliko ya ghafla ya mwelekeo (erratic flight).

Trionda haina ugonjwa huo wa Jabulani. Inafikia hatua yake ya utulivu kwenye kasi ndogo ya kilomita 43 tu kwa saa, tofauti kabisa na Jabulani iliyokuwa ikiyumba ikifikia kasi ya kilomita 79 hadi 97 kwa saa. Hii ina maana Trionda utakuwa mpira unaotabirika na mtulivu sana kwenye krosi, kona, na mipira ya adhabu.

Mita 10 za Kupotea: Habari Njema kwa Magolikipa

Hata hivyo, utulivu huo una gharama yake. Ripoti hiyo inafichua kuwa pindi Trionda unapopigwa kwa nguvu kubwa ya mbali, unakutana na upinzani mkubwa wa upepo kuliko mpira wowote uliowahi kutumika katika kipindi cha miaka 20 iliyopita.

Kwenye vipimo vya kimaabara, shuti linalopigwa kwa kasi ya mita 35 kwa sekunde, mpira wa Trionda utaanguka umbali wa mita 10 fupi ukilinganishwa na mipira ya Al Rihla (2022) au Brazuka (2014).

 Hili ni dongo gizani kwa wapiga mashuti ya mbali, lakini ni sherehe kwa magolikipa watakaopata sekunde chache za ziada kujipanga.

Mwisho, wataalamu wametoa angalizo lingine: ngozi hiyo ya kwaruza inaweza kuwasaidia wachezaji mafundi kuuzungusha mpira hewani (spin) kwa kiwango kikubwa zaidi. Hii ina maana mashuti yanaweza yasiende mbali sana, lakini yale yatakayofika golini yatapinda kwa pembe kali, jambo ambalo linaweza kurudisha ugumu huo huo kwa walinda milango.

 

No comments