Samia aipongeza Tanzanite Queens kwa kuingia fainali Kombe la Dunia
Tanzanite Queens iliifunga Cameroon
mabao 2-0 katika Uwanja wa New Amaan Complex, Unguja jana na kufuzu kwa faida
ya bao la ugenini baada ya matokeo kuwa 3-3 kwani katika mechi ya awali
iliyochezwa jijini Yaoundé, Cameroon iliibuka na ushindi wa mabao 3-1.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram
Rais Samia aliandika; “Ninaipongeza timu ya Taifa ya Wanawake ya Mpira wa Miguu
chini ya miaka 20 (Tanzanite Queens), kwa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia mwaka
2026. Ushindi wenu ni historia na heshima kubwa kwa nchi yetu, ikiwa ni mara ya
kwanza Tanzania kufuzu kushiriki mashindano hayo.
“Ninaielekeza Wizara ya Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mamlaka zote zinazohusika kufanya
maandalizi bora yatakayoiwezesha timu yetu kuiwakilisha vyema Tanzania na
Afrika Mashariki katika mashindano hayo” alimaliza Rais Samia.
Tanzanite Queens imefikia rekodi
iliyowahi kuwekwa na timu ya Taifa ya wanawake ya vijana chini ya umri wa miaka
17 'Serengeti Girls' na ile ya timu ya taifa ya Wanawake ya Futsal ya kuwa timu
pekee za taifa za Tanzania zilizowahi kufuzu fainali za Kombe la Dunia chini ya
Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA).
Serengeti Girls ilishiriki fainali
za Kombe la Dunia mwaka 2022 na kuishia katika hatua ya robo fainali wakati
katika Futsal, Tanzania iliishia katika hatua ya makundi.
Kocha Mkuu wa Tanzanite Queens,
Bakari Shime anaandika rekodi ya kuwa kocha pekee wa soka Tanzania kuwahi
kuzipeleka timu mbili za taifa katika fainali za Kombe la Dunia mara ya kwanza
aliiongoza Serengeti Girls kufuzu fainali zilizofanyika India.
Shime alisema haikuwa kazi rahisi
bali akawapongeza wachezaji kwa kuichukua mechi kutoka Cameroon na kuja
kuimaliza hapa nchini.
“Wachezaji wamejitolea, wameshindana
kitu ambacho ilikuwa shida yetu kubwa kwenye mpira wa miguu wa wanawake kwa
hiyo kiwango cha ushindani kilikuwa kidogo lakini kwenye mechi hii umeona
tumeweza kuvumilia nguvu za wapinzani wetu na mwisho tukapata matokeo mazuri”
alisema Shime.

Post a Comment