TRILIONI MOJA KUIMARISHA UCHUKUZI MAZIWA MAKUU

 



Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kwa dhati kuubadilisha muonekano wa sekta ya uchukuzi nchini kwa kuwekeza kiasi kikubwa cha zaidi ya shilingi trilioni moja katika miradi ya usafiri wa majini.

Msemaji Mkuu wa Serikali, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo,Ndugu Gerson Msigwa, amebainisha kuwa uwekezaji huo mkubwa unalenga kununua meli mpya, kukarabati zilizopo, na kuboresha miundombinu ya bandari katika maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika, Nyasa, na ukanda wa Bahari ya Hindi.

Akizungumza na waandishi wa habari machi 22,2026 alisema hatua hii ni sehemu ya mkakati wa serikali wa kuunganisha huduma za usafirishaji na reli ya kisasa ya SGR ili kujenga ushoroba wa kati wenye tija, ambao ni kiungo muhimu kwa nchi jirani zisizo na bahari kama Uganda, DRC, na Burundi.

Kupitia uwekezaji huu, Tanzania inajipanga kuwa kitovu cha biashara kikanda, jambo litakalochochea ukuaji wa pato la taifa na kuimarisha ushindani wa bidhaa za ndani katika masoko ya kimataifa.

Akizungumza akiwa mkoani Mwanza, Msigwa alisisitiza kuwa kukamilika kwa meli kubwa ya MV Mwanza 'Hapa Kazi Tu' kwa gharama ya jumla ya shilingi bilioni 120 ni kielelezo cha mafanikio hayo, ambapo meli hiyo ina uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo.

Aidha, serikali inaendelea na ujenzi wa meli nyingine mpya ya mizigo katika Ziwa Victoria itakayobeba tani 3,000 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 145.4.

Miradi hii inakwenda sambamba na ukarabati wa meli za kimkakati kama MV Umoja uliogharimu dola za Marekani 8,830,521.62 ambazo ni sawa na Shilingi bilioni 22.9 na MT Ukerewe unaogharimu Shilingi bilioni 7.5.

Uwekezaji huu siyo tu unaimarisha sekta ya uchukuzi, bali pia unashusha gharama za usafirishaji kwa wafanyabiashara ikilinganishwa na usafiri wa barabara, hali inayopunguza bei za bidhaa kwa mlaji wa mwisho na kukuza uchumi wa kaya.

No comments