Rais Samia Apokea Ripoti ya Maboresho ya Kodi: Mkakati wa "Kuvua Gamba" waandaliwa



Na Mwandishi Wetu, BSKY Media

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepokea rasmi ripoti ya Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi nchini, huku akiahidi utekelezaji wa mapendekezo hayo kwa awamu ili kuendana na mahitaji ya sasa ya kiuchumi.

Hafla hiyo iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 18 Machi, 2026, inaashiria hatua kubwa ya mabadiliko tangu tathmini ya mwisho ya aina hiyo iliyofanywa na Tume ya Mtei takribani miaka 35 iliyopita (1989–1991).

Mambo Muhimu Katika Ripoti Hiyo:

  • Idadi ya Mapendekezo: Tume imewasilisha jumla ya mapendekezo 284 ambayo Rais ameahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi kupitia mikakati ya muda mfupi, kati, na mrefu.
  • Ongezeko la Mapato: Inakadiriwa kuwa utekelezaji wa mapendekezo haya unaweza kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha TZS trilioni 11.025 ndani ya miaka mitatu ya mwanzo.
  • Lengo la Kikodi: Tanzania inalenga kufikia uwiano wa mapato ya kodi kwa Pato la Taifa (Tax-to-GDP ratio) wa asilimia 18.
  • Dira ya 2050: Maboresho haya ni sehemu ya maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuchangia asilimia 70 ya mapato.

"Hata Nyoka Hujivua Gamba"

Akizungumzia ulazima wa mabadiliko hayo, Rais Samia amesisitiza kuwa mfumo wa sasa unapaswa kubadilika ili uwe wa haki, usio na tafsiri kinzani, na usioumiza biashara.

"Pamoja na changamoto za mfumo wa kodi, mabadiliko ni lazima na muhimu. Hata nyoka hujibadilisha, hujivua gamba. Sisi pia tunapaswa tubadilike," alisema Rais Samia.

Changamoto Zilizoibuliwa na Tume

Mwenyekiti wa Tume hiyo, Balozi Ombeni Sefue, alibainisha kuwa mfumo wa sasa unakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo:

  1. Viwango vikubwa vya kodi na tozo fulani.
  2. Udhaifu katika utatuzi wa migogoro ya kodi.
  3. Uratibu hafifu miongoni mwa taasisi zinazokusanya mapato.
  4. Wigo mdogo wa walipakodi, hali inayofanya kodi kukusanywa kutoka kwa watu wachache.

Balozi Sefue alionya kuwa bila mabadiliko makubwa, nchi itaendelea kukamua maziwa bila "kulisha ng'ombe," akimaanisha lazima mfumo uimarishe uwekezaji ili uweze kuzalisha kodi endelevu.

 

No comments