ULINZI WA BAHARI SASA USIPIME

 


 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Profesa Palamagamba Kabudi amesema Sh bilioni 5.8 zimetumika kukamilisha mradi wa kuimarisha ufuatiliaji wa ulinzi wa bahari katika maji ya Pwani ya Tanzania kufuatia athari za mgogoro wa Bahari Nyekundu.

Pamoja naulinzi uwepo wa mradi huo unatatua changamoto za kiusalama na kukuza maendeleo kwa wananchi.

Akieleza kuhusu mradi huo ulioanza Machi 2025 na kukamilika baada ya uzinduzi wa boti mbili za doria zenye mwendokasi mkubwa ziitwazo PB Sailfish 2 na PB Sailfish 3, Profesa Kabudi alibainisha kuwa uwekezaji huo unalenga kukabiliana na uhalifu katika mwambao wa Pwani uliosababishwa na ongezeko la mashambulizi ya wanamgambo wa Houthi katika Bahari Nyekundu yaliyotishia usalama wa meli na kuongeza gharama za usafirishaji.

Mbali na boti hizo zenye uwezo wa kubeba watu 12 kila moja na kufika Zanzibar kwa nusu saa pekee, Profesa Kabudi alieleza kuwa mradi huo ulijumuisha mafunzo ya kuwajengea uwezo vikundi vya wakulima wa mwani, ujenzi wa kaushio la mwani, na ununuzi na usambazaji wa mashine za kusaga mwani kwa ajili ya kuongezea thamani mazao yao katika Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga.

Makamu Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP), Profesa Provident Dimoso alibainisha kuwa chuo hicho kilisimamia ununuzi wa boti hizo kwa kuzingatia sheria za umma na viwango vya kimataifa ambapo boti hizo ziliharimu Sh bilioni 4.2 zikiwa na uthabiti wa hali ya juu, mifumo ya kisasa ya urambazaji na mawasiliano kwa ajili ya doria na operesheni za uokoaji.

Naye Balozi wa Japan nchini, Mikami Yoichi alipongeza hatua hiyo na kueleza imani yake kuwa serikali ya Tanzania itahakikisha boti hizo zinatumika kwa ufanisi na zinatunzwa ipasavyo ili ziweze kuleta tija kwa taifa kwa miaka mingi ijayo.

 

No comments