WANDISHI WA HABARI WAPATIWA MAFUNZO YA KUDHIBITI UHALIFU



Wandishi wa habari Mkoa wa Pwani wamepatiwa mafunzo maalum na Jeshi la Polisi kuhusu mfumo mpya wa kidijiti unaowezesha wananchi kutoa taarifa za viashiria vya uhalifu kabla matukio hayajatokea.

 Akitoa mafunzo hayo, Mkuu wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa Polisi Mkoa wa Pwani, Godfrey Ngowi, alieleza kuwa mfumo huo unajulikana kama CEWER na umebunmiwa mahususi kurahisisha upatikanaji wa taarifa za matukio yanayopangwa kufanyika ili yaweze kuzuiwa mapema. 

Alisisitiza kuwa waandishi wa habari ni wadau muhimu wenye uwezo mkubwa wa kufikisha ujumbe huo kwa jamii ili wananchi wengi waweze kuufahamu na kuutumia kikamilifu katika kulinda usalama wao.

Ngowi alifafanua kuwa tofauti na mifumo mingine inayotumika kusubiri tukio litokee ndipo hatua zichukuliwe, mfumo huu unalenga kudhibiti uhalifu tangu katika hatua za awali za viashiria vyake. Aliongeza kuwa mfumo huo umeundwa kwa ustadi mkubwa kuhakikisha usiri wa watoa taarifa unalindwa kikamilifu, ambapo mwananchi anaweza kuchagua kuficha jina lake au namba yake ya simu endapo hataki utambulisho wake ufahamike, jambo litakalowapa wananchi ujasiri wa kuripoti bila hofu ya kujulikana.

Kuhusu kasi ya utendaji kazi, Ngowi alieleza kuwa taarifa zinazotolewa kupitia mfumo huo zitawafikia viongozi wa ngazi zote kwa wakati mmoja kuanzia ngazi ya Polisi Kata, Wilaya, Mkoa, hadi Makao Makuu ya Polisi bila kuwa na ucheleweshaji wowote. 

Hali hiyo itawezesha ufuatiliaji wa karibu na kuchukuliwa kwa hatua za haraka za kuzuia uhalifu kabla madhara hayajatokea, hivyo kuimarisha usalama zaidi katika jamii kupitia ushirikiano wa karibu kati ya wananchi na jeshi la polisi.

No comments