Citibank Kuendelea Kushirikiana na Tanzania Kwenye Masoko ya Mitaji na Miundombinu
Benki ya
Kimataifa ya Citibank imethibitisha nia yake ya dhati ya kuendelea kuimarisha
ushirikiano wa kimkakati na Tanzania, ikiwemo kutoa ushirikiano mkubwa katika
masoko ya mitaji ya ndani na kimataifa, ufadhili wa miradi ya kimkakati ya
miundombinu, na uwekezaji wa sekta binafsi.
Hayo
yamejiri katika mkutano wa kimkakati uliofanyika jijini London, nchini
Uingereza, kati ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, na Afisa Mkuu
Mtendaji wa Citibank anayesimamia Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Bwana
Akin Dawodu.
Mkutano huo
ulikuwa na lengo la kukuza zaidi uhusiano wa kifedha uliodumu tangu benki hiyo
ianze shughuli zake nchini humo mwaka 1995.
Katika
mazungumzo hayo yaliyowashirikisha pia Balozi wa Tanzania nchini Uingereza,
Balozi Mbelwa Kairuki, na Kamishna wa Idara ya Deni la Serikali, Bw. Japhet
Justne, viongozi hao walipitia uwezo wa nchi kukopesheka kimataifa na mipango
ya kuanzisha hati fungani ya kimataifa ya Eurobond hapo mbeleni.
Aidha
walizungumzia ufadhili wa mabenki ya mikopo ya usafirishaji, pamoja na mageuzi
ya soko la mitaji.
Citibank
ilikubali kuunga mkono Tanzania katika adhima yake ya kufikia masoko ya mitaji
barani Ulaya, Marekani, Mashariki ya Kati na Asia, huku ikisifiwa kwa mchango
wake katika ukuaji wa kiuchumi.
Waziri
Balozi Omar aliwatangazia wawekezaji hao maendeleo makubwa ya kiuchumi nchini,
akionesha ongezeko la uzalishaji wa umeme, ukarabati mkubwa wa bandari za Dar
es Salaam, Tanga, na Mtwara, na upanuzi wa miundombinu ya anga, sambamba na
kuanza kwa utekelezaji rasmi wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kuanzia Julai
mwaka huu.
Alisema
Dira hiyo imelenga kufikisha uchumi wa Tanzania kufikia dola za Marekani
trilioni moja katika kipindi cha miaka 25 ijayo, ambapo asilimia 70 ya
uwekezaji huo inatazamiwa kutoka sekta binafsi.
Vilevile,
aligusia kukamilika kwa kiasi kikubwa kwa mazungumzo ya mradi mkubwa wa gesi
asilia wa LNG wenye thamani ya dola bilioni 42 za Marekani.
Kuhusu
mazingira ya biashara na kodi, Waziri huyo alieleza kuwa Serikali inafanyia
kazi mapendekezo 284 yaliyotolewa na tume maalum zilizoundwa na Rais Dkt. Samia
Suluhu Hassan ili kuboresha mfumo wa kodi na biashara, akisisitiza kuwa mageuzi
yajayo yatajikita katika kupanua wigo wa kodi na kuimarisha rasilimali za ndani
badala ya kuongeza mizigo kwa wananchi. Katika mkutano huo Balozi Omar alipendekeza
kuanzishwa kwa mfumo rasmi wa ushirikiano wa kimkakati kati ya Serikali na
Citibank utakaogusa masoko ya mitaji, ufadhili wa miundombinu, na uhamasishaji
wa sekta binafsi ili kuharakisha maendeleo ya nchi.




Post a Comment