ZAIDI YA WANANCHI 180 WANUFAIKA NA MATIBABU YA BURE DAR ES SALAAM
Mkurugenzi
Mtendaji wa Hospitali Bingwa ya MDM Urology,
Deogratius E. Mahenda, na Mkurugenzi wa Kituo cha Huduma za Afya
Nyumbani cha Nilax, May C. Moshatsi, kwa nyakati tofauti wamesisitiza
umuhimu wa kuimarisha programu za elimu ya afya kwa jamii na
kupanua wigo wa vipimo vya magonjwa yasiyoambukiza ili kusaidia utambuzi wa
mapema na kuokoa maisha ya wananchi
Wametoa
kauli hizo baada ya kuhitimishwa kambi maalum ya matibabu ya siku mbili
iliyolenga kusogeza huduma za afya karibu na jamii
Kambi
hiyo iliyofanyika kwa siku mbili hivi karibuni, ilihusisha jopo la wataalamu wa
fani mbalimbali za udaktari waliotoa huduma za ushauri, vipimo, utambuzi wa
magonjwa, pamoja na elimu ya afya kwa umma baada ya kupata idhini kutoka
serikalini
Katika kambi hiyo, jumla ya wagonjwa 182 walihudumiwa
katika idara tofauti za kibingwa na zile za kawaida
Idara
ya macho (Optometrists) iliongoza kwa kuhudumia wagonjwa 43, ikifuatiwa na
idara ya uchunguzi wa saratani iliyohudumia wanawake 36, huku daktari wa
kawaida akihudumia watu 30
Idara
nyingine zilizotoa huduma ni pamoja na meno (wagonjwa 29), mfumo wa mkojo na
uzazi kwa wanaume (wagonjwa 26), magonjwa ya wanawake (wagonjwa 10), pamoja na
idara ya mifupa iliyohudumia wagonjwa 8
Ripoti ya kambi hiyo imebainisha kuwa katika idara ya
mfumo wa mkojo (Urology), matatizo yaliyoonekana zaidi ni pamoja na maambukizi
ya njia ya mkojo (UTI), kutanuka kwa tezi dume (BPH), mawe kwenye figo, na
changamoto za kushindwa kutoa mkojo
Kwa
upande wa uchunguzi wa saratani ya matiti, uliofanywa na Taasisi ya Shujaa kwa
kushirikiana na Hospitali ya Saratani ya Ocean Road, wanawake wote 36
waliofanyiwa vipimo walikutwa wakiwa salama bila dalili zozote za ugonjwa huo
Aidha, changamoto nyingine za kiafya zilizojitokeza ni
pamoja na matatizo ya kutoona vizuri na maambukizi ya macho, matatizo ya meno
kama kuoza na maumivu ya fizi, pamoja na magonjwa ya mifupa kama maumivu ya
mgongo na viungo
Katika
kliniki ya kawaida, magonjwa ya malaria, shinikizo la juu la damu, na
maambukizi ya njia ya hewa yalikuwa miongoni mwa malalamiko makuu ya wagonjwa
waliofika kambini hapo
Post a Comment