Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Friday, September 20, 2013

MAMBO YA CRISTIANO RONALDO MUACHIE LIONEL MESSI



TIMU nyingine 16 za Ligi ya Mabingwa zilionyeshana kazi juzi Jumatano na kuwepo na matukio ya kushangaza kuliko yale ya Jumanne.

Chelsea wakiwa na matumaini ya kuanza vizuri, wakiwa chini ya kocha wao, Jose Mourinho, wakiwa nyumbani dhidi ya Basel,  mambo yalikuwa mabaya.
Pamoja na Arsenal kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, lakini walikumbana na upinzani mzito kutoka kwa wenyeji wao, Marseille.

Barcelona waliwakaribisha Ajax katika Uwanja wa Camp Nou na hii ilikuwa ndio mechi bab kubwa kwa usiku ule wa Jumatano.
Utamu zaidi ulikuwa pale Lionel Messi, alipopiga ‘hat-trick’ wakati Barca wakiibuka na ushindi wa mabao 4-0.

Kwa sasa Messi amefikisha mabao 62 kwenye Ligi ya Mabingwa na kuwa mchezaji wa kwanza kufunga zaidi ya ‘hat-trick’ katika ligi hiyo, huku akiwa ameifungia klabu yake ya Barca ‘hat-trick’ 24.
Siku moja kabla ya Messi kupiga ‘hat-trick’, mpinzani wake, Cristiano Ronaldo, na yeye alipiga ‘hat-trick’ wakati Real Madrid wakiichapa Galatasaray mabao 6-1 katika ligi hiyo ya mabingwa na kuonekana kama vile amejibu mapigo kwa mpinzani wake huyo.
Baada ya ‘hat-trick’ ya Ronaldo, baadhi ya wachambuzi wa soka walionekana kumkebehi Messi na kusema hana kitu.

Lakini kwa hat-trick hiyo ya Leo Messi, amedhihirisha kuwa alistahili kuwa mshindi wa tuzo ya mchezaji bora wa dunia (Ballon d'Or) kwa mara ya nne.
Wachezaji hao, wamekuwa na upinzani mkubwa uwanjani hata katika kinyang’anyiro cha tuzo za Ballon d'Or na kila mara Messi ameonekana kuwa kidume.

Huenda Messi, ameshawishiwa na ‘hat-trick’ ya Ronaldo, hivyo hakuna budi mambo ya Ronaldo tumuachie Messi ashughulike nayo mwenyewe uwanjani.

Pamoja na klabu hizo kunyakua mataji nane ya Ligi ya Europa na Ligi ya Mabingwa kwa pamoja, Barcelona na Ajax hawajawahi kukutana kabla ya mechi ya juzi ya Kundi H kwenye Uwanja wa Nou Camp.
Zaidi ya yote, Messi alionyesha kiwango kikubwa kama msimu ule wa mwaka 2009 na 2011, ambao waliibuka na mataji lukuki.
Ushindi huo ulikuwa mahususi kwa Kocha wa Barca, Gerard Martino, ambaye atakwenda Argentina kwenye mazishi ya baba yake.

“Ilikuwa mechi ya aina yake. Inauma kwa kile kilichotokea, lakini wote tuko pamoja naye,” alisema Messi, akimzungumzia kocha wake, Martino.
Ajax walikuwa chini ya kiwango chao kile walichoonyesha mwaka 1995 waliponyakua taji lao la nne la Ligi ya Mabingwa.

Bao la kwanza la Messi lilikuwa la mpira wa adhabu, ambao aliupiga karibu na lango la wapinzani na kugonga mwamba kabla ya kutinga wavuni.
Lile la pili lilikuwa la aina yake, baada ya Messi kupokea pasi kutoka kwa kiungo Sergio Busquets, akiwa upande wa kulia na kuingia nao ndani na kuachia shuti kwa mguu wake wa kushoto na kuandika bao la pili kwa Barca.

Beki wa kati wa Barca, Gerard Pique, naye alifunga kwa kichwa, akiunganisha mpira wa krosi uliopigwa na Neymar kutoka upande wa kushoto.

Lakini, Messi hakutaka kuwaachia nafasi wengine wang’ae, baada ya kupachika bao lake la tatu na la nne kwa klabu yake, baada ya kupokea pasi ya Xavi, dakika ya 15 kabla ya mpira kumalizika.
Mambo yalikuwa mabaya zaidi kwa Ajax, pale Kolbeinn Sigthorsson aliposhuhudia penalti yake ikidakwa na mlinda mlango wa Barca, Victor Valdes, baada ya Javier Mascherano, kumuangusha Thurani Serero.

Katika mechi hizo za makundi, mechi nyingine ilikuwa ni ile ya AC Milan, ambao waliepuka aibu ya kutoka sare na Celtic katika uwanja wao wa San Siro, baada ya Emilio Izaguirre kujifunga mwenyewe na Sulley Muntari kuongeza bao jingine na Rossoneri kuibuka na ushindi.

Mourinho, alishangazwa na matokea ya klabu yake ya Chelsea, baada ya kupokea kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya FC Basle katika Uwanja wa Stamford Bridge, kwenye mchezo huo wa Kundi E.
Wenyeji walionekana kuongoza, baada ya nyota wa Brazil, Oscar, kuwafungia bao la kwanza, akiitumia vizuri kazi nzuri ya David Luiz na Frank Lampard.
Oscar alipata nafasi nyingine ambayo angeweza kuongeza bao la pili, lakini shuti lake liligonga mwamba.

Nyota wa Basel, Mohamed Salah, aliupitisha vizuri mpira jirani na Ashley Cole na kutinga wavuni katika dakika ya 71, kabla ya Marco Streller kupiga bao jingine la kichwa na Basel kupata ushindi wasioutarajia.

Mourinho, alionekana kuwa mtulivu na kusema: “Sijashtuka. Huo ndio ukweli,  wakati mwingine hupati ushindi. Kiukweli sina furaha. Tumerudishwa nyuma katika harakati za kufuzu, lakini tumebakiza mechi tano na tutamaliza tukiwa katika nafasi mbili za juu.”
Schalke 04 wanaliongoza kundi hilo, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Steaua Bucharest.

Nyota wa Japan, Atsuto Uchida na kiungo wa Ghana, Kevin-Prince Boateng na nyota wa Ujerumani, Julien Draxler, ndio waliotingisha nyavu za Steaua Bucharest na kuipa Schalke ushindi huo.
Mshindi wa pili msimu uliopita, Borussia Dortmund, amekumbwa na majanga, baada ya kuanza vibaya kwa kupokea kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Napoli, katika mchezo wa Kundi la F, ambalo linajulikana kama Kundi la Kifo.

Ilikuwa huzuni kwa Wajerumani hao, ambao mwishoni mwa wiki waliichapa Hamburg mabao 6-2, kufuatia kocha Jurgen Klopp na mlinda mlango Roman Weidenfeller wote kuonyeshwa kadi nyekundu,  baada ya Gonzalo Higuain kufunga bao la kuongoza.
Lorenzo Insigne, aliongeza bao la pili kwa Napoli, kabla ya bao la kujifunga mwenyewe la Camilo Zuniga.

Arsenal waliungana na Napoli kileleni mwa kundi hilo la kifo, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Marseille, katika Uwanja wa Stade Velodrome.
Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger, alisema bao la kwanza ndio lilikuwa msingi wa ushindi.
“Nilijua tangu matokeo yakiwa 0-0, baada ya nusu saa nilikuwa na uhakika kuwa timu itakayopata bao la kwanza ndiyo itakayoibuka na ushindi,” alisema Wenger.

Winga Theo Walcott, alifunga bao la kwanza kwa shuti kali, kabla ya Aaron Ramsey, kuendelea kuonyesha kiwango chake kizuri kupachika bao la pili na la sita kwa msimu huu.
Jordan Ayew, alifunga bao la penalti dakika za majeruhi, baada ya Ramsey, kumuangusha Jordan na Andre Ayew.

Atletico Madrid walikuwa na usiku mzuri kwa kuwachapa wageni wao, Zenit St Petersburg mabao 3-1.
Miranda, alifunga bao la kwanza kabla ya nyota wa Brazil, Hulk kusawazisha.
Lakini, mabao kutoka kwa Arda Turan na Leo yaliifanya Atletico kuongoza Kundi G, juu ya Porto, ambao wameshinda bao 1-0 ndani ya Uwanja wa Austria Vienna, likifungwa na Lucho Gonzalez.

No comments:

Post a Comment