Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, August 1, 2013

SAKATA LA YANGA NA HAKI ZA TV ULAYA


* England inategemea nafasi ya timu kwenye ligi
* Hispania ni uwezo, nguvu ya timu
* Wingi wa mashabiki, historia vigezo Italia

STORI kubwa kwenye vyombo vya habari wiki hii, ni kitendo cha klabu ya Yanga kupinga mechi zake kuonyeshwa na kituo cha televisheni cha Azam.
Kila mtu amesema yake kuhusiana na sakata hilo, kuna wanaoiponda Yanga na wale wanaoiunga mkono kwenye ishu nzima ya haki za televisheni.

Pande zote mbili kwenye sakata hili zinahoja, kwa sababu kila mtu anasema kile anachokiamini yeye kwa mtazamo wake.
Makala haya hayajalenga kuegemea upande wowote katika sakata hili, lakini kwa sababu lengo la kila kinachofanyika ni kutaka ligi ya Tanzania kuwa na ubora kama wa nchi za Ulaya, basi tumeona kuna umuhimu wa kuangalia wenzetu wanafanya nini na kulinganisha na hali ilivyo kwenye sakata hili.

Mkataba wa Azam Tv
Dili la televisheni la Azam Tv ni la miaka mitatu, ambalo thamani yake ni shilingi bilioni 5.56, huku wakitaka kuonyesha jumla ya mechi 182 kati ya hizo 60 tu ndio moja kwa moja (live), nyingine zitakuwa zilizorekodiwa.
Katika dili hili, Azam Tv watakuwa na haki ya kuonyesha mechi nne za kila timu kwa msimu, huku wakitoa kiasi cha shilingi milioni 100 kwa timu zote, lakini kiasi hicho kitapanda kadri miaka inavyosonga mbele.
Asilimia 25 ya hizo milioni 100 itatolewa kwa klabu kabla ya ligi kuanza na kipengele muhimu kuliko vyote ni kwamba, hakuna timu itakayolipwa zaidi ya mwenzake.

Madai ya Yanga
Katika kupinga michezo yao kuonyeshwa, Yanga wamekuja na hoja tano, ambazo Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Yusuf Manji alizieleza kwa wanahabari.
Hoja ya kwanza inakichwa cha Bodi ya Tanzania Premier League, wanadai kwamba bodi iliyoko sasa ni ya mpito na haikuchaguliwa kidemokrasia na haitakiwi kuingia mikataba ya muda mrefu wakati huu ikikaribia kuondoka madarakani, pia haina mjumbe hata mmoja kutoka Yanga.

Hoja ya pili ya Yanga ni utaratibu wa dunia nzima, humu wamesema hakuna sehemu yoyote duniani timu ikalazimishwa kuachia haki zake za televisheni, huku pia wakipinga kugawana sawa mapato ya televisheni na timu nyingine kwa kudai kwamba kipengele cha nafasi ya timu kwenye Ligi lazima kiangaliwe na pia mkataba huo umekosa viwango (Premiums) na kusisitiza hii itapoteza ushindani kwenye ligi.

Hoja ya tatu ya Yanga ni kwamba, migogoro ya maslahi, humu wamedai kwamba Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Mpito ya TPL ni Mkurugenzi mwandamizi wa Makampuni ya Azam na  kwa hivyo mazungumzo ya siri kati ya Bodi ya TPL na Azam ni ya kutiliwa mashaka.

Pia wameeleza kwamba, Makampuni ya Azam yanashindana kibiashara na makampuni mengi yakiwemo ya utengenezaji wa vinywaji baridi, hivyo hili litahatarisha biashara na udhamini wa Yanga kutoka kwa makampuni mengine yenye upinzani na Yanga. Pia wakadai kwamba Azam FC wanauadui wa kimichezo na Yanga, wakitolea mfano sakata la Mrisho Ngassa kupelekwa Simba kwa mkopo.

Hoja ya nne ni kukosekana kwa uwazi, katika hili walidai kwamba, mchakato mzima wa kurusha matangazo ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara ulifanywa kwa siri na hakushindanishwa, huku wakiongeza kwamba hata Yanga ilipoomba kuupitia mkataba huo kisheria ilinyimwa.

Na la mwisho ni mazingatio ya kibiashara, wanadai kwamba, Mahakama ya Kisheria ndiyo yenye haki ya kuamua mzozo wowote leseni na siyo FIFA, lakini TPL wanasingizia ni FIFA, wanasema wahusika wote wanatakiwa kuhusishwa kwenye mchakato huo kwa sababu una maslahi ya kibiashara. Pia walizungumzia kuhusu kupungua kwa mapato ya mlangoni ambayo ni chanzo muhimu cha mapato cha Yanga ambapo kila mchezo wanaweza kuingiza milioni 50 na zaidi, ni zaidi ya milioni 8.2 ambazo zitapatikana katika mapato ya televisheni.
Baada ya kuona ofa ya Azam Tv na madai ya Yanga, sasa tuangalie wenzetu walioendelea hali ikoje.

Hali ilivyo England
England ndiyo nchi ambayo huvuna kiasi kikubwa cha fedha kwenye suala zima la urushwaji wa mechi zake kwenye televisheni, na hivi ndivyo mchakato mzima ulivyo.
Mkataba wa kurusha matangazo ya redio na televisheni Ligi Kuu England, huuzwa kwa miaka mitatu mitatu na hufanywa kwa mfumo wa mnada. Haki huuzwa katika mafungu sita na kila fungu linaonyesha mechi 23, na hakuna televisheni moja ambayo hupewa haki ya kununua mafungu yote sita. Mafungu hayo hupewa jina la A-F na yanatofautishwa na muda wa mechi kurushwa.

Ligi Kuu England huuza haki zake za televisheni kwa ujumla wa timu zote na siyo timu moja moja kuuza haki zake, hii hutengeneza ‘balance’ ya mapato.
Kwenye Ligi Kuu England mapato ya haki za televisheni, hugawanywa kwa wastani wa 50:25:25; Asilimia 50 hugawanywa sawa miongoni mwa klabu, asilimia 25 hugawanywa kutokana na nafasi ambayo timu itamaliza kwenye Ligi na asilimia 25 nyingine hutolewa kama gharama za kutumia miundombinu ya klabu wakati wa kurusha matangazo. Wakati mapato yanayopatikana nje ya Uingereza, hugawanywa sawa miongoni mwa klabu 20 za Ligi Kuu England.

Mkataba wa sasa wa haki za televisheni nchini England, ni pauni bilioni 1.78 (shilingi trilioni 4.282), mkataba huo unatarajiwa kukua na kufikia kiasi cha pauni bilioni 5 (shilingi trilioni 12.03) siku za usoni.
Mapato ya kuuza haki za televisheni ndani ya England, yanaonyesha kwamba timu ambayo inamaliza juu kwenye ligi itapata fedha nyingi kuliko ile ya chini, wakati yale ya nje ya England yanagawanywa sawa kwa timu zote 20.

Mfano msimu uliopita, Manchester United waliokuwa mabingwa wa Ligi Kuu England, waliingiza kiasi cha pauni milioni 13.4 (shilingi bilioni 32.24) na Queens Park Rangers ilimaliza katika nafasi ya mwisho kwenye Ligi ilipata pauni milioni 5.8 (shilingi bilioni 13.955).

Hali ilivyo Ujerumani
Bundesliga wamesaini mkataba mpya wa kuonyesha mechi zao siku za karibuni, mkataba huo utakuwa kati ya mwaka 2013 -2016 na unaanza kufanya kazi rasmi msimu ujao.
Fedha za haki za televisheni kutoka ndani ya Ujerumani, ni euro milioni 628 (shilingi trilioni 1.318) na nje ya Ujerumani ni euro milioni 70 (shilingi bilioni 146.941) kwa msimu.

Mgawanyo wa fedha za haki za televisheni kwenye Bundesliga kwa msimu, ni tofauti na nchi nyingine za Ulaya, huku kuna mfumo wa pointi (Point System).
Asilimia 40 ya mapato yanagawanywa kulingana na pointi za timu kwenye msimu uliopo (kwa sasa ni msimu wa 2013-14), na nafasi kwenye ligi katika kila siku ya mechi inajumuishwa humu. Asilimia 30 inaangalia msimu uliopita (2012-13), asilimia 20 msimu kabla ya uliopita (2011-12), na asilimia 10 miaka mitatu iliyopita (2010-11).

Bingwa msimu wa 2010-11 anapewa pointi 36, mshindi wa pili 35 mshindi wa tatu pointi 34. Msimu wa 2011-12 mshindi wa kwanza anapata pointi 72, wa pili 70 na wa tatu 68, msimu wa 2012-13 mgawanyo wa pointi kwa timu tatu za juu ni 108, 105 na 102. Unaweza kuona pointi hizo zinazidishwa mara mbili.
Cha kuelewa hapa ni kwamba, pointi hizi zinatumika kujua timu itakuwa nafasi ya ngapi wakati wa mgao wa mapato ya televisheni. Timu yenye pointi nyingi itashika nafasi ya kwanza (msimu wa 2013-14) na itapata euro 760,000 zaidi ya mshindi wa pili, tofauti hii itaendelea kuongezeka mpaka kwa timu iliyoshika mkia. 

Tofauti ya bingwa na aliyeshika mkia mara mbili zaidi. Hali ilivyo sasa, Bayern watapata euro milioni 25.84 (shilingi bilioni 54.242), Dortmund euro milioni 25.07 (shilingi bilioni 52.626) wakati timu iliyoshika mkia Greuther Furth, ilipata euro milioni 12.92 (shilingi bilioni 27.121) kwa msimu ujao.
Pia kuna kiasi kidogo cha fedha kinatolewa kwa timu kutokana na haki stahiki, hii inategemea idadi ya mechi zake ilivyoonyeshwa na klabu zake.

Hali ilivyo Hispania
Hispania sasa hivi wanajaribu kubadili mfumo wake kutoka ule wa haki za televisheni kutawaliwa na Real Madrid na Barcelona, mpaka ule wa angalau mgao sawa.
Mfano msimu uliopita, Real Madrid iliingiza euro milioni 140 (shilingi bilioni 293.883) kwa kuuza haki zake za televisheni, timu iliyowakaribia ni Barcelona ambao waliingiza euro milioni 134 (shilingi bilioni 281.288), wakati hali ikiwa hivyo kwa Barca na Madrid timu nyingine zimekuwa zikipata kiasi kidogo sana mfano Granada walifanikiwa kupata euro milioni 12 (shilingi bilioni 25.189).

Sasa hivi Serikali ya Hispania inaangalia uwezekano wa kuanzisha sheria ambayo itazibana Barca na Madrid na kuuza kwa pamoja haki zao za televisheni na kuziwezesha timu nyingine angalau kupambana nao.
Barcelona na Real Madrid wanaingiza mara 10 zaidi ya timu nyingine 12 za La Liga, ni Atletico Madrid na Valencia ambazo angalau wanakaribiana na timu hizo mbili, japo nao wameachwa mbali kiuhalisia.

Hali ilivyo Italia
Serie A, Novemba mwaka jana waliingia mkataba mpya wa televisheni ambao utadumu kati ya msimu wa 2012-13 hadi 2014-15, mkataba huo unathamani ya euro milioni 840 (shilingi trilioni 1.763), katika dau hilo timu zinazoshuka daraja zitapewa euro milioni 30 (shilingi bilioni 62.974) kwa ajili ya kuwasaidia huko chini.
Tofauti na England ambapo hupanga mgawanyo mzima mwisho wa msimu, Italia mgawanyo hufanywa kabla ya msimu kuanza hasa kwa kuangalia taarifa za kihistoria.

Kuna vitu vitano vinaangaliwa wakati wa kugawanya fedha za haki za televisheni na vitu hivyo ni pamoja na:-
Dau la pamoja (Dau Fixed Amount Element), ambalo kila timu hupata pauni milioni 15.2 (shilingi bilioni 36.571).
Ishu ya pili ni Idadi ya mashabiki (Supporters Index Element), hapa kuna asilimia 25 ya mapato yote, idadi hii hujulikana kupitia utafiti uliofanywa na makampuni mbali mbali na kuna jumla ya mashabiki milioni 37.6 nchini Italia. Juventus ambao wanatajwa kuwa na mashabiki wengi zaidi hufaidika hapa na hupata pauni milioni 45 (shilingi bilioni 108.272), kulinganisha na Siena yenye mashabiki wachache hupata pauni milioni 1.2 (shilingi bilioni 2.887).

Kitu cha tatu wanaangalia ni Idadi ya watu kwenye mji timu inatoka (Town Population), kipengele hiki fedha hugawanywa kulingana na idadi ya watu kwenye mji timu inatoka, hapa timu mbili za Turin (Torino na Juventus), wanapata dau sawa. Wanaofaidika sana hapa ni Roma wanapata pauni milioni 5 (shilingi bilioni 12.5), kulinganisha na Siena na Chievo wanaopata pauni 300,000 (shilingi milioni 721.8).
Nafasi ya msimu uliopita (last season performance), kuna dau ambalo hupangwa kutokana na nafasi ambayo timu ilimaliza msimu uliopita, hapa ni asilimia tano tu ya pato lote ndiyo hutolewa.

Misimu mitano iliyopita (Last 5 seasons) hapa kuna asilimia 15, mgao huu huangalia sana nafasi ambayo timu imemaliza kwenye misimu mitano iliyopita, timu kubwa ndiyo zinafaidika sana na hili kwa sababu zina uhakika wa kufanya vizuri kila msimu.
Sababu za Kihistoria (Historical Results Element), asilimia 10 ya mgao wote huwekwa hapa, historia hiyo ni kuanzia mwaka 1946, kwa mara nyingine Juventus na miamba ya Milan ndiyo inafaidika sana hapa kwa sababu wamekuwa juu kwa muda mrefu sana na historia inawabeba sana wao.

Hitimisho
Ni ndoto ya kila Mtanzania kuona siku moja Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, inakuwa kama zile za Ulaya na ili hili lifanikiwe ni lazima tufuate wanachokifanya kwa asilimia kubwa hata kama tutafanya yetu.

Na kwa jinsi hali ya mambo ilivyo kwenye nchi za wenzetu, hakuna hata nchi moja ambayo timu zote zinapata mgao sawa, hivyo basi kwa kuangalia na wanachokisema Yanga, utagundua kwamba kina mashiko kwa asilimia kubwa, haiwezekani timu ya mwisho kwenye ligi ipate mgao sawa na bingwa, hivyo basi TPL na Azam TV hawanabudi kuangalia upya mchakato mzima na kuja na mkataba bora ambao kila timu itaridhika nao.

No comments:

Post a Comment