Makamu wa Rais Ndejembi Awasili Vienna Kumwakilisha Rais Samia kwenye Jukwaa la Kimataifa la IAEA
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi amewasili mjini Vienna, nchini Austria, na kuongoza kikao cha maandalizi cha viongozi na wataalamu mbalimbali wa Tanzania watakaoshiriki Jukwaa la Kisayansi la Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA Scientific Forum).
Mhe. Ndejembi yuko nchini humo kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwenye jukwaa hilo la kimataifa linalotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 15 hadi 16 Septemba 2026, likiwa linafanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala huo (IAEA General Conference).
Kikao hicho cha maandalizi kinalenga kuweka mikakati thabiti ya ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo mkuu unaowakutanisha viongozi, wanasayansi, na wawakilishi wa nchi wanachama 181 kutoka duniani kote ili kujadili masuala mbalimbali ya matumizi ya amani ya teknolojia ya nyuklia, usalama, na ushirikiano wa kiufundi.
Mkutano huo wa mwaka unaofanyika kuanzia tarehe 14 hadi 18 Septemba 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Vienna (VIC), unatoa fursa maalum ya kujadili masuala mbalimbali ikiwemo mpango mkuu wa IAEA wa "Rays of Hope" unaolenga kupanua wigo na upatikanaji wa huduma za matibabu ya kansa duniani kote.
Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huu chini ya uongozi wa Makamu wa Rais unaonyesha dira na utayari wa nchi katika kushirikiana na jumuiya ya kimataifa kuendeleza matumizi salama ya sayansi na teknolojia ya atomu katika sekta za maendeleo, afya, kilimo, na usimamizi wa rasilimali za maji.
Kupitia mikutano hiyo ya kimataifa, wataalamu wa Tanzania wanapata fursa ya kubadilisha uzoefu, kujadili maazimio ya kukuza teknolojia safi, na kuimarisha ushirikiano utakaosaidia kuchochea maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.

Post a Comment