Goat Races ndani ya viwanja vya Posta, Septemba 19
Jumla ya mbuzi 80
wanatarajiwa kushiriki katika mbio za kihistoria za mbuzi zinazojulikana kama
The Goat Races ambazo zimelenga kukusanya Shilingi milioni 200 kwa ajili ya
kuchangia huduma mbalimbali za jamii.
Aidha mbio hizo mwaka huu
zimepangwa kufanyika Septemba 19 katika viwanja vya Posta Kijitonyama jijini
Dar es Salaam.
Akizungumza katika mkutano
na waandishi wa habari, Rais wa Rotary Club ya Dar es Salaam Oysterbay, Paul
Muhato, amesema kuwa fedha hizo zitaelekezwa katika kutoa ufadhili wa masomo
kwa watu waliopo na wanaojiunga na vyuo vikuu na vyuo vya kati, sambamba na
kuboresha masuala ya afya.
Katika mbio hizo
zilizohamishwa kutoka viwanja vya zamani vya Green Oysterbay kutokana na
maandalizi ya michuano ya Afcon 2027 na kupelekwa viwanja vya Posta, klabu hiyo
imejipanga kuvunja rekodi ya mwaka jana ambapo walifanikiwa kukusanya Sh
milioni 160.
“Goat Races ni tukio la kufurahia siku nzuri
pamoja huku tukifanya jambo lenye maana kwa jamii. Mwaka huu tunakuja kwa
ukubwa zaidi na tumeandaa Safari Adventure yenye burudani na msisimko kwa
familia nzima, yote ikiwa ni kwa ajili ya kusaidia jambo jema. Tunaualika umma
mzima kuungana nasi.”
Aidha Muhato alimtangaza
rasmi mdhamini mkuu wa tukio hilo kuwa ni Vodacom Tanzania itakayochangia Sh
milioni 150 pamoja na kugharamia uandaji wa tamasha hilo ambalo linatarajiwa
kuhudhuriwa na watu 5,000 huku muda wake ukiongezwa hadi saa nne usiku kuanzia
saa sita mchana.
Akizungumza wakati wa kutangazwa rasmi kwa
udhamini huo, Bwana Joseph Sayi, Mkuu
wa Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania, alisema kampuni hiyo
inajivunia kuendelea kuunga mkono mpango ambao tayari umeonyesha matokeo halisi
katika jamii.
“Ushirikiano wetu na Rotary Club of Dar es Salaam
Oyster Bay, ambao sasa umefikia mwaka wa nne, tayari umesaidia kuboresha
miundombinu ya shule na kutoa ufadhili wa masomo kwa zaidi ya wanafunzi 350 wenye uhitaji katika taasisi za elimu
ya juu na mafunzo ya ufundi stadi.
“ Mwaka huu, tunaendeleza mafanikio hayo kwa
kuboresha zaidi mazingira ya kujifunzia pamoja na huduma za maji, usafi na
usafi wa mazingira. Tunazialika taasisi nyingine kuungana nasi ili kwa pamoja
tuweze kuleta matokeo makubwa zaidi katika jamii.” Alisema Sayi
Mratibu wa Mbio za Mbuzi,
Bi. Rashida Nas, aliukaribisha ushirikiano unaoendelea kati ya
Vodacom Tanzania na Rotary, pamoja na mchango mkubwa wa wadhamini na washirika
wengine wanaorejea mwaka huu.
“Tunafurahi sana kuwa na Vodacom Tanzania kama
mdhamini wetu kwa mara ya nne, na tunawashukuru kwa kuendelea kutuamini, pamoja
na wadhamini na washirika wetu wote. Tukiwa katika eneo jipya na kubwa zaidi,
ambapo watoa huduma mbalimbali wa vyakula na vinywaji pamoja na burudani
watashiriki nasi siku nzima, Goat Races 2026 itakuwa ni sherehe
inayoonyesha nguvu ya ushirikiano katika kuleta mabadiliko katika sekta ya
elimu nchini Tanzania.”
Akielezea taratibu za
ushiriki na viingilio, Muhato amesema kuwa mtu au taasisi inayotaka kununua
mbuzi wa mashindano inawapata kwa Shilingi laki saba, dau ambalo ni sawa na
kukata tiketi nne za VIP kwa bei nafuu.
Tiketi moja ya VIP kwa sasa
inauzwa kwa Sh laki mbili na itapanda na kuwa Sh 230,000 mwezi ujao kabla ya
kuuzwa Sh 250,000 getini, wakati tiketi za kawaida zikiwa ni Sh elfu 30, watoto
wenye umri wa miaka 12 wakilipia elfu kumi, na watoto chini ya miaka mitano
wakiruhusiwa bure chini ya kauli mbiu ya Safari Adventure.
Katika ufafanuzi wake
kuhusu msaada wa elimu, Muhato alibainisha kuwa hadi kufikia mwaka huu wa 2026,
jumla ya watu 350 wamefadhiliwa kupitia mapato ya mbio hizo, ambapo kwa mwaka
jana pekee wa 2025 waliwafadhili watoto 100 katika vyuo mbalimbali, wanafunzi
30 wa vyuo vya ufundi na amali, pamoja na watu sita waliopata ufadhili katika
vyuo vya usafiri wa anga.
Muhato alisisitiza kuwa
ufadhili huo hutolewa kwa wenye mahitaji kupitia vigezo maalumu kama vile alama
bora za darasani, ukosekanaji wa ufadhili mwingine, na kupata nafasi ya chuo.
Mbali na burudani, chakula,
na msisitizo wa mavazi ya asili ya safari, tukio hilo litatoa zawadi mbalimbali
kwa washindi wa mbio na wale watakaovaa vizuri zaidi.
Wakati huo huo, Muhato
alibainisha kuwa Rotary ya Oysterbay ipo katika hatua za mwisho za kufanya
mpango wa kutiliana saini mikataba ya ushirikiano na wizara zinazohusika na
elimu na afya ili kuendeleza na kurahisisha juhudi zao za kuwezesha upatikanaji
wa huduma bora nchini, huku akiwasihi wananchi kutembelea tovuti ya
goatraces.tz kujipatia tiketi mapema.


Post a Comment