DC MPOGOLO ATOA SIKU 14 MKANDARASI KUKAMILISHA BARABARA YA MUHIMBILI


 


Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amempa mkandarasi China Wu Yi Construction siku 14 kuhakikisha uwekaji wa lami umeanza katika barabara inayopita eneo la Hospitali ya Taifa Muhimbili, huku akiagiza TARURA na TAKUKURU kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo wa DMDP II Package IV wenye thamani ya Shilingi bilioni 26.06.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua mradi huo wenye urefu wa kilomita 7.38 unaohusisha barabara 16, Mpogolo amesema kuwa barabara ya Muhimbili ni muhimu sana kwa wagonjwa na wananchi, hivyo haiwezi kuendelea kucheleweshwa wakati Serikali imekwisha kutoa zaidi ya Shilingi bilioni 5.

“Nataka ndani ya siku 14 barabara hii iwe imeanza kumwagwa lami. Meneja wa TARURA Wilaya ya Ilala simamia hili. Pia nataka TAKUKURU Wilaya ya Ilala ifuatilie commitment hii na kuhakikisha kila mmoja anawajibika kwa nafasi yake. Baada ya siku 14 tutarudi hapa kuona kazi iliyofanyika,” amesema Mhe. Mpogolo

Amesema kuwa pamoja na muda wa mradi kuongezwa kutoka Agosti 14 hadi Desemba 16, 2026, hilo halimpi mkandarasi sababu ya kufanya kazi kwa kusuasua, na kumtaka kuongeza mitambo, vifaa, wataalamu, pamoja na kufanya kazi mchana na usiku.

“Serikali imelipa fedha. Tunachotaka sasa si maelezo, tunataka matokeo. Ongezeni vifaa, ongezeni watu, ongezeni zamu na mfanye kazi usiku na mchana. Mradi huu ni wa wananchi na lazima tuone thamani ya fedha zao,” amesema.

Hadi sasa, mradi umefikia takribani asilimia 55 ya utekelezaji, huku Serikali ikiwa tayari imelipa zaidi ya Shilingi bilioni 5.

Aidha, amemtaka Mhandisi Mshauri, M/s Mhandisi Consultancy, kuwasilisha vielelezo vyote vya maandishi alivyomwandikia mkandarasi kutokana na kuchelewa kwa kazi hiyo, akisisitiza kuwa wasimamizi hao wanalipwa kupitia fedha za mradi na wanapaswa kuwajibika kikamilifu ili kuhakikisha wananchi wanapata thamani halisi ya fedha za umma.

“Tusilaumu Mkandarasi peke yake. Mhandisi Mshauri naye ana wajibu wake. Serikali inamlipa kupitia fedha za mradi ili asimamie kazi na kuhakikisha Mkandarasi anafanya kazi kwa mujibu wa mkataba. Nataka kuona barua na maelekezo yote uliyompa Mkandarasi, hatua ulizochukua na commitment yako ya kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati. Kila mmoja atawajibika kwa nafasi yake,” amesisitiza Mhe. Mpogolo.»

Ameongeza kuwa usimamizi wa mradi haupaswi kuishia kwenye nyaraka pekee, bali unapaswa kuonekana kupitia kasi ya kazi, ubora wa utekelezaji na matokeo yanayopatikana eneo la mradi.

“Unalipwa kwa ajili ya kusimamia. Tunataka usimamizi unaoonekana kwenye matokeo, si kwenye karatasi pekee. Commitment yako lazima ionekane kwenye kasi ya kazi ya Mkandarasi,” amesema.

Mhe. Mpogolo amesisitiza kuwa Meneja wa TARURA Wilaya ya Ilala pamoja na Mhandisi Mshauri wanapaswa kuongeza ufuatiliaji wa utekelezaji wa mradi na kuhakikisha maagizo yanayotolewa kwa Mkandarasi yanatekelezwa kwa wakati.

Mhe. Mpogolo ameeleza kuwa Wilaya ya Ilala itaendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa Mradi wa DMDP II Package IV ili kuhakikisha fedha za Serikali zinakwenda sambamba na thamani ya kazi inayofanyika na wananchi wanapata barabara bora kwa wakati.

Mradi wa DMDP II Package IV unahusisha ujenzi wa barabara 16 zenye urefu wa jumla ya kilomita 7.38, kwa gharama ya Shilingi bilioni 26.06, ukiwa unatekelezwa na China Wu Yi Construction.

No comments