Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Sunday, August 9, 2015

WALINUNULIWA GHALI CHELSEA WAKAGEUKA MAGARASA


CHELSEA ni moja ya klabu zilizopata kusajili wachezaji wengi wazuri; na hata sasa bado wanasajili vijana wadogo na kuwatoa mkopo kwa klabu mbalimbali maeneo tofauti duniani.

Wakati moja ya njia za klabu kujenga kikosi imara ni kuwa na msingi katika kusajili chipukizi au kupandisha wale walio kwenye akademia zake, kuna njia mbadala.

Njia hiyo ni kuvunja benki na kusajili wachezaji wenye majina makubwa. Tulipata kuona wachezaji wakubwa ambao Chelsea walisajili kwa kiasi kikubwa cha fedha na kuwafaa.

Leo hii tugeukie upande wa pili kwa kuangalia majina makubwa waliyosajili lakini dimbani mwao wakageuka kuwa magarasa na hasara tupu kwa klabu.


  Fernando Torres

Mchezaji huyu wa Hispania aliletwa Stamford Bridge kutoka Liverpool kwa ada iliyoshitua wengi ya pauni milioni 50.

Kocha mmoja baada ya mwingine waliotua hapo walishindwa kumtumia Torres aliyekuwa akishuka kiwango kadiri muda ulivyokwenda, akawa tofauti kabisa na nyota aliyekuwa Anfield.

Huyu amewekwa kwenye kundi la ununuzi mbaya zaidi katika historia ya soka ya England. Msimu uliopita Jose Mourinho alifikwa na maji shingoni kiasi cha kumbeza mshambuliaji huyo kwa kutoifanya kazi yake, ndipo akamuuza Atletico Madrid alikoanzia kung’ara.


Andriy Shevchenko

 

Huyu ndiye aliyekuwa akiitwa ‘The Original Torres’. Shujaa huyu wa Ukraine alipendwa sana na mmiliki wa Chelsea, Roman Abramovich, lakini ukweli ni kwamba kununuliwa kwake kwa pauni milioni 30 kutoka AC Milan 2006, alikuwa si yule wa awali.

Baada ya kuingia Chelsea miguu yake ilipatwa kigugumizi mara kwa mara na mashabiki wakashindwa kuelewa kulikoni. Ilibidi awekwe kwenye meli na kurejeshwa Milan kwa mkopo baada ya misimu miwili tu kisha akatupiwa virago moja kwa moja kwenda Dynamo Kiev 2009.


Chris Sutton

 

Huyu ni uthibitisho kwamba Chelsea walikuwa wakitumia fedha nyingi kwa wachezaji wasiotoa matunda tarajiwa, muda mrefu kabla hata mashabiki wa soka kumsikia Abramovich.

Chris Sutton aliwasili Stamford Bridge akitoka Blackburn kwa ada ya pauni milioni 10 ambayo kwa mwaka 1999 ilikuwa kubwa sana. Hakupata kufufuka tangu alipoanza kucheza kwa mara ya kwanza dhidi ya Sunderland, aliposhindwa kufunga bao la wazi kabisa akiwa na kipa Thomas Sorensen. Aliishia kufunga mabao matatu tu katika mechi 39 ndiyo maana baada ya msimu mmoja tu alipigwa bei kwenda Celtic.


Shaun Wright-Phillips

 

Kocha Mourinho angeweza kutumia vyema zaidi fedha kiasi cha pauni milioni 21 alipoamua kwenda Manchester City kumsajili winga Shaun Wright-Phillips.

Kuna hoja kwamba hakuwahi kupata fursa ya kweli kwa timu hiyo japokuwa ufungaji wa mabao 10 katika mechi 124 unaweka wazi hali yake. Ni mchezaji aliyekuwa na kipaji cha aina yake ambaye hata hivyo hakutokea kuwa sehemu muhimu ya kikosi cha ushindi.


 

Juan Sebastian Veron

Raia huyu wa Argentina aliyekuwa na kipaji kikubwa aliendana na matumizi ya kutisha yaliyokuja zama za Abramovich. Ajabu ni kwamba Chelsea waliamua kumwaga pauni milioni 15 kwa mchezaji ambaye tayari alishaonekana garasa akiwa na Manchester United kiwango chake kiliposhuka.

Alicheza mechi 15 tu na Chelsea kabla ya kuanza msururu wa kutolewa kwa mkopo na kuingia kwenye vitabu vya historia kama moja ya majina makubwa zaidi yaliyoanguka.


 

Winston Bogarde

Mdachi huyu aliingia akiwa mchezaji huru lakini akaishia kuwa moja ya wachezaji hovyo zaidi kupata kusajiliwa katika historia ya Ligi Kuu.

Bogarde alishindwa kutamba klabuni hapo kwa sababu mpira ulimkataa au aliukataa mpira licha ya kwamba alikuwa akilipwa kiasi kikubwa cha mshahara kwa wiki – wakati ule mwaka 2000 ikiwa ni pauni 40,000 kwa wiki.

Chelsea walijaribu kumwondosha lakini akakataa kufuta mkataba wake hadi umalizike na alikuwa akienda mazoezini akitoka Amsterdam, maana hata mechi hakuwa akipangwa tena, alikuwa akila mshahara tu. 

 


 

Adrian Mutu

Unamkumbuka Adrian Mutu? Huyu alihusika kwenye moja ya pilika za ajabu zaidi za usajili katika historia ya Chelsea. Alisajiliwa kwa pauni milioni 15.8 lakini akafunga mabao sita tu ligi kuu.

Walau Chelsea walipata sababu ya kuachana naye, pale alipokutwa ametumia dawa za kulevya aina ya kokeni. Licha ya kumtimua, walifungua kesi ili kudai fidia kwamba alikuwa amekwenda kinyume na mkataba kwa kushindwa kuwatumikia kutokana na kutumia mihadarati.



 

Gael Kakuta

Jina hili hutajwa karibu kila wakati orodha ya magarasa yaliyotokana na wachezaji kutoka akademia ya Chelsea inapotolewa. Akiwa na umri mdogo alitoka Lens ya Ufaransa hadi London 2007 na aliwasababishia Chelsea matatizo, kwani walifungiwa kusajili, kisha marufuku hiyo ikaondolewa lakini akaishia kucheza mechi sita tu za ligi.

Huyu aliathiriwa pia na mfumo wa Chelsea wa kuingiza na kuondoa makocha na alizungushwa kote Ulaya kwa mkopo kabla ya kiangazi hiki kutupwa Sevilla.

Hata hivyo, si haki kwake kuwekwa kwenye kundi moja kama akina Torres na Shevchenko kwa sababu bado ana umri wa miaka 24 tu; labda atafufua soka yake siku zijazo.



 

Robert Fleck

 
 Kabla ya Torres na Shevchenko, au hata Sutton, alikuwapo mtu anayeitwa Robert Fleck. Chelsea walifungua zama mpya za Ligi Kuu ya England kwa kuvunja rekodi kwa kutoa pauni milioni 2.1 kumsajili mshambuliaji huyo wa Norwich mwaka 1992.

Ikatokea kuwa kituko, kwani Fleck alifunga mabao manne tu katika mechi 48 akiwa na Blues.




 Khalid Boulahrouz

Huyu alisajiliwa kutoka Hamburg, Ujerumani 2006 kwa pauni milioni nane mwaka 2006. Mdachi huyu alipachikwa jina la ‘mla watu’ na kabla ya kuingia hapo alikuwa bechi mahiri.

Alipendwa na kuheshimiwa; akapewa jezi maarufu namba tisa lakini baada ya mechi 13 tu ligi kuu na kuonekana hana lolote alipelekwa Sevilla kwa mkopo kabla ya kutupiwa virago moja kwa moja 2008.


No comments:

Post a Comment