Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Monday, April 15, 2013

SIMBA YATOA TAMKO LEO KUHUSU MASHABIKI WA YANGA KUWASHANGILIA JANA


Adobe Systems SIMBA SPORTS CLUB 
P.O.BOX 15318 | TEL+255 222183330 |FAX +255 222183330 |MSIMBAZI/MCHIKICHI STREET | DAR ES SALAAM | TANZANIA | EMAIL   simbasportsclub@yahoo.com|WEBSITE www.simba.co.tz| AFFILIATED TO TFF, DRFA and IDFA
                                                                                                                   15/04/2013
                          TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KLABU ya Simba inapenda kutoa taarifa zifuatazo kwa vyombo vya habari siku ya leo, Jumatatu, Aprili 15, 2013.
KUHUSU TIMU
MARA baada ya mechi ya jana dhidi ya Azam FC, wachezaji wote wa Simba walipewa mapumziko ya siku mbili (leo na kesho) na timu itaanza tena mazoezi keshokutwa Jumatano asubuhi katika viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Wachezaji wamepewa mapumziko hayo kutokana na kutumika kwa kipindi kirefu mfululizo tangu timu ilipokwenda katika mikoa ya kanda ya ziwa na kambini Bamba Beach jijini Dar es Salaam.
Ni matarajio ya uongozi na benchi la ufundi kwamba wachezaji hao wataanza mazoezi wakiwa na nguvu mpya na tayari kwa changamoto ya mechi nne zilizobaki kumalizia Ligi Kuu ya Tanzania.
Uongozi wa Simba unawaomba wapenzi na wanachama wake kuendelea kuisapoti timu yao kwa namna ileile waliyoionyesha katika mikoa ya kanda ya ziwa na dhidi ya Azam jana. Ingawa uwezekano wa kutwaa ubingwa haupo wala kutwaa nafasi ya pili, lakini bado kuna kazi ya kutetea heshima na hadhi ya Simba ili iweze kumaliza katika nafasi nzuri.
Wachezaji na viongozi hawataweza kufanya lolote pasipo umoja na mshikamano wa wapenzi na wanachama wake. Kama kauli mbiu ya Simba isemavyo, “NGUVU MOJA.”
MECHI YA AZAM
PAMOJA na kukubaliana na matokeo ya mechi ya jana dhidi ya Azam, uongozi wa Simba unapenda kuweka rekodi wazi kwamba haukuridhishwa na uchezeshaji wa mwamuzi, Oden Mbaga, hasahasa katika kipindi cha pili.
Kwa bahati nzuri, msimamo huu wa Simba hauna hata chembe ya ushabiki kwa vile hata washabiki waliokuwa katika upande wa watani wetu wa jadi, nao pia walionekana kutofurahishwa na uchezeshaji wa Mbaga.
Mbaga ni mwamuzi mwenye beji ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) na katika hali ya kawaida ilitazamiwa mechi ingechezeshwa kwa viwango vya kimataifa lakini hali ilikuwa kinyume chake.
Simba inaamini kwamba Mbaga hakuutendea haki mchezo ule wa jana. Simba inasema hivi kwa sababu inataka mwamuzi huyo ajirekebishe na kwamba matokeo ya mechi viwanjani yaamuliwe na ubora wa timu na si maamuzi yenye utata.
UJUMBE MFUPI WA MANENO KWENYE SIMU (SMS)
KUNA ujumbe mfupi wa maneno umeenezwa kwenye baadhi ya simu za mkononi za wapenzi wa Simba zikidai kwamba washabiki wa Yanga waliokuwa wakiishangilia klabu yetu jana walifanya hivyo kwa sababu klabu hizi mbili zimeingia katika mahusiano.
Ujumbe huo ukadai kwamba lengo la mahusiano hayo mapya baina ya Simba na Yanga ni kuhakikisha kwamba Simba inafungwa kwa idadi kubwa ya mabao kwenye mechi ya watani wa jadi Mei 18 mwaka huu.
Ujumbe huo, ukaenda mbali zaidi kwa kudai kwamba hata kambi ya Simba ya Bamba Beach imefadhiliwa na Yanga.
Ujumbe huo wa simu ni wa kuchekesha. Na unachekesha sana. Yeyote aliyetunga meseji hii ana nia ya kuleta machafuko ndani ya klabu ya Simba. Inaonekana haridhishwi na hali ya amani iliyopo klabuni kwa sasa.
Uongozi wa Simba unakana kuwepo kwa mahusiano yoyote ya kuhujumu timu baina ya viongozi wa klabu na Yanga. Kitendo cha kushangiliwa kwa timu pinzani si kigeni kwani kimewahi pia kutokea katika nchi kadhaa duniani.
Ikumbukwe kwamba kimsingi, si jinai au mwiko kwa shabiki wa Yanga kuishangilia Simba. Kama washabiki wa wapinzani wetu wa jadi walivutiwa na kiwango chetu na kuamua kutushangilia, hiyo haikuwa dhambi.
Uongozi unapenda kuwaomba wanachama wa Simba kuwa na imani na uongozi wao na kufahamu kwamba unafanya kila unaloweza kulinda na kuhifadhi hadhi na heshima ya klabu.
Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC

No comments:

Post a Comment