Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, June 1, 2017

BERNARDO SILVA MASHINE MPYA MAN CITY


Image result for BERNARDO SILVA
NDEGE yake ilitua muda mfupi tu baada ya kumalizika kwa mechi za Ligi Kuu ya England (ECL), lengo likiwa kupimwa na kukubali maslahi binafsi na Manchester City ili msimu ujao akipige Etihad.
Si yeye wala kocha Pep Guardiola waliopenda kupoteza muda juu ya jambo hilo, wote wakionekana kuwa makini na kutaka wamalizane mapema ili lisitokee jingine na kuvuruga mipango – kila mmoja akionekana kuwa na hamu.
Wakati Guardiola amechukua hatua ya haraka kwenye kuanza usajili, mchezaji mwenyewe, Bernardo Mota Veiga de Carvalho Silva kutoka Ureno alitaka ahakikishe kwamba ima faima anajiunga na matajiri hao wa Manchester akitoka Monaco, Ufaransa.
Jina lililozoeleka zaidi ni Bernardo Silva na si kwamba yanatumika yote kwenye mlolongo huo hapo juu, akiwa ni Mreno aliyezaliwa Agosti 10, 1994 na amekuwa akifurahia Ligue 1 – Ligi Kuu ya Ufaransa na Timu ya Taifa ya Ureno akicheza eneo la kiungo.
Na leo ndiyo siku rasmi ambayo atachukuliwa kwamba ameanza mkataba wake, kwani ndipo Chama cha Soka (FA) kimefungua rasmi dirisha hili kubwa la usajili la msimu wa kiangazi, litakaloona mbwembwe kwa wenye fedha na kukimbilia makombo kwa wasio na kisu kikali.
Naam, Man City wameachana na pauni milioni 43.5 kwa ajili ya kifaa hiki katika ada ya uhamisho. Silva atakayeungana na Silva (David) mwingine hapo Etihad, hajaanza kusikika leo kwani alikuwa kwenye kikosi cha U-19 cha Timu ya Taifa ya Ureno kwenye michuano ya Uefa 2013.
Ni yeye aliyetia mchango sana wakasonga hadi nusu fainali na haikushangaza pale alipotajwa kuwa moja kati ya watu 10 wenye umri mdogo wenye kipaji kikubwa katika Ulaya kwenye soka.
Hakuchaguliwa na marafiki zake, bali wana habari kutoka nchi mbalimbali za Ulaya, kama England, Ufaransa, Italia, Ujerumani, Hispania na kwingineko, ikiwamo Ureno.
Alianza kuchezea kikosi ha wakubwa cha Ureno Machi 31, 2015 walipokipiga dhidi ya Cape Verde katika mechi ya kirafiki na mguu wake ulihusika kwenye moja ya mabao matano waliyoshinda dhidi ya Ujerumani (U-21) kwenye Uefa.
Watu wanajua kutoa majina – na hutofautiana baina ya mtu mmoja na mwingine, ambapo kinda huyu wa Man U anayekwenda kukutana na akina Gabriel Jesus, anaitwa bazooka, yaani kwamba ni aina ya mchezaji anayweza kujitanua anavyopenda uwanjani, akiwapelekesha wachezaji wa timu pinzani.
Ni mtu aliyekuwa akiishi kwenye nyumba iliyobana sana kwenye maflati hapo jijini Monaco, ambapo alianza maisha akiwa na hali ya chini, akiosha vyombo hotelini kujipatia chochote cha kupeleka kinywani.
Anaelezwa na walimu wake kwamba ni mchezaji mwenye ufundi mkubwa na maono ya kimichezo anapokuwa uwanjani, akicheza kana kwamba mpira umeshikiliwa kwa gundi mguuni pake, ambapo kuupoteza ni ngumu sana.
Asifikiri kwamba yaliyokuwa Monaco ndiyo yapo humu kwenye EPL, maana kule kwanza kuna uwezekano mkubwa wa kutolipa kodi, lakini pia mtindo wa maisha ni wa kujirusha sana, kukiwamo macasino mengi na utajiri wa aina hyake.
Hata hivyo, yote niliyotaja hapo juu hayamhusu yeye moja kwa moja, bali alikuwa akiona kwa wengine huko Monaco. Hajiingizi kwenye hayo, bali alitumia fedha zake kwa uangalifu, akiwa na chumba kilichobana sana cha kulala na jiko dogo.
Hakuwa amenunua hata mashine ya kuosha vyombo, hivyo alikuwa akiosha mwenyewe kwa mikono yake na vivyo hivyo kwa kufua nguo zake na kuzianika kwenye balkoni kwa ajili ya kuzikausha.
Ni kweli alikokaa aliangaliana na bahari, mandhari nzuri isipokuwa kwa udogo wa eneo lake si hivyo. Kwa pauni 30,000 kwa wiki alizokuwa akilipwa hapo Monaco, angeweza kuzitumia kuchukua nyumba kubwa tu kwenye viunga vya jiji.
Manchester kule hataiona bahari tofauti na Monaco na haijaeleweka atatafuta nyumba ya aina gani, kwa sababu moja ya sifa zake ni mtu asiyetaka kutumia kiasi kikubwa cha fedha kwa mambo yake mwenyewe. Hajichori tatuu wala kununua saa au magari ya kifahari.
Akiwa na umri wa miaka 22 amejijengea nidhamu fulani anayotaka ahakikishe kuishikilia na anaondoka wakati Monaco waliokosa ubingwa mara kadhaa wakiuchukua kwa kuwashinda mahasimu wao – Paris Saint-Germain (PSG).
Wanamsema kuwa ni aina ya mtu anayeona vitu kabla ya wengine wote – kutafuta vyumba, kupokea mpira, kugawa pasi, kukimbia na  mpira na kisha kutafuta eneo zuri kwa ajili ya kupokea tena mpira na kufungwa – utampenda. Si rahisi kumwona uwanjani eti akiwa amekaa; muda wote anasongea na kukimbia.
“Mnamzungumzia Bernardo Silva? Achana na hilo jina, mwito bazooka, anasambaa kwa kujitanua lakini pia anaushikilia mpira mguuni pake kana kwamba kuna gundi. Ningeweza kulipa fedha kwa ajili ya kumtazama akicheza nakuambia,” anasema Benjamin Mendy, beki wa kushoto wa Monaco baada ya timu yao kutwaa ubingwa kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 17.
Mchezaji mwenzake mwingine (wa zamani sasa), Jemerson, ambaye ni beki wa kati, anasema Silva ana uchawi wa aina yake na kwamba ni kama vile ametoka sayari nyingine. Anasema hufanya vitu visivyo vya kawaida kwenye mazoezi sana na kwenye mechi. Anamalizia kwa kicheko, na anapoulizwa kulikoni, anasema ni kutokana na jinsi masikio ya Silva yalivyo kiajabu.

No comments:

Post a Comment