PSSSF YAWATAKA WAANDISHI WA HABARI KUWAELIMISHA WANACHAMA UMUHIMU WA KUHAKIKI MICHANGO, MAFAO KIDIJITALI
Na Neema Nkumbi -
Shinyanga
Hatua hiyo
imeelezwa kulenga kuhakikisha taarifa zao zinakuwa sahihi na kupunguza
changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa kudai mafao.
Wito huo umetolewa
leo, Septemba 18, 2026, mjini Shinyanga wakati wa semina ya PSSSF kwa waandishi
wa habari kutoka Mtandao wa Wanablogu Tanzania (Tanzania Bloggers Network –
TBN) na Klabu za Waandishi wa Habari za mikoa ya Shinyanga na Simiyu.
Katika semina
hiyo, Msimamizi PSSSF Mkoa wa Simiyu
Salum Miraji ameeleza kuwa matumizi ya mifumo ya kidijitali yamekuwa sehemu ya
maboresho ya huduma za mfuko, yakilenga kumwezesha mwanachama kupata na
kuhakiki taarifa zake bila kulazimika kufika katika ofisi za PSSSF.
Ameeleza kuwa
mwanachama anaweza kutumia mfumo huo kufuatilia taarifa zake, ikiwemo taarifa
za michango, na kubaini mapema endapo kuna taarifa zisizo sahihi ambazo
zinaweza kuleta changamoto wakati wa uchakataji wa mafao.
PSSSF imewataka
waandishi wa habari kutumia majukwaa yao kuwaelimisha wanachama kuhusu umuhimu
wa kufanya uhakiki huo mapema, badala ya kusubiri hadi wanapofikia hatua ya
kustaafu au kuhitaji mafao.
Katika semina
hiyo, Mratibu wa Tanzania Bloggers Network – TBN Kanda ya Ziwa, Kadama Malunde,
amesisitiza umuhimu wa waandishi kutumia nafasi yao na taaluma waliyonayo
kuwafikishia wananchi elimu na taarifa sahihi zinazoweza kuwasaidia kutambua
haki na huduma wanazostahili.
Akizungumza kwa
niaba ya Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, Malunde amesema waandishi wana nafasi
muhimu katika kuhakikisha wananchi wanaelewa masuala ya hifadhi ya jamii,
ikiwemo umuhimu wa wanachama kufuatilia taarifa zao za michango na mafao kwa
kutumia mifumo inayotolewa na taasisi husika.
Amesema mafunzo
wanayopata waandishi yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza uelewa wao na baadaye
kutumia ujuzi huo kuwaelimisha wananchi kwa lugha rahisi, sahihi na
inayoeleweka.
“Leo tunapaswa
kuwa na furaha ya kupata elimu. Kwa mwandishi wa habari, kujifunza ni sehemu ya
kazi yetu. Dunia inabadilika, teknolojia inabadilika na mahitaji ya jamii
yanabadilika,” amesema Malunde.
Malunde amesema
TBN, iliyoanzishwa mwaka 2015, imeendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali,
ikiwemo PSSSF, katika mafunzo na ujenzi wa uwezo wa wanablogu na watengeneza
maudhui nchini.
Amesema maendeleo
ya teknolojia yameongeza kasi ya usambazaji wa taarifa, hivyo waandishi
wanapaswa kuwa makini kuhakikisha taarifa wanazozifikisha kwa jamii
zinathibitishwa, zina usahihi na zinazingatia misingi ya uwajibikaji wa
taaluma.
“Taarifa za
kidijitali zinaweza kuwafikia watu wengi kwa muda mfupi. Hivyo, nidhamu,
usahihi na uwajibikaji ni muhimu sana. Uwezo wetu na nidhamu yetu ndiyo misingi
inayoweza kutufanya kuwa waandishi bora na wenye mchango mkubwa kwa jamii,”
amesema.
Aidha, Malunde
amesema historia ya TBN inaonesha umuhimu wa kujifunza, kushirikiana na kujenga
uwezo miongoni mwa waandishi na watengeneza maudhui ili kuongeza mchango wao
katika jamii.
“Tanzania ina
waandishi wenye uwezo mkubwa, na tunapaswa kuendelea kuutumia uwezo huo kwa
manufaa ya jamii. Tuyatumie mafunzo haya kupata uelewa zaidi na kisha
kuwafikishia wananchi taarifa kwa lugha rahisi na inayoeleweka,” amesema.
Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari ana wajibu wa kuthibitisha taarifa kabla ya kuzichapisha au kuzitangaza, kuheshimu vyanzo vya habari na kuwajibika kwa maudhui anayoyafikisha kwa umma.
“Mwandishi wa
habari anatakiwa kuthibitisha taarifa, kuheshimu vyanzo vya habari na
kuwajibika kwa kila anachochapisha au kukitangaza,” ameongeza.
Naye Kaimu Afisa
Mfawidhi PSSSF Shinyanga Sunday Rashid amesema mfuko huo umeendelea kuboresha
mchakato wa maandalizi ya mafao kwa kuanza kushughulikia taarifa za mtumishi
anayekaribia kustaafu miezi sita kabla ya tarehe yake rasmi ya kustaafu.
Hatua hiyo
inalenga kutoa muda wa kutosha wa kuhakiki taarifa za mwanachama na
kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza kabla ya kufikia muda wa
kustaafu.
Semina hiyo
imelenga kuwajengea waandishi uelewa kuhusu huduma za PSSSF ili waweze kutumia
taaluma yao kuelimisha jamii, hususan wanachama, kuhusu haki, wajibu na namna
ya kufuatilia taarifa zao za hifadhi ya jamii.
Post a Comment