PSSSF YATAKA WASTAAFU KUTUMIA MIFUMO KUEPUKA MATAPELI
Na Marco Maduhu,
SHINYANGA
WASTAAFU nchini
wametakiwa kuwa makini na watu wanaojitambulisha kama mawakala wa Mfuko wa
Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), wakihimizwa kutumia njia rasmi za mifumo
ya kidijiti ya mfuko huo kuhakiki taarifa zao na kufuatilia mafao yao.
Tahadhari hiyo
imetolewa leo, Septemba 18, 2026, na Afisa Msimamizi wa PSSSF Mkoa wa Simiyu,
Salum Mwegelo, wakati wa semina ya PSSSF kwa waandishi wa habari wa Mtandao wa
Wanablogu Tanzania (Tanzania Bloggers Network – TBN) na Klabu za Waandishi wa
Habari za Shinyanga na Simiyu.
Mwegelo amesema
baadhi ya wastaafu wamekuwa katika hatari ya kutapeliwa kutokana na kutumia
watu wasio rasmi wanaodai kuwa wanaweza kuwasaidia katika taratibu za kuhakiki
taarifa, kufuatilia au kupata mafao yao.
Amesema watu hao
wanaweza kuomba taarifa nyeti za wastaafu, ikiwemo namba za siri za akaunti za
fedha na taarifa nyingine binafsi, ambazo zinaweza kutumiwa kufanya miamala
bila ridhaa ya wahusika.
Mwegelo
amesisitiza kuwa PSSSF haina mawakala wanaotoa huduma kwa niaba ya mfuko huo,
hivyo wastaafu wanapaswa kuwa na tahadhari dhidi ya mtu yeyote
anayejitambulisha kama wakala wa PSSSF na kuwaomba taarifa zao za siri.
Amesema wastaafu wanapaswa kutumia njia rasmi zinazotolewa na PSSSF, ikiwemo kufika katika ofisi za mfuko huo au kutumia mifumo ya kidijitali inayowawezesha wanachama na wastaafu kufuatilia na kuhakiki taarifa zao kwa usalama.
Amesema matumizi
ya mifumo ya kidijitali ni miongoni mwa njia zinazoweza kuwasaidia wanachama kupata
taarifa zao kwa urahisi bila kulazimika kuwapa watu wengine taarifa zao binafsi
au za kifedha.
Kwa upande wake,
Afisa Uhusiano wa PSSSF, Abdul Njaidi amewataka waandishi wa habari na
wanablogu kutumia taaluma yao kuwafikishia wananchi taarifa sahihi kuhusu
huduma za mfuko huo, hususan elimu inayohusu haki, wajibu na taratibu za kupata
mafao.
Njaidi amesema
vyombo vya habari, blogu na majukwaa ya kidijitali vina nafasi kubwa katika
kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wanachama na wastaafu kwa lugha rahisi na
inayoeleweka, huku akiwataka waandishi na wanablogu kuthibitisha taarifa kabla
ya kuzifikisha kwa umma.
Amesema elimu
sahihi inaweza kusaidia kuwawezesha wanachama na wastaafu kutambua njia halali
za kupata huduma za PSSSF na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wanaoweza kutumia
mwanya wa ukosefu wa taarifa kuwahadaa.
Mratibu wa
Tanzania Bloggers Network (TBN) Kanda ya Ziwa, Kadama Malunde, amepongeza PSSSF
kwa kuandaa semina hiyo, akisema mafunzo kama hayo ni muhimu kwa waandishi wa
habari na wanablogu kwa kuwa yanawaongezea uelewa wa masuala wanayopaswa
kuyafikisha kwa jamii.
Malunde amesema
waandishi na wanablogu wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha kila taarifa
wanayoitoa kwa umma inathibitishwa, ina usahihi na inatoka katika vyanzo
vinavyoaminika, hususan katika kipindi hiki ambacho taarifa za kidijitali
zinaweza kusambaa kwa kasi kubwa.
“Semina kama hii
ni muhimu kwa sababu inatupa nafasi ya kujifunza na kuongeza uelewa. Tukiwa waandishi
na wanablogu, jukumu letu si kuchapisha taarifa tu, bali kuhakikisha taarifa
tunazowafikishia wananchi ni sahihi, zimehakikiwa na zina manufaa kwa jamii,”
amesema Malunde.
Naye Mwenyekiti wa
Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Greyson Kakuru, amesema semina
hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa
imewapa uelewa zaidi kuhusu huduma za PSSSF na masuala yanayowahusu wanachama
na wastaafu.
Kakuru amesema
maarifa yaliyopatikana yatawasaidia waandishi na wanablogu kuandaa na kusambaza
habari zenye usahihi, huku wakitoa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kutumia
huduma za PSSSF na kujilinda dhidi ya utapeli.
Post a Comment