Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, March 8, 2018

23 WAITWA TAIFA STARS KUIVAA ALGERIA NA DR CONGO



KIKOSI cha wachezaji 23 wa timu ya Taifa ya soka ‘Taifa Stars’ ambao watacheza michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa ya kalenda ya FIFA kimetajwa jana na kocha msaidizi wa timu hiyo Hemedi Morocco.
Akizungumza leo Morocco alisema Taifa Stars inatarajia kuingia kambini Machi 18 na itaondoka kesho yake Machi 19 kwenda Algeria kucheza mechi Machi 22 na kitarudi Tanzania Machi 24.
Baada ya kurudi nchini kitaingia kambini kujiandaa na mchezo dhidi ya DR Congo utakaochezwa Uwanja wa Taifa, Machi 27.
“Mwezi huu Taifa Stars itacheza michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa ya kalenda ya FIFA hivyo tunatarajia kufanya vizuri ili tujiweke vizuri katika viwango vya kimataifa vinavyotolewa na FIFA kila mwezi,” alisema Morocco
Pia Morocco alisema kumwita Thomas Ulimwengu wameangalia vitu vingi japo alikiri kutokuwa vizuri kwa mchezo ila watamwangalia katika mazoezi ya Taifa stars kwani daktariwake amesema amepona na amecheza michezo miwili ya kirafiki.
Wachezaji waliotwa ni makipa Aishi Manula, Ramadhan Kabwili na Abdurahman Mohamed, walinzi wapembeni ni Shomari Kapombe, Hassan Kessy na Gadiel Michael.
Walinzi wa kati ni Kelvin Yondani, Abdi Banda, Erasto Nyoni, viungo wa kati ni Hamis Abdallah, Mudathir Yahaya, Said Ndemla, Faisal Salum na Abdulazizi Makame.
Viungo wa pembeni ni Farid Mussa, Thomas Ulimwengu, Ibrahim Ajib, Shiza Kichuya na Mohamed Issa na washambuliaji ni Mbwana Samatta, Simon Msuva, John Bocco na Zayd Yahaya.
Wakati huo huo kocha wa timu ya Taifa ya vijana waliochini ya miaka 20 (U-20) Oscar Mirambo amesema timu hiyo imanza mazoezi kwa ajili ya maandalizi ya mchezo  wa AFCON dhidi ya Congo utakaochezwa Machi 31.
“Baada ya mchezo wa kwanza tutarudiana  Aprili 21 na endapo tutafuzu tutacheza na Mali mwezi Mei na baada ya hapo endapo tutaitoa Mali tutakutana na mshindi kati ya Cameroon na Uganda ,” alisema Mirambo
Pia Mirambo alisema wachezaji 43 wapo kambini na watawachuja na kubaki 23 ambao watachezaji mashindano hayo na kikosi hicho kinaundwa na wachezaji wa iliyokuwa Serengeti boys iliyoshiriki fainali za Gabon na wengine kutoka katika vikosi mbalimbali vya timu B.

No comments:

Post a Comment