Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, March 8, 2018

MVUA ILIVYOONDOA LADHA YA MCHEZO WA SIMBA DHIDI YA AL MASRY






MVUA kubwa  iliyonyesha jana jioni ikiambatana na upepo mkali ilisababisha kukatika kwa umeme kwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam na kufanya mechi ya Simba na Al Masry ya Misri kusimama kwa takriban dakika 30. 
Mechi hiyo ya kombe la Shirikisho Afrika ilisimama zikiwa zimesalia dakika 12 kumalizika, huku timu hizo zikiwa sare ya kufungana mabao 2-2. Hata hivyo baada ya mvua kukatika na umeme kurudi uwanjani hapo, waamuzi waliamuru mechi iendelee kwa dakika ilizosimama ambapo ilimalizika kwa matokeo hayohayo ya 2-2. 
Hii si mara ya kwanza kwa Simba yenye historia ya kutofungwa na timu za waarabu nyumbani kukutana na dhahama ya mvua na mechi kuahirishwa ama kusimama. Mwaka 2001 kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa, ilikutana na dhahama hiyo kwenye uwanja wa Uhuru (Zamani taifa) ambapo mechi yake dhidi ya Ismaili ya Misri iliahirishwa kutokana na mvua kubwa ambapo mpaka mapumziko Simba ilikuwa mbele kwa mabao 2-0 yaliyofungwa na Joseph Kaniki na Shekhan Rashid. 
Kwa mujibu wa kanuni za Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wakati huo, mechi ikiahirishwa inarudiwa yote baada ya saa 48, hivyo mechi hiyo ilirudiwa baada ya siku mbili ambapo Simba ilishinda bao 1-0 lililofungwa na Kaniki, lakini iliondolewa kwenye michuano maana katika mechi ya kwanza iliyochezwa Misri Ismaili ilishinda mabao 2-0. 
Kwa matokeo hayo ya jana, Simba inahitaji kupata ushindi wa aina yoyote ugenini wiki ijayo, au itoke sare ya zaidi ya mabao mawili. Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao la kuongoza katika dakika ya nane likifungwa na nahodha wake John Bocco kwa mkwaju wa penalti iliyotolewa na mwamuzi baada ya mchezaji wa Al Masry Mohammed Koffi kunawa mpira eneo la hatari.
Bao hilo lilidumu kwa dakika mbili tu kabla ya Masry  kusawazisha kupitia kwa Ahmed Gomaa akiunganisha krosi ya Mohamed Ahmed. Al Masry walipata bao la pili katika dakika ya 26 kwa mkwaju wa penalti iliyotolewa na mwamuzi baada ya James Kotei kunawa mpira kwenye eneo la hatari. Penalti hiyo ilikwamishwa wavuni na Ahmed Abdalraof.
Katika kipindi chote cha kwanza Simba ilionekana kuzidiwa na wageni walifanya mashambulizi langoni kwao mara kwa mara. Simba, ilikwenda mapumziko ikiwa nyuma kwa mabao 2-1 jambo lililofanya benchi lake la ufundi kufanya mabadiliko dakika chache baada ya kuanza
kwa kipindi cha pili ambapo alitoka Bocco na nafasi yake kuchukuliwa na Laudit Mavugo. Awali, kabla ya kutoka Bocco, benchi la ufundi liliamua atoke Shizza Kichuya, lakini mchezaji huyo pamoja na wenzie waliokuwa uwanjani waligoma na kushauri asitoke ndipo ilipoamuliwa
atoke Bocco. Mabadiliko hayo yalirudisha uhai kwa Simba ambapo sasa walipeleka mashambulizi mfululizo langoni mwa Al Masry ambapo Kichuya na Okwi walikosa mabao kwa nyakati tofauti kwa kupiga mipira ya juu wakiwa kwenye nafasi nzuri ya kufunga.
Emmanuel Okwi aliisawazishia Simba bao la pili kwa mkwaju wa penalti iliyotolewa na mwamuzi baada ya Koffi wa Masry kushika mpira eneo la hatari. Dakika chache baada ya bao hilo ndipo mvua kubwa iliponyesha na kusababisha umeme kukatika hali iliyozua mtafaruku.

No comments:

Post a Comment