Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Sunday, March 3, 2013

ASHANTI YA ILALA A.K.A WATOTO WA JIJI WARUDI RASMI LIGI KUU TANZANIA BARA

Beki wa Ashanti (mwenye jezi nyekundu ) akiondoa mpira kwenye himaya ya mshambuliaji wa Villa Squad kwenye mchezo wa lligi daraja la kwanza uliochezwa uwanja wa Karume jijini Dar es salaam

TIMU ya Ashanti United imekata tiketi ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 na Villa Squad kwenye mchezo wa Ligi daraja la kwanza uliochezwa uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam juzi.

Kwa matokeo hayo Ashanti imefikisha pointi 28 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote kwenye kundi B hata wakifungwa michezo miwili iliyosalia huku Villa wao wakiwa na pointi 20 na michezo miwili pia.

Mchezo huo ulikuwa na ushindani mkubwa na uliojaa ufundi huku mashabiki wa timu zote wakichangia kasi ya uchezaji kutokana na kushangilia kuanzia dakika ya kwanza hadi ya 90.

Ashanti walijipatia bao dakika ya tisa kupitia kwa Zablon Raymond wa Villa ambaye alijifunga wakati akiokoa shuti la Maliki Jaffary kwa kichwa na kutinga wavuni, Villa walisawazisha bao kupitia kwa Ali Mrisho baada ya kuwazidi mbio mabeki wa Ashanti na kufanya timu ziende  mapumziko zikiwa sare ya bao 1-1.

Kipindi cha Pili kwa timu zote kuendelea kushambulia na kufanya mabadiliko na dakika  ya 54  mshambuliaji Fakii Rashid wa Ashanti aliwanyanyua mashabiki baada ya kuwapiga chenga mabeki wa Villa na kubaki na golikipa na kufunga bao kirahisi lakini Villa nao walizidisha mashambulizi na dakika ya 65 walisawazisha bao kupitia kwa Amri Mwideni baada ya kutokea piga nikupige langoni kwa Ashanti.

Kwa matokeo hayo ambayo yamepokelewa kwa furaha na mashabiki na viongozi, Ashanti imeungana na Mbeya City ambayo ipo kundi A kukata tiketi ya kucheza ligi kuu msimu ujao na kuliacha kundi C ambalo ni gumu wakiwania nafasi moja ambapo timu za Rhino, JKT Kanembwa na Pamba  mojawapo anaweza kuichukua endapo yeyote atafanya vibaya.

Mchezo mwingine kwenye kundi B umechezwa kwenye uwanja wa Mabatini, Pwani na Polisi Dar es Salaam wakaifunga Green Warriors mabao 2-1.

Kundi C ilichezwa michezo minne, mkoani Mara maafande wa Polisi Mara waliifunga Polisi Dodoma bao 1-0  mchezo uliochezwa uwanja wa Karume, uwanja wa Kambarage Shinyanga Rhino Rangers ya Tabora waliondoka na pointi tatu baada ya kuifunga Mwadui bao 1-0.

Kwenye uwanja wa Lake Tanganyika wenyeji JKT Kanembwa waliifunga Polisi Tabora mabao 2-0 na mjini Kiteto Manyara, Pamba na Morani walitoka sare ya 0-0

Kundi A, Kurugenzi ya Makambako iliutumia vema uwanja wa nyumbani na kuweza kuwafunga vinara wa kundi hilo ambayo imekwisha kukata tiketi ya kucheza ligi kuu msimu ujao,  Mbeya City bao 1-0 .
 
                                  

No comments:

Post a Comment