Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Saturday, September 10, 2016

YANGA YAIFIKISHA POINTI SABA BAADA YA KUIFUNGA MAJIMAJI 3-0





YANGA imerejesha furaha kwa mashabiki wake baada ya leo kushinda mabao 3-0 dhidi ya Majimaji katika mechi ya Ligi Kuu iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam.

Mabingwa hao watetezi wa ligi hiyo wamepata ushindi  baada ya kutoka sare ya bila kufungana katika mechi dhidi ya Ndanda iliyochezwa Mtwara, Jumatano ya wiki hii.

Yanga ilipata bao la kuongoza katika dakika ya 20, likifungwa na Deus Kaseke aliyeuwahi mpira wa penalti iliyopigwa na Simon Msuva.

Awali, mwamuzi wa mechi hiyo Emmanuel Mwandebwa wa Arusha alitoa penalti kwa Yanga baada ya mchezaji wa Majimaji kushika mpira eneo la hatari na ndipo Msuva alipopiga penalti mara ya kwanza, lakini mwamuzi alimtaka kurudia tena akidai alikosea, akaipiga mara ya pili ikaamuliwa kurudia tena, akapiga mara ya tatu mpira ukagonga mwamba na ndipo Kaseke alipouwahi na kuujaza wavuni.

Kipindi cha kwanza kiliisha kwa Yanga kuongoza kwa bao 1-0. Katika kipindi hicho, Yanga walitengeneza nafasi nyingi lakini walishindwa kuzitumia huku Majimaji wakicheza kwa kuzuia zaidi.

Amisi Tambwe aliifungia Yanga bao la pili dakika ya 81 kwa kichwa, ikiwa ni baada ya kufunga katika dakika ya 74 na mwamuzi kulikataa akidai mfungaji aliotea. Dakika tano baadaye, Tambwe aliongeza bao la tatu kwa pasi ya Juma Mahadhi.

Kutoka kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya, Azam jana iliendelea kuzoa pointi kwenye uwanja huo baada ya kuifunga Mbeya City mabao 2-1.

Kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, Ndanda ilitoka sare ya bila kufungana na Kagera Sugar. Huku kwenye uwanja wa Mwadui Shinyanga, Mwadui imetoka sare ya mabao 2-2 na Stand United.

Katika uwanja wa Mabatini Mlandizi, Ruvu Shooting iliitambia JKT Ruvu kwa kuifunga bao 1-0.

Ligi hiyo inaendelea tena leo kwenye uwanja wa Uhuru ambapo Simba itaikaribisha Mtibwa Sugar ya Manungu, Turiani.

Mechi hiyo inatarajiwa kuwa kali na ya vuta nikuvute kutokana na timu hizo kutambiana kwa zamu kila zinapokutana.

Timu hizo zinakutana zikiwa na makocha wapya Joseph Omog wa Simba na Salum Mayanga wa Mtibwa na wote wakionesha kuwa wanalitaka taji kulingana na ubora wa vikosi vyao.

Mtibwa Sugar inapokutana na Simba au Yanga ni wazi kuwa hucheza kwa kukamia, lakini mwisho wa siku mmojawapo huibuka na ushindi.

Msimu uliopita timu hizi zilikutana raundi ya kwanza Januari 16, mwaka huu Simba ikaibuka na ushindi wa bao 1-0 katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, pia ilipokutana katika raundi ya pili Mei 15, mwaka huu bado Simba ilishinda bao 1-0.


No comments:

Post a Comment