Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, August 22, 2013

WAHISPAINIOLA WATANO WANAOTIKISA LIGI YA ENGLAND



LIGI Kuu England imejaa mastaa kutoka kila kona ya ulimwengu huu, lakini kwenye miaka ya karibuni, Wahispaniola wamezidi kujaa kwenye ligi hiyo.
Hakuna cha ajabu katika hili, hasa kutokana na mafanikio ya timu ya taifa ya Hispania kwenye michuano ya kimataifa kutoka mwaka 2008.

Japokuwa wachezaji bora wa Hispania wanapenda sana kuchezea klabu za Barcelona au Real Madrid, wale walioamua kuingia Ligi Kuu England wamethibitisha ubora wao kwa kutawala ligi hiyo.
Ni haki kusema kwamba, wachezaji wote wa Kihispaniola ni mafundi na wanajua wanachokifanya uwanjani.

Hata hivyo kwa sababu makala haya yanakuletea tano bora ya wachezaji wa Kihispaniola, England ndiyo maana kuna mafundi wengine wanakosekana.
Michu wa Swansea City anabahati mbaya kukosekana kwenye listi hii, baada ya msimu mzuri wa kwanza England, wakati mastaa wa Manchester City, Jesus Navas na Alvaro Negredo wanakila sababu ya kuwa mastaa pale Etihad.
Hawa ndio mafundi watano wa Kihispaniola tishio England.

5. Roberto Soldado - Tottenham
Sawa, Roberto Soldado amecheza mechi moja tu kwenye Ligi Kuu England, lakini Mhispaniola huyo ameshathibitisha kwamba ni suluhisho la matatizo ya White Hart Lane msimu huu.
Staa huyo mwenye miaka 28, tayari ameshafungua akaunti yake ya mabao ya Ligi Kuu England, na malengo yake sasa ni kufunga mabao 20 na zaidi mpaka mwisho wa msimu.
Jamaa ni mfungaji wa asili, Soldado pia ni hatari akiwa kwenye eneo la hatari anaweza kuirudisha Tottenham Hotspur kwenye nne bora msimu huu au mbali zaidi.

4. David de Gea - Manchester United
Baada ya kuanza kwa kusuasua England, David de Gea ameibukia kuwa mmoja kati ya makipa bora wa Ligi Kuu England.
De Gea (22), bado anatafuta nafasi ya kucheza mechi yake ya kwanza kwenye timu ya taifa ya wakubwa ya Hispania, lakini anaonekana ndiye atakuja kuwa mrithi wa kudumu wa Iker Casillas siku gwiji huyo wa Real Madrid akitundika gloves zake.
De Gea anakila kitu ambacho kipa wa kiwango cha juu anatakiwa kuwanacho; anajiamini, yuko fasta, anaweza kufanya maamuzi ya haraka na hapotezi umakini langoni.

3. David Silva - Manchester City
David Silva anawakilisha maana halisi ya kiungo mshambuliaji wa kileo wa Hispania; ana umbo dogo, mjanja mjanja na amebarikiwa uwanjani.
Staa huyo wa Manchester City alitua Etihad mwaka 2010, baada ya kucheza kwa mafanikio kwa miaka sita aliyokuwa na Valencia na tangu wakati huo amekuwa kipenzi cha mashabiki wa City kutokana na uwezo wake.
Silva alishinda Kombe la FA kwenye msimu wake wa kwanza England, kabla ya kubeba taji la Ligi Kuu England miezi 12 baadaye.

2. Juan Mata - Chelsea
Kiwango cha Juan Mata, Chelsea msimu uliopita kilikuwa hakina mfano wake.
Mata, 25 alifunga mabao 20 na kutengeneza mengine 35 kwenye mechi 64 za The Blues, ambao walichukua taji la Europa League.
Kuna uvumi kwamba, Jose Mourinho anataka kumuachia Mhispaniola huyo wakati huu wa usajili wa kiangazi, lakini staa huyo wa zamani wa Valencia ni hatari na atatisha popote atakapoenda.

1. Santi Cazorla - Arsenal
Kitendo cha Arsenal kumnasa Santi Cazorla (27) kutoka Malaga, Agosti mwaka jana kwa dau la chini ya pauni milioni 15, ni sawa na utapeli.
Licha ya kuhusishwa na Real Madrid, Cazorla aliamua kujifunga mkataba wa muda mrefu Emirates, habari hii ilikuwa mbaya kwa timu kama Real Madrid ambazo zilitaka kumsajili kwa hali na mali.
Kwa uwezo wake wa kutumia miguu yote hata akiwa amebanwa kunamfanya Cazorla kuwa kiungo mwenye kipaji cha pekee, alifunga mabao 12 na kutengeneza 14 kwenye msimu wake wa kwanza England na atakuwa mchezaji muhimu wa kumaliza ukame wa mataji Arsenal msimu huu.
Arsenal wanabahati sana kuwa naye, lakini watarajie klabu kubwa kuja kumsaka kama ukame utaendelea Emirates.

No comments:

Post a Comment