Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Thursday, August 22, 2013

MATANA ROONEY NI BIASHARA KICHAA YA MOURIHNO NA MOYES




RIPOTI zinasema kwamba, Manchester United sasa wako tayari kuzungumza na Chelsea juu ya mustakabali wa Wayne Rooney, baada ya David Moyes kukataa ofa mbili za Jose Mourinho za kwanza.
 
Lakini ripoti hiyo inadai kwamba, Man United watakuwa tayari kumuuza Rooney ikiwa tu, Mourinho atakubali kumjumuisha kiungo wa Kihispaniola Juan Mata kwenye ofa yake.
Mourinho mwenyewe ameshaweza wazi kwamba, atamfukuzia Rooney mpaka siku ya mwisho ya dirisha la usajili, lakini akasisitiza kwamba akimkosa anaplan B na C, huku akigoma kuwataja wachezaji ambao atawachukua kama akishindwa kumnasa Rooney.

Wachambuzi na mashabiki wa soka wamekuwa na mitazamo tofauti kuhusu mchakato wa kumuhusisha Mata kwenye dili la kumnasa Rooney kuna wanaoona Mourinho anachemsha.
Ili kujua nani analamba dume na nani anachemsha kwenye dili hili, makala haya yanaangalia takwimu muhimu za kila mchezaji msimu uliopita.

Mata alishinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Chelsea wa mwaka, msimu uliopita, kutokana na kuwa na msimu mzuri sana, akifunga mabao muhimu na kusaidia kupatikana kwa mengine mengi.
Mhispaniola huyo alifunga jumla ya mabao 12 kwenye mechi 35 za Ligi Kuu England. Huku akifunga mengine nane kwenye michuano mingine, hivyo alimaliza msimu na mabao 20 kwenye michuano yote.

Rooney naye alifunga mabao 12 ya ligi kwenye mechi chache zaidi, lakini hakuweza kufikia idadi ya kutengeneza mabao kama ya Mata msimu uliopita.
Mata aliwatengenezea wachezaji wenzake wa Chelsea jumla ya nafasi 95, wakati Rooney alifanya hivyo mara 49 tu kwa msimu mzima.

Wachezaji wote wawili msimu uliopita, walicheza kwenye nafasi moja kati ya tatu zilizonyuma ya mshambuliaji na walikuwa muhimu sana kwenye mafanikio ya timu zote msimu huo wa 2012-13.
Japokuwa, Rooney hakutawala vyombo vya habari kama alivyofanya Robin van Persie pale Man United, alikuwa na nafasi muhimu kwenye kikosi cha Sir Alex Ferguson kilichorudisha taji la ligi kuu Old Trafford.

Mata pia alimfunika Rooney lilipokuja suala la kugombea mipira, alishinda mipira hiyo kwa asilimia 55 wakati, Rooney kwa asilimia 41 na hata kwenye kupiga pasi zilizofika Mata aliongoza pia, alipiga pasi zilizofika kwa asilimia 85, huku Rooney akifanya hivyo kwa asilimia 83.
Kama ukipewa jukumu la kuchagua mchezaji na baada ya kuona takwimu hizi ni wazi kabisa Mata atakuwa chaguo la kwanza. Amethibitisha ubora wake kwamba ni mchezaji mzuri na mwenye tabia nzuri. Pia ana miaka miwili chini ya Rooney.

Hakuna sababu ya msingi kwa Jose Mourinho kumtoa kafara staa huyo, lakini hili linaweza kubadilika kutokana na nia ya dhati ya Mreno huyo kumpata Rooney.
Takwimu zinaonyesha wazi kwamba, Mourinho atachemsha kwa kumtoa Mata na fedha kwa ajili ya Rooney, huku Man United wakilamba dume kutokana na ukweli kwamba, Rooney ameshaonyesha nia ya kutaka kuondoka Old Trafford huku timu hiyo bado ikihitaji kiungo fundi kumchezesha RVP.
Lakini kwa upande wa pili wa shilingi, baada ya kumuona Mata akicheza pambano la juzi dhidi ya Aston Villa na mfumo unaotumika na Mourinho kwa sasa, hata kama akibaki kwenye timu hiyo hatafanya vizuri kama msimu uliopita.

Inaonekana kama Mourinho ameamua kuimarisha zaidi pembeni, hivyo ile nafasi ambayo Mata alikuwa nayo ya kucheza huru haitakuwepo tena na Chelsea kwa sasa inahitaji straika wa kweli, kutokana na Fernando Torres, Demba Ba na Romelu Lukaku kushindwa kuongoza mashambulizi ya timu hiyo.

Hivyo ujio wa Rooney kwenye timu hiyo hautatumika kama kiungo bali atakuwa straika namba moja wa timu, kitu ambacho kitaongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji ya timu hiyo na kuifanya kuwa moto zaidi.

Man United wanaweza kufaidika zaidi kwa kumtoa Rooney na kupata fedha na Mata, Mhispaniola huyo ataweza kuziba pengo la Rooney kwenye idara ya utengenezaji, lakini kama siku RVP akiumia watapata tabu sana mtu wa kucheza mbele na umuhimu wa Rooney utaonekana hapo.

Kwa kifupi uhamisho wa wawili hao ni sawa na biashara kichaa kwa timu zote mbili kwa sababu kuna mawili wote wanaweza kulamba dume au kuchemsha au mmoja kuchemsha na mmoja kulamba dume.

No comments:

Post a Comment