Zungu ataka vijana watumie teknolojia vizuri




 SPIKA wa Bunge, Mussa Zungu amewataka vijana watumie vizuri muda na teknolojia wapate maendeleo. 

Zungu alisema hayo katika Maadhimisho ya Maulid Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Dar es Salaam juzi usiku.

 Alisema Dira 2050 imewagusa vijana na wanapaswa kuitumia fursa hiyo kujenga maisha yao na taifa kwa ujumla. Zungu alisema katika dira hiyo vijana wamepewa fursa waweze kunufaika na matunda ya maendeleo yanayolengwa. 

Alisema mitandao ya kijamii imekuwa ikitumiwa na baadhi ya watu kupoteza muda, kusambaza taarifa za uongo na za upotoshaji badala ya kuitumia kuzalisha kipato na kukuza uchumi. 

Aliwataka vijana kutumia teknolojia kutangaza biashara zao, kufanya huduma za usafirishaji na kuongeza wigo wa mapato na kueleza kuwa amefurahishwa na kaulimbiu ya Maulid Kitaifa 2026 inayosisitiza tabia njema na matumizi sahihi ya teknolojia. 

“Ni ujumbe mkubwa sana kwa Watanzania ambao kwa asilimia kubwa sasa hivi tunapoteza muda kutumia mitandao badala ya kuzalisha uchumi, tunatumia mitandao kutoa taarifa nyingi za uongo ambazo ni za upotoshi na za kuumiza na kuumizana wananchi wetu hapa Tanzania,” alisema Zungu. 

Alisisitiza watumie mitandao hiyo kutangaza biashara na si kutumia katika vitu ambavyo havina tija. “Niombe sana vijana, bodaboda, sio lazima ungoje abiria, weka uaminifu na duka la spea. 

Mtu hana sababu ya kutoka Temeke aje mjini kutafuta spea, mchukulie spea yake baada ya kuchukua abiria, unaongeza jitihada za mapato yako kwa ubunifu wa kuweza kufanya kupeleka spea, chakula na vitu mbalimbali,” alihimiza.


No comments