MWANARIADHA SISILIA PANGA ANG’ARA BRAZIL, ATWAA DHAHABU
Mwanariadha nyota wa
Tanzania, Sisilia Panga, amehitimisha mwaka 2025 kwa kishindo baada ya kunyakua
medali ya dhahabu katika mbio maarufu za barabarani za Sao Silvestre Road
zilizofanyika Desemba 31 jijini Sao Paulo, nchini Brazil.
Katika ushindi huo wa
kihistoria, Sisilia alitumia dakika 51 na sekunde 08, akiwagaragaza wanariadha
mashuhuri duniani na kuonesha uvumilivu wa hali ya juu pamoja na mbinu za
kipekee zilizomuweka kileleni mwa ushindani huo mkubwa.
Mafanikio haya ya
Sisilia Panga yamezidi kuimarisha hadhi ya Tanzania katika ramani ya riadha
kimataifa, ikithibitisha kuwa ni chimbuko la wakimbiaji wa mbio ndefu wa daraja
la kwanza.
Akizungumzia
mafanikio hayo, Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Rogath Stephen,
alimpongeza Sisilia kwa nidhamu ya hali ya juu na kujituma kulikopelekea
ushindi huo mnono. Alieleza kuwa mafanikio hayo ni mfano wa kuigwa kwa
wanariadha wengine wanaochipukia nchini.
Rais huyo wa RT
alitumia fursa hiyo kuwataka wanariadha nchini kuongeza bidii katika mazoezi na
kudumisha nidhamu binafsi, akisisitiza kuwa uzalendo na fahari ya kulilinda
jina la taifa ni nyenzo kuu za mafanikio kimataifa.
Ushindi wa Sisilia
Panga nchini Brazil unakuja kama medali nyingine ya dhahabu ya kihistoria kwa
taifa ndani ya mwaka 2025. Mafanikio hayo yanafuatia hatua nyingine kubwa
iliyofikiwa na Alphonce Simbu, ambaye aliandika historia kwa kuwa Mtanzania wa
kwanza kushinda medali ya dhahabu ya dunia katika mbio za Marathon jijini
Tokyo, Japan.

Post a Comment