BONDIA FRANK SHAGEMBE ATWAA MKANDA WA AFRIKA (WBO)
Bondia
Frank Shagembe kutoka mkoani Mbeya ameandika historia mpya katika medani ya
ngumi nchini baada ya kutwaa mkanda wa Afrika wa WBO katika pambano la
kusisimua la Knockout ya Mama msimu wa saba.
Shagembe alifikia
mafanikio hayo kwa kumtandika mpinzani wake, Haruna Osumanu kutoka nchini
Ghana, katika pambano lililofanyika juzi kwenye viwanja vya Posta Kijitonyama
jijini Dar es Salaam.
Akizungumza
kwa kujiamini mara baada ya kutangazwa kuwa bingwa, Shagembe alieleza kuwa
mpinzani wake alishindwa kuhimili kasi na uzito wa ngumi zake, hali
iliyompelekea kuhitimisha pambano hilo mapema kabla ya raundi zote kumalizika.
Bondia huyo
alisisitiza kuwa licha ya kuwa na mwili mdogo ukilinganisha na Osumanu, hakuwa
na hofu yoyote kwani alijiandaa vyema chini ya benchi lake la ufundi na kupata
usimamizi madhubuti kutoka kwa uongozi wake wa Mafia Boxing Promotion.
Shagembe
alibainisha kuwa ushindi huo ni utimilifu wa malengo aliyojiwekea kwa asilimia
100 kabla ya kupanda ulingoni. Akizungumzia mustakabali wake, aliahidi kufanya
makubwa zaidi huku akitamba kuwa kwa sasa hakuna bondia nchini anayeweza kumudu
makonde yake, akidai kuwa mabondia wengi wamekuwa wakimkwepa ulingoni.
Aidha, bondia
huyo alitumia fursa hiyo kutoa shukrani za dhati kwa Rais Samia Suluhu Hassan
kwa jitihada zake kubwa za kukuza sekta ya michezo nchini.
Usiku
huo wa Knockout ya Mama ulikuwa na mfululizo wa matokeo ya kusisimua ambapo
Yusufu Changarawe alimshinda Abdul Kisenga na kutwaa mkanda wa ubingwa wa Taifa
wa TPBRC, huku Amiri Matumla naye akijitwalia mkanda wa TPBRC kwa kumpiga
Sebastian Bau.
Katika mapambano
mengine, Yohana Mchanja alimchakaza bondia kutoka Ufilipino, Renz Rosia, wakati
Asemahle Wellem akijihakikishia ubingwa wa WBO Afrika baada ya kumshinda
Emmanuel Martey.

Post a Comment