Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Wednesday, August 30, 2023

BMT YAVUNJA UONGOZI WA TAFF, YATEUA KAMATIYA MUDA

 

Peter Sarungi aliyetenguliwa TAFF

Na Rahel Pallangyo

BARAZA la Michezo la Taifa (BMT),limevunja uongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu kwa watu wenye ulemavu Tanzania (TAFF) na kuteua wajumbe wa kamati ya muda itakayosimamia shughuli za shirikisho kwa muda wa siku 90 tangu leo.

Uongozi wa TAFF waliondolewa madarakani ni Peter Sarungi (Rais) na  Moses Mabula (Katibu Mkuu).

Katika taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano inasema BMT imevunja uongozi huo kwa mamlaka lililopewa na Sheria ya Baraza la Michezo la Taifa Sura ya 49 pamoja na kanuni za Baraza la Michezo la Taifa na kanuni za usajili namba 442 za mwaka 1999.

“Kamati hiyo itaundwa na Vincent Kaduma  (Rais), Athuman Lubandame  (Makamu wa Rais), Iddi Lulida  (Katibu Mkuu), Robert Manyerere  (Naibu Katibu Mkuu) na Leonard Liunda  (Mweka Hazina),” ilisema taarifa hiyo.

Aidha katika kipindi hiki cha siku 90, kamati teule inapaswa kuratibu marekebisho ya Katiba ya Shirikisho, kuratibu usajili wa wanachama, kuratibu mchakato wa Uchaguzi Mkuu, kusimamia shughuli zote za shirikisho katika kipindi chote cha uteuzi na kuunda kamati nyingine ndogo za kuwawezesha kutekeleza vizuri majukumu yao.

Kuvunjwa kwa uongozi huo kumetokana na kukizana na makubaliano yao na serikali ambapo jana uongozi wa TAFF walizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam kuwa timu ya Taifa ya soka ya watu wenye ulemavu ‘Tembo Warriors’, iko kwenye hatihati ya kwenda kushiriki mashindano ya African Para Games yanayotarajiwa kufanyika kuanzia Septemba 3 hadi 12 jijini Luanda, Ghana kwa sababu hawana fedha za kupeleka timu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Said Yakubu alisema walikubaliana na TAFF wasipeleke timu kwenye mashindano hayo badala yake serikali itaanda timu kwa ajili ya mashindano ya Afrika (CAAF) ya kufuzu fainali za dunia yatakayofanyika Novemba mwaka huu.

 “Mashindano haya tulikubaliana nao wasiende kwa kuwa kuna mashindano makubwa zaidi yanakuja ambayo tungeanza na kambi kabisa. Wameshazungumza na Baraza la Michezo Tanzania (BMT). Hiyo nyingine sasa sijajua wanatoa wapi,” alisema Yakubu.

Naye Katibu Mkuu wa BMT, Neema Msitha alisema serikali haijatoa pesa ya kambi kwa ajili ya timu hiyo hivyo haiwezi kugharamia kupeleka timu ambayo haijaandaliwa kwenye mashindano.

“Tulikubaliana kwa vile kuna mashindano mawili mwaka huu na yamefuatana katika kipindi kifupi sisi tutapeleka timu kwenye mashindano ya Afrika ya kufuzu fainali za dunia, hivyo haya tulikubaliana hatutapeleka timu,” alisema Neema.


No comments:

Post a Comment