Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Sunday, April 16, 2017

ONYINYE NDIDI NI N'GOLO KANTE MPYA LEICESTER


Image result for n'golo kante

LICHA ya kufanya vyema kwenye msimu ambao uliwapatia Leicester ubingwa wa England, ni wachache waliomzungumzia Onyinye Wilfred Ndidi.
Hii, kwa kiasi kikubwa, ni sababu ya kuwapo kwa kiungo mwingine, N’Golo Kante, aliyekuwa injini ya timu hiyo kabla ya kununuliwa na matajiri wa London, Chelsea.
Kundoka kwa Kante kumefungua mlango wa dhahabu kwa Ndidi, ambaye sasa anawika King Power Stadium, tena akionesha uwezo wa kumzidi Kante.
Ligi Kuu ya England (EPL) ina vipaji muhimu na adimu, na ni kama hivi vinavyokua sasa, baada ya kusajiliwa hapo kutoka Genk kwa pauni milioni 15 Januari.
Huyu ni mchezaji wa kimataifa wa Nigeria ambaye kwa bahati mbaya ya Leicester, tayari ameanza kuhusishwa na uhamisho kwenda ama Manchester United au Arsenal, kutokana na mfuatano wa mechi alizoonesha kiwango cha hali ya juu.
Ukimwangalia vizuri utaona kwamba kuna maeneo hata anamzidi Kante, japokuwa wengi ukiwauliza hilo hawataki kusikia lolote juu ya kusema Kante yupo chini – ni mtu anayependwa sana, lakini huyu naye watampenda tu.
Kama Kante, Ndidi ana stamina ya aina yake na inayotakiwa EPL, huku akiwa hana woga kuingiza mwili wake mahali kwa ajili ya kutaka kuuchukua mpira kwa adui – hahofii kuumia, na haumii hovyo.
Alipofanya makabiliano 10 katika dakika 65 tu dhidi ya Liverpool, alifupisha mambo mengi yaliyomsababisha bosi Craig Shakespeare kumsajili baada ya kufukuzwa kazi kocha aliyewapa ubingwa, Claudio Ranieri.  Takwimu hizo zinakaribia zile za Kante ‘mharibifu wa ukweli’.
Uwezo wake wa kutoa pasi za uhakika ni mkubwa na jicho kwa mpira, hasa anapotoka mbali, na hili ndilo limekuja kubadili mwelekeo wa Leicester kuanzia alikoachia Ranieri, anayeziba ombwe la Kante ni Ndidi.
Mwanasoka huyu anasema kwamba amekulia kwenye mazingira magumu ya kijeshi jijini Lagos na anaamini hali hiyo ndiyo imempaisha hadi kufikia  kuja kumshika mweusi mwenzake, Kante, japo huyu wa pili anatoka Ufaransa.

Anasema akiwa maeneo hayo ya kambi za kijeshi, alikuwa na nguvu na uwezo wa kukimbia, ambapo baba yake aliyekuwa mwanajeshi hakutaka awe mwanasoka, hivyo alifurahi sana alipopelekwa kwenye operesheni za kulinda amani.
Hakutarajia angekuwa katika kikosi cha kwanza cha timu inayocheza EPL hata kidogo, kwa sababu mipango yake haikwenda vyema awali. Ilikuwa Julai 2015, miezi sita ya mwanzo ya Ndidi huko Genk akiwa kana kwamba hayupo; ikawa ngumu sana chini ya kocha Alex Mcleish.
Kuwasili kwa kocha mpya, Peter Maes kulibadili mazingira na fursa za Ndidi, akaanza kufanya vyema, hasa kwenye mechi ya kwanza dhidi ya OH Leuven na timu nyingine kubwa kama mabingwa Gent.
Anasema kulikuwa na shinikizo kubwa juu yake, akiwa na umri wa miaka 18, pasipo na uzoefu wowote mkubwa.
“Nilikuwa na wasiwasi mkubwa na sikuweza hata kutoa pasi vizuri, nilipelekwa kwenye nafasi mpya na kocha hakuwa aina ya wale ambao hutulia, anabwatukia kila mchezaji na baada ya nusu ya kwanza akanitoa uwanjani. Mapumziko tu!
Anasema baada ya hapo alikaa benchi mechi kadhaa, lakini akajifua sana na aliprudi tu, nyota ikawa imewaka tena na baada ya kuhamia Leicester, ni tegemeo kubwa na tishio kwa wachezaji wa timu pinzani.
Alianza kuonesha vitu adimu, na sasa Leicester wanasema hawajutii kuondoka kwa Kante, japokuwa tena wana shinikizo juu yao, kutokana na klabu kubwa kumtolea macho ili wamchukue.
Ana sifa ya kufunga mabao machache, lakini akifanya hivyo ni kwa staili ya aina yake, na alifanya hivyo kwenye mechi ya Kombe la FA dhidi ya Derby County, akaonesha tena dhidi ya Stoke kwa mpira wa mbali, aina ya mchezo inayoonesha kwenda kinyume na umri wake mdogo.

Imewachukua mabingwa watetezi hawa miezi sita kupata mtu wa kuvaa viatu vya Kante, laiti Ranieri angemuona Kante alipoondoka, basi si ajabu wangetetea taji lao, maana sasa wako vyema, lakini muda umewatupa mkono, kwani wameachwa mbali sana na timu nyingine.
Ndidi ana umri wa miaka sita pungufu ya Kante na amenunuliwa kwa pauni milioni 17, akiwafaa sana, akicheza kwenye timu iliyokuwa ikipambana kuepuka kushuka daraja hadi wiki chache zilizopita.
Anakataa kujifananisha na Kante, au kuzungumzia juu ya kufananishwa huko akisema:“Naweza kujiona mwenyewe kama mimi tu, iwe watu wanasema kwamba nacheza kama Kante au ni mzuri kuliko yeye au yeye mzuri kuliko mie siwasikilizi, ninachotaka ni kucheza tu na kuzidi kuboresha kiwango changu, kufanya kazi kwa bidii ndilo lengo langu kwa sasa.
“Sie tunafanya yale mambo ya msingi, na mie hupenda kuwa na mawazo, imani na nguvu ya kushinda siku zote, nikifanya kazi na wenzangu kitimu kuliko kuwaza na kusimulia nacheza kama nani.”
Baba yake alikuwa akienda kulinda amani kwenye nchi kama Sudan pamoja na maeneo yaliyochafuka ya kaskazini mwa Nigeria mara kwa mara, na Ndidi alifurahi babaye alipoondoka.
“Nilikuwa nafurahi sana alipoondoka kwa sababu hakutaka nicheze mpira, bali nitie juhudi shuleni. Kila akiondoka nilijisemea sasa ni wakati wangu wa kucheza hasa,” anasema.
Zilikuwapo timu rasmi zilizopangwa za wajeshi, kuanzia chini ya umri wa miaka 10 hadi za wakubwa, hivyo akiwa tineja alionwa na Nduka
Ugbade, aliyekuwa nahodha wa Nigeria kwenye mechi za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) U-16.
Alikuwa miongoni mwa waliokuwa mabingwa 1985 na sasa alikuwa kwenye kambi za kijeshi akifundisha soka. “Nadhani nilichokifanya naye ilimaanisha kwamba nilikuwa na nguvu kuliko watu walivyotarajia niwe nazo nilipokwenda kukabiliana nao uwanjani,” anasema.
Anakumbukia aina ya mateso aliyopata, ikawa kama adhabu kwake kwenye jeshi, kumbe ilikuwa ni kipaji kinafinyangwa na Ugbade.
Alipata nafasi Akademia ya Nath Boys, moja ya shule za soka zinazothaminiwa zaidi jijini Lagos na ni hapo jitihada za Ugbade za vipindi vya mazoezi zilipozaa matunda.
Ndidi akiwa na umri wa miaka 16, Nath Boys waliingia kwenye mashindano yaliyoshirikisha timu 40 na ilikuwa akademia dhidi ya timu za wakubwa hata kutoka Ligi Kuu ya Nigeria.
Kati ya maskauti waliokuwa wakifuatilia mashindano hayo ni Roland Janssen, enzi hizo akiwa Genk na sasa anafanya na Manchester United.
Anasema ushawishi wake kwenye soka na nafasi hiyo ni kumtazama Nahodha wa Chelsea, John Terry, akatwaliwa na Genk, akaingia kwenye timu ya taifa ya vijana na sasa yupo na ya wakubwa, huku klabu kubwa kabisa Uingereza zikimtazama.

No comments:

Post a Comment