Blogroll

KWA MAWASILIANO ZAIDI TUWASILIANO KUPITIA BARUA PEPE pallangyorachel@yahoo.com AU NIPIGIE KUPITIA NAMBARI 0715187511

Pages

Tuesday, March 28, 2017

TAIFA STARS YAENDELEA KUWAPA RAHA WATANZANIA





TIMU ya soka ya Taifa, Taifa Stars leo imeendeleza wimbi la ushindi baada ya kuifunga Burundi mabao 2-1 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
Huo ni ushindi wa pili kwa Stars katika mechi za kirafiki za kimataifa baada ya mwishoni mwa wiki iliyopita kuifunga Botswana mabao 2-0.
Mabao ya Stars jana yalifungwa moja kwa kila kipindi kupitia kwa wachezaji Simon Msuva na Mbaraka Yusuf.
Msuva ndiye aliyeanza kuandika bao la kuongoza katika dakika ya 20 akiunganisha pasi ya Ibrahim Ajibu na kuachia shuti lililomzidi mlinda mlango wa Burundi, Nahimana Jonathani.
Bao hilo liliiamsha Burundi ambayo nayo ikaanza kufanya mashambulizi na dakika ya 31 nusura mshambuliaji Laudit Mavugo aandike bao, lakini akiwa kwenye nafasi nzuri ya kufanya hivyo shuti lake lilipaa juu na kufanya Stars kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao hilo.
Mavugo aliisawazishia Burundi bao katika dakika ya 54 akitumia vema makosa ya kipa wa Stars, Deogratius Munishi ‘Dida’ aliyeacha lango ambapo Mrundi huyo alimwahi na kuujaza mpira wavuni.
Bao hilo lilidumu kwa dakika 24 tu kwani Yusuf aliiongezea Stars bao la pili katika dakika ya 78  akiunganisha pasi ya Ajib na kuachia shuti ambalo liligonga mwamba na mpira kumrudia kabla ya kuuwahi na kuuweka kimiani.
Ushindi huo, Stars imelipa kisasi kwa Burundi ambayo ilicheza nayo mwaka 2014 na kufungwa mechi zote.
Kocha Mkuu wa Stars, Salum Mayanga aliitumia mechi hiyo kuangalia kikosi kitakachocheza mechi za kuwania kufuzu Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani (Chan) zinazotarajiwa kuchezwa baadaye mwaka huu.

No comments:

Post a Comment